Author :
Dr. Y. Salim
Date:
Sat, 05 Feb 2000
Subject:
KATIBA SI MSAHAFU
Wa-Bara wanakemea
Hivi karibuni maoni tofauti yenye kuunga mkono au kupinga urekibishaji wa
Katiba ya Serikali ya Zanzibar yamesikika. Kauli kali kali zimetolewa
kushambulia matayarisho hayo ya ubadilishaji wa Katiba ya Zanzibar. Watu
wanaotambulika na kuheshimika kama akina Jaji Warioba wamesikika wakitoa
maoni yao dhidi ya mpango huo na hadi kuufananisha na usultani. Wataalamu
wengine wameuita udikteta na un´gan´ganiaji wa madaraka. Ndugu zetu wa
Bara
wamechukua jitihada kubwa kuweka maoni yao wazi na yasikike pembe zote. La
muhimu zaidi mara hii Wana-CCM wa Bara nao wamejitokeza hadharani na
kusambaza barua walizomuandikia Dr. Salmin Amur Juma (SAJ), Rais wa
Zanzibar.
Moyo, Diria na Ali Ameir
Kwa upande wa Zanzibar akina wanasiasa wakongwe kama vile Hassan Nassor
Moyo kaweka mawazo yake dhidi ya mapendekezo hayo bayana kabisa. Ingawaje,
Moyo
kwa muda mrefu sasa haishi tena Zanzibar na ni siri ya wazi kwamba Moyo na
Dr. SAJ ni paka na chui. Nyuma ya mgongo wa Hassan Nassor Moyo kuna akina
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania Ali Ameir na Balozi Hassan Diria,
kwa upande wa wale wana-CCM wa Kizanzibari walioko Bara. Kwa pamoja hawa
wamekuwa
wakipanga mikakati ya siri ya kumpindua Dr. SAJ. Aliyeweza kujitokeza kati
yao kuonekena na kusikikana hadharani ni Moyo, yeye hana cha kuogopa tena,
tonge yake imekwisha salimika na hamtegemei Dr. SAJ kwa njia yoyote.
Balozi Diria ameonyesha hamu na shauku yake kubwa ya kutaka kuwania au
kugombania
cheo cha Urais wa Zanzibar, lakini baada ya kuona kwamba Dr. SAJ bado
anakitaka kiti chake ikabidi Mtukufu Balozi Diria arudi nyuma kidogo na
kuingia mvunguni. Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya ndani yeye amejigeuza
muitikiaji dhikiri angurumae ndani kwa ndani bila ya nini anachokiitikia
kujulikana. Ukoko wa CCM-ZNZ wanamjua vizuri msimamo wake na kujua kwamba
siku atakayo anguka Kingi, yeye ndiye atakae kuwa wa mwanzo kusema "the
King is dead, long live the King", na atahakikisha kwamba Kingi
anapoanguka
atajiweka mbali sana ili shina na matawi yasije muangukia.
Dr. Omar apiga mbizi
Oktoba inakaribia, wengine wameona uchaguzi unapiga hodi, kama kampeni
sija
fanya sasa basi naweza kuchelewa kibweni au kwa maneno ya leo kuchelewa
n´gambo ya pili. Kwa kiwango fulani Dr. SAJ ameweza, akin´gan´gania mpini
na kuachia wenziwe washike pakali, kwa siku zote kutimua timua mambo
Zanzibar na
kwa kiwango fulani kuweza kuwaziba midomo maadui zake. Kwa upande wa CUF,
amewatia ndani viongozi wake na kufanya harakati za CUF kwa kiwango
kikubwa
kushughulikia kesi ya "uhyena" na kupoteza lengo la kampeni za uchaguzi na
ujenzi wa maendeleo ya nchi kwa jumla. Lakini mashine ya Dr. SAJ
haikuwashughulisha wana-CUF tu, bali mitambo iliwakumba hata wale viongozi
wa
Zanzibar ambao walikuwa na ndoto ya kuuchuchumilia Urais wa Zanzibar. Hali
hii ilimlazimisha mtu kama Makamu wa Rais Dr. Omar Ali Juma (Dr. OAJ)
kufanya
kampeni ya kupiga mbizi bila ya kuthubutu kuibuka. Kwa hivyo kampeni yake
ikawa inadunga vile vikundu fulani vya jamii ambavyo, yeye mwenyewe, Dr.
