Author :
Dr. Y. Salim
Date:
Tue, 25 Jan 2000
Subject:
KISUKARI KWA MTU WA KAWAIDA 1
Muongozo kwa wagonjwa wa kawaida wa Ugonjwa wa kisukari
Utangulizi
Mara nyingi inakuwa ni vigumu kuwa mgonjwa katika nchi zetu za kimasikini
kutokana na sababu mbali mbali, moja wapo ya sababu hizo ikiwa ni upungufu
wa
mtu wa kawaida wa kupata taaluma ya siha ya kimsingi kinyume na zile nchi
zilizo endelea.
Madhumuni ya maelezo haya mafupi ni kujaribu kuwa funua macho wagonjwa wa
kawaida kuhusu kujipatia ujuzi wa magonjwa ili hatimae waweze kufahamu
sababu
za magonjwa tofauti, kuweza kujikinga na kufuata miko matibabu
itakikanavyo.
Kwa kuanzia nitatoa makala tatu zote zikilengwa kwa wagonjwa na wale
wafanya kazi wa siha ambao hawashughulikii ugonjwa wa kisukari kila siku
pamoja na
kuwalengea wale ambao wanawatayarishia maakulati wagonjwa wa kisukari na
ukoo
wa wagonjwa hao kwa jumla ambao watafaidika na ujuzi wa chakula cha siha
bora. Ni muhimu kujua kwa kila mtu, hasa wale jamaa mlio huko ghuba na
makanzu yenu yanayo ficha matumbo, kwamba mkipunguza utumiaji wa mafuta,
siagi, samli na margarini katika chakula na kwa wakati huo huo mkafanya
riadha, mtaweza kupunguza uzito na kwa mara nyingi mtaweza kuepuka na
kupanda
kwa kiwango cha sukari katika damu. Kwa wale wengineo katika ukoo kula
chakula bora kutawakinga na magonjwa ya kisukari na magonjwa ya
moyo-na-mishipa-ya-damu.
Muongozo huu wa mwanzo utashughulikia ugonjwa wa kisukari kwa jumla na
baadae
kujaribu kuchambua aina tofauti za kisukari.
Nini ugonjwa wa kisukari ?
Tunapokula chakula, sukari kutokana na chakula inaingia kwenye damu.
Insulin huisaidia sukari kutoka kwenye damu na kuiingiza kwenye mfano
musuli, pahali ambapo sukari hutumiwa kama ni nguvu (energy). Kiwango cha
sukari katika damu
ni 3-7 mmol/l (54-126mg/dl).
Ikiwa sukari haiwezi kuingia katika mfano musuli, basi sukari hujirundika
katika damu. Hapo sukari katika damu hupanda na ikiwa itapimwa mara kadhaa
kila asubuhi kabla ya chai ya asubuhi na kuonekana kuwa iko zaidi ya 6,7
mmol/l (121mg/dl) basi hapo mtu husemekana kuwa na kisukari.
Kuna aina tatu za kisukari
Aina ya 1: (type 1) mtu huwa hafanyi insulin. Hali hii zaidi huonekana
baina ya watoto na vijana (zamani ikijulikana kama insulin dependent
diabetes
mellitus- IDDM).
Aina ya 2: mtu anaweza kufanya insulin, lakini huwa haitoshi, na huwa
haifanyi kwa kasi sawa na wale watu wasio na kisukari. Sababu kuu ya hali
hii, ni kwamba mtu huwa ana mashahamu mengi tumboni au kitambini/vitambini
na
kwa wakati huo huo huwa hafanyi riadha ya kutosha (zamani ikijulikana kama
non-insulin dependent diabetes mellitus-NIDDM).
Kisukari cha waja wazito (Gestational diabetes) huchomoza wakati wa mimba,
na
ili kulinda mtoto tumboni mara nyingi inabidi mja mzito apewe insulin ili
sukari ya damuni iwe baina 4-8mmol/l. Ikiwa mja-mzito atakuwa na sukari
nyingi damuni akiwa na mimba, kutakuwa na uwezekano mkubwa kwamba, mtoto
atazaliwa na athari tofauti.