OAJ,
alijuwa kwamba siri yake hawataifichua. Katika kampeni hii fedha nyingi
zimemtoka Dr. OAJ katika kulishia-lishia, hasa kwa watu binafsi ambao kwa
mfano walifikwa na maafa, kama vile kufiwa au wale waliokuwa wamekabiliwa
na matumizi makubwa kama vile harusi n.k.
Dr. Omar mtoto wa Butiama
Dr. OAJ si mwana siasa lakini ni mtu Wazanzibari wanaeweza kumwita
juttarr.Yaani mjanja, rogi bila ya watu kuweza kuchukizwa na urogi wa aina
hiyo, lakini tatizo ni kwamba Dr.OAJ, alivuka mipaka kwa wale wanaoujua
uchungu wa wana-AfroShirazi wakitoneshwa. Pale alipoingilia kati kuhusu
kutiwa sahihi suala la "Muwafaka", na hadharani kuja kuwafunza na
kuwaadhiri Wana-Afro wenziwe. Kwa hilo hawakuweza kumsamehe wala hakuweza
kusamehewa
pale alipouweka Muungano mbele ya Zanzibar. Na ndio maana pale alipokwenda
Bara kushika cheo cha Umakamu wa Rais, wenziwe walipumua na kusema muache
atoke na kutokomea.
Zaidi ya hayo kilichowachukiza Wazanzibari kwa jumla na sio CCM-ZNZ tu ni
pale alipopendekezwa na Nyerere kuwa ndio mrithi wa Salmini Zanzibar.
Suala
muhimu halikuwa kuwa atawekwa kwenye kiti cha Dr. SAJ au la. Suala muhimu
likiwa ni kwa nini Nyerere alimchagua yeye awe mtawala wa Zanzibar, kwa
nini
awe yeye? Na kwa nini hasa Nyerere awachagulie Wazanzibari nani awaongoze
au awe Rais wao.
Madhambi ya Nyerere
Hali hii ilitokana na sababu mbili muhimu, moja ikiwa pale Nyerere
alipoilazimisha Zanzibar, eti kwa kipengee cha kuvunja Katiba ya
Muungano,
kujitoa katika Jumuiya ya Waislaam wa Ulimwengu. Hapa Wazanzibari
walihisi
kwamba, Katiba ni Nyerere na Nyerere ni Katiba. Sababu nyengine muhimu
ambayo
imekuwa ikitokota ndani kwa ndani katika nyoyo za Wazanzibari ni pale
walipoanza kutambua kwa uwazi zaidi kwamba Nyerere alijishirikisha kwa
kiwango kikubwa sana kuwanyima Waislaam wa Tanganyika haki sawa. Hili
lilikuwa ni pigo kubwa mno kwa Wazanzibari kutambua, hasa kwa wale
waliokuwa wakimpenda Nyerere, wawe ni wapinzani au wana-CCM, kwa sababu
karibu
Wazanzibari wote ni waislaam. Kwa hivi sasa, kwa sababu ya vitimbi vya
Nyerere Wazanzibari wengi zaidi wanauona Muungano, sawa na U-Nyerere
yaani
upikaji majungu dhidi ya uislaam. Vile vile ilipodhihirika kwamba Rais
Mkapa kwa kutumia Uhariri wake wa Magazeti wakati huo, alikuwa ni upondo
wa kidau
cha Nyerere, ikawa sasa Mkapa nae hapendezi Zanzibar.
CCM-ZNZ walioko Bara
Kwa hivyo kumkumbatia Nyerere na sasa Mkapa kumemuweka Dr. OAJ pahala
pabaya katika nyoyo za Wazanzibari, ingawa inawezekana angelikuwa mgombea
bora wa
CCM-Zanzibar. Ujuttarr na ulaghai wake Dr. OAJ ungeliweza kumpeleka mbali
kama bahati ingelikuwa upande wake. Lakini tatizo liliopo ni kwamba nae
hivi karibuni kajitia katika kundi la wana-CCM wanaombwekea Dr. SAJ. Kuna
wale
walio karibu na hatamu za utawala wanao amini kwamba Dr. Omar
asingethubutu
kusema alivyosema kama Mkapa hakumbonyeza.. Inamkinika asemayo Dr. Omar
yakawa ni ya kweli, na yale wanaosema akina Moyo, Diria, Ali Ameir yakawa
nayo ni sahihi, lakini Wazanzibari wanauliza, jee, haki za kibinaadam na
za
kidemokrasia ya Zanzibar zinajulikana na kutambulika pale tu wanapowania
nofu
la Urais wa Zanzibar? Zaidi kuna uhakika gani kwamba hao wanaoshutumu leo
wasingelifanya kama hayo au akhasi ya hayo kama wao wangelikuwa na hatamu
za utawala. Kama kweli hawa wana uchungu na Wazanzibari kwa nini sauti zao
hazijasikikika zikiitetea Zanzibar kabla ya hapa? Ali Ameir akiwa ni
Waziri
wa usalama mwenye uchungu na Wazanzibari, mwenye uchungu na haki za
binaadam na demokrasia, kwa nini akawa amrisha askari polisi na FFU kwenda
kuwapiga
raia marungu, isitoshe akazidi kupeleka askari kutoka Bara kwenda
kuangamiza raia wasio na silaha wala hatia. Kwani adui wa Ali ameir ni
nani? Ni Salmini na katiba yake au ni wavunja haki za binaadamu na waponda
ponda demokrasia?
Kwa hivyo ikiwa Katiba itabadilishwa isibadilishwe, kwa maslahi ya hawa
waliotajwa hapo juu, wao wasiwe na tamaa yoyote. Afadhali wanyamaza kimya
kuwaiga akina Amani Karume ambao wanaweza kuwa na uwezekano wa kumuangusha
Salmini kuliko wale waliokuwa Mrima.
Haki za binaadam hazikuvunjwa leo tu
Tukiwawacha viongozi wa CCM wa Kizanzibari walio kuwa Bara, kuna wale
Wabunge
waliomuandikia Dr. SAJ wakitarajia kumbadilisha mawazo Raisi wa Zanzibar.
Mhesh. Jaji Warioba ni mmoja kati ya wa mwanzo kujitokeza hadharani na
kupinga azma na njama za Dr. SAJ na kutosita kufananisha hatua hiyo kuwa
sawa
na usultani. Maneno mazito kutoka kwa Mtanzania Mzito. Lakini basi, hivyo
kweli katika historia yetu ya karibuni hatuja wahi kuona utawala
uliofanana
au kupitilia huo tuitao usulatani Tanzania? Ikiwa usultani una maana ya
utawala wa mabavu, udikteta, utawala wa kuamua mambo kibinfasi, ulio
pungufu kidemokrasia na ulio na sifa za uvunjaji wa haki za kibinaadaam
basi usultani
Tanzania haujamalizika januari 1964, kwani watu wakitiwa ndani bila ya
kupelekwa mahakamani, watu wakiteswa vizuizini na wengine hata kupoteza
maisha yao. Tanzania bado haijayakemea maovu hayo hadharani, maovu ambayo
yakitokea Bara na Zanzibar. Wanasheria wasifika bado hawajaweza kujitokeza
kwa uwazi kulaani kubaguliwa kwa Waislaam katika Tanganyika tokea
kupatikana uhuru wa Tanganyika. Hali hiyo ya kuyakemea mabaguzi kama hayo
yanahitaji
ujabari na imani safi ya kumtetea yoyote yule anaekandamizwa bila ya
kujali
imani ya kidini, kisiasa, kikabila au kirangi. Baadhi yetu bado tunasubiri
kulaaniwa kwa kitendo cha CCM cha kumvua Alhaji Jumbe Urais wa Zanzibar na
bado tunasubiri kulaaniwa kwa kitendo cha kuwafukuza akina Seif Shariff
kutoka katika CCM. Viongozi wa CCM wawache mtindo wa kumlaumu na kulaani
maovu ya Dr. SAJ na wakati huo huo kuyanyamazia maovu ya Nyerere.
Kosa la Salmini ni kutikisa kibiriti
Mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar tumekuwa nao tokea oktoba 1995, jumia ya
madola imekuwa ikienda mbio kujaribu kusuluhisha, lakini ni CCM hii hii
ambayo ikijaribu kukokota miguu kama wenye magonjwa ya matende ya miguu
ili
kuchelewesha mapatano. Muwafaka umetiwa sahihi kijanja janja na hata hivyo
huajatekelezwa hadi leo. Wafadhili nao wamekuwa wakijaribu kujishughulisha
na
matatizo ya Zanzibar na kufikia hadi ya kuizuiliya Zanzibar misaada.
Viongozi
wa CUF wamekuwa kizuizini kwa sasa zaidi ya miaka miwili. Mtiririko wa
mambo yote haya yametokea na viongozi wa CCM wa Bara, Wataalam wa Sheria
wa Bara na
Warioba wameyanyamazia. Leo, kwa sababu, Salmini anataka kubadilisha
Katiba
waheshimiwa wote hao wamekuja juu na kumkemea Salmini, na yote nini
sababu?