Kisukari kinazidi Zanzibar
Ingawa sina takwimu za karibuni kuhusu kisukari huko Zanzibar lakini, ni
siri
ya wazi, kwamba idadi ya watu wenye kisukari ya Aina ya 2 wameongezeka
mara
dufu. Hali hii inatokana na upungufu wa wataalamu wa kutosha wa magonjwa
haya, upungu au bei za juu za madawa haya, mabadiliko ya malaji, umasikini
na
upungufu wa mipango maaluum kwa upande wa serikali. Sio masikini tu
waliokumbwa na ugonjwa huu bali hata wale wanaoishi Mazizini, Mbweni,
Mombasa
na kwengineko kunakoishi wanaojiweza nao wamekumbwa. Kwa kawaida kila pale
penye mzazi mmoja mwenye kisukari watoto 2 kati ya 5 wana hatari ya
kupata
kisukari.
Watoto khususan wana hatari ya kurithi upungufu wa kasi ya kazi ya insulin.
Hata ikiwa wazazi wamepata kisukari baada ya kuwazaa watoto wao, wazee
tayari wanakuwa wameshawarithisha watoto wao hatari ya upungufu wa kasi
hiyo.
Ingawaje, kisukari bila ya shaka kinaweza kukingika, yaani mtu asipate
ugonjwa, ikiwa mtu atajikondesha kwa kula chakula bora na kufanya riadha.
Ikiwa mmoja kati ya wazazi ana kisukari, inatakiwa wale watoto wakubwa
wapimwe sukari katika damu asubuhi kabla hawakula kila baada ya miaka
miwili.
Sukari na shahamu katika damu zinaambatana
Ikiwa sukari katika damu itakuwa iko juu kwa muda mrefu, shahamu katika
damu nayo itapanda.
Kisukari kwa hivyo ni ugonjwa wa kisukari na wa kishahamu
Kiwiliwili kina athirika ama ikiwa sukari itakuwa imepanda au shahamu
itakuwa
imepanda katika damu. Haya mambo mawili yanaleta matatizo kama yale ya
magonjwa ya moyo (heart attack), kiharusi (stroke) kupungua kasi ya macho
(hatimae upofu), magonjwa ya mafigo, upungufu wa usambazaji wa damu na
kupungua kuhisi miguuni (wengine hadi ya kuungua bila ya kuhisi) hali
inaweza
kusababisha kukatwa vidole, sehemu ya nyayo na miguu (Seyyid Abdulla Bin
Khalifa). Zaidi ya hayo kasi za udume za mwanamume hupungua.
Chakula bora chenye shahamu kidogo, riadha na hatimae dawa vinaweza
kupunguza
idadi ya sukari na shahamu katika damu ikawa ya kawaida. Hali hii
inamfanya
mtu ajihisi vizuri kiakili na kuweza kuishi maisha mazuri na ya kawaida.
Upimaji wa sukari damuni
Kwa wale wenye uwezo ni jambo la maana kununua mashine ya kupimia sukari
damuni au vituo vya siha viwe na mashine angalau mbili ili moja itaweza
kui
chunga nyengine ikiwa ina fanya makosa ya kupima hasa pale vifaa vikiwa
vimekwisha muda au kuathirika kwa sababu hii au ile. Angalia ! upimaji wa
damu ni muhimu sana.
Pima damu yako mara moja kwa wiki kabla hujanywa chai ya asubuhi na saa
moja na nusu baada ya kunywa hiyo chai.
Mapendekezo ya viwangovya sukari damuni:
-4-7 mmol/l (72-126 mg/dl) kabla ya chai/chakula cha asubuhi
-si zaidi ya 10 mmol/l (180 mg/dl) saa moja na nusu baaba chakula cha
asubuhi
Kama sukari yako damuni iko juu zaidi, ni muhimu kwamba, unaji shajiisha
zaidi kupunguza kiwango cha sukari damuni. Wasiliana na tabibu wako,
ukihisi hufanukiwi
Riadha
Riadha inaleta siha njema ya akili na kiwiliwili. Fanya ile riadha
uipendayo mwenyewe. Wakati una kisukari, ni lazima ufanye riadha ambayo
inaambatana na mwendo wa miguu wa mchapuo muwafaka kwa kiasi cha saa
moja.
Faida ya riadha
-unakusaidia kupunguza uzito
-insulin yako itafanya kazi bora
-viwango vya sukari na shahamu katika damu vitaanguka
-moyo utapata nguvu - kwa hivyo kuweza kujikinga na heart attack
-presha itashuka
Matibabu ya dawa
Kama riadha na chakula bora havisaidii itabidi kutumike dawa za aina ya
vidonge au insulin.
Shahamu nyingi kwenye damu inatibika kwa vidonge, riadha na chakula bora.
Tabibu wako ataamua aina gani ya matibabu utahitajia.
Ni muhimu kwamba unatumia dawa zako