Hakuna jengine isipokuwa kwa sababu Salmini ameparaganya mipango ya
Watawala wa Dodoma ambao walikuwa wameshawapangia Wazanzibari nani
awatawalie. Hasira za CCM-Bara sio kwamba Salmini anabadilisha Katiba, au
si kwamba Zanzibar
kuna mgogoro wa kisiasa au sio kwamba viongozi wa CUF wanaadhibiwa kwa
sababu
ya maoni na msimamo wao wa kisiasa, wala sio kwamba Wazanzibari wasio
hatia
wamepigwa marungu bure siku ya kesi ya "uhyena". La, kosa ni kwamba
Salmini
kaamua kuwatikisia kibiriti na kuonyesha kwamba yeye anajitambua kwamba ni
Raisi wa Zanzibar na Zanzibar ni Dola, Nchi na Taifa kamili lisilokubali
kuendeshwa kutoka Dodoma. Salmini kawaweza kwa kuwa hawawezi kumtimua kama
alivyotimuliwa Jumbe na Seif Shariff kwani yeye yutayari kuifufua ASP.
Katiba si mshahafu - Mkapa hashindi 2000
Katiba si msahafu, inaweza kubadilishwa, pale wakati na mahitaji yanapo
lazimu. Kwa Katiba ya Zanzibar ni Wazanzibari ndio wenye haki pekee ya
kuibadilisha au kuirekibisha Katiba yao. Watanganyika, majirani wengine au
watu wengine wa nje wanaweza kutoa maoni yao lakini hawana haki ya
kushiriki au kushirikishwa katika uundaji, ubadilishaji au urekibishajiwa
Katiba ya
Zanzibar. Ni Wazanzibari ndio ambao wataamua kuwa urekibishaji maalum au
unaohusika wa Katiba ni wenye lengo la kibinafsi au wenye maslahi na umma.
Katiba ya Zanzibar ni Katiba ya Zanzibar na Katiba ya Muungano ni Katiba
ya
Muungano, hili lazima wabunge wa Bara walitambue na kuliheshimu. Wabunge
wa
CCM, Wanasheria na Watawala wa Bara hawawezi kulinyamazia kimya suala la
kurekibisha Katiba ya Muungano, kitendo ambacho kina lengo la
kumhakikishia
Mkapa ushindi na kwa wakati huo huo kuzidi kumpa madaraka ya kuweza
kukandamiza upinzani. Utafiti tofauti ukiwemo za CCM-Bara umeonyesha wazi
kwamba katika raundi ya kwanza ya uchaguzi wa Rais wa Muungano, Mkapa
atashinda kwa kiwango kidogo sana, yaani baina ya asilimia tano hadi saba
(5-7%), wakati katika raundi ya pili ya uchaguzi wa Rias wa Tanzania Mkapa
atashindwa vibaya sana kwa vile upinzani utakuwa na mtetezi mmoja tu. Kwa
hivyo inatufanya wengine tuamini kwamba, kama inavyosemekana, lengo la
kubadilisha Katiba Zanzibar na Bara halina tofauti, yote ni kwa madhumuni
ya kumuendeleza Rais anaetawala abaki madarakani. Sasa kwa nini Mkapa
aruhusiwe na Salmini apingwe ? Tukiliwachilia mbali hilo na
kujishughulisha na siasa za
ndani za CCM-Bara, imedhihirika wazi kwamba pindi pakiwa na upigaji kura
huru
Mkapa hawezi kukubaliwa kusimamia Urais na wajumbe wenzake wa Bara na ndio
maana akawa amejaa tele katika mfuko wa Salmini, siku mfuko huo
utakapotoboka, ole wake Mkapa. Haifiki miezi sita tokea Mkapa kushindwa
katika uchaguzi wa ndani ya Chama na kubidi kulishia mapesa chungu nzima
na
kutumia vitisho ili wajumbe wamuungwe mkono, donda la Mkapa bado
halijapona
na linauma bado.
Kamati Kuu ya CCM
Katika hotuba ya sherehe za Mapinduzi za mwaka huu, 2000, Dr.Salmini
alifoka bila ya kuchokozwa na kutishia kwamba yoyote yule atakaeleta fujo
au vurugu
basi atapambana na kali ya dola, na hakuta kuwa na huruma. Kwa wakati huo
hakukuwa na sababu yoyote kwa Dr. SAJ kusema hivyo kwani Wazanzibari
walikuwa
wanaendelea kama tabia yao ya desturi kuwa ni wavumilivu na kuwa wa pole.
Na CUF kuendelea na msemo wao kuwa " wako tayari kuinunua amani kwa bei
yoyote" na ndio maana ingawa viongozi wao wametiwa vizuizini kwa zaidi ya
miaka
miwili, wafuasi wa CUF hawakufanya fujo au ghasia yoyote. Kwani Dr. SAJ
alipokuwa akitoa onyo hilo Wabunge wa CCM-Bara walikuwa wapi ? Kwani
hotuba
hiyo ilitolewa kwa kichina au kiswahili ? Hivyo kweli hawakufahamu Dr. SAJ
alikuwa ana jaribu kusema nini kwa matamshi hayo ambayo hayajashokozwa au
kusababishwa na chokochoko yoyote? Hivyo ilikuwa hawajui kama Dr.SAJ
alikuwa anajitayarisha ikibidi kutumilia kipengee cha Katiba pale ambapo
upinzani
ungechokozwa na kuchokozeka na kuanza kuingia katika ghasia ? Hivyo
hawajui
kwamba Rais wa Zanzibar anaweza kutumia kipengele cha vita katika Katiba
ya
Zanzibar na kuendelea Uraisi wake na kuzuia uchaguzi ? Hivyo hawazijui
zile
mbinu tofauti zilizotayarishwa, kama moja haikufaa kutumika nyengine, ili
mradi Katiba ipigwe chenga? Mbinu hizi zote zimeshafika katika Kamati Kuu
ya CCM na zimepelekwa kwa muda mrefu. Sasa ikiwa hali ni hiyo kwa nini
Wabunge
wa Bara wakasubiri muda wote huo na ndio kwanza leo kujitokeza ati
kuwaombea viongozi wa CUF waachiwe na ati Katiba isibadilishwe. Siku zote
hizo walikuwa
wapi?
Wazanzibari wote waamue
Kama ilivyo Katiba ya Bara si Msahafu basi Katiba ya Zanzibar nayo si
Msahafu. Mabadiliko na marekibisho ni mambo ya lazima na yanayo wahusu
Wazanzibari pekee. Lakini urekibishaji wa Katiba utakikanao ni ule utakao
kuwa wa haki na wa halali na wa kuondosha vipengere vyote vilivyo dhidi na
maslahi ya Wazanzibari. CCM-ZNZ wametuambiya kwamba ni wananchi, yaani
Wazanzibari ndio wanao yataka mabadiliko hayo, kwa hivyo wengi wape. Ikiwa
ni
Wazanzibari wote, yaani CCM-ZNZ na Upinzani pamoja wanataka hivyo, basi
wananchi lazima wapewe haki hizo za kujiamulia Katiba yenye mfumo gani
wanaitaka, na Wazanzibari wote washiriki kikamilifu bila ya uoga, vitisho
na bila ya mapendeleo yoyote na maamuzi hayo kusimamiwa na wale wasio
fungamana na upande wowote. Wazanzibari wooote wapewe haki ya kutoa maoni
yao huru
kuhusu kipengele cha kumzidishia muda zaidi ya vipindi viwili Rais wa
Zanzibar. Wazanzibari wapewe haki ya kuamua kuwa Rais awe au asiwe anateua
Tume ya Uchaguzi na wasimamizi wa uchaguzi. Kuteua Mhakimu au kutoteua.
Awe
na nguvu zaidi au asiwenazo. Aweze kushitakiwa au asiweze. Wazanzibari
wapewe haki ya kuondosha vipengere vinavyowanyanganya haki za Kidola, za
kuwa
na Nchi na Taifa huru. Wazanzibari wapewe haki ya kurekibisha Katiba ya
Muungano kwa yale yenye faida au hasara ya Zanzibar na kuirejesha Katiba
ya
Muungano ili ihudumie yale mambo kumi na moja tu (11) yaliokubaliwa katika
Katiba Mama ya Muungano, wakati ikirejeshea Zanzibar haki zake za kuwa na
Rais Kamili, Bendera , Wimbo wa taifa, Nembo na Katiba huru ya Zanzibar.
Haya yanaweza kupitishwa kihalali pekee kwa kutumia njia ya kura ya maoni
itakayo simamiwa na wasimamizi huru..
Wasalaam
Dr. Yussuf S. Salim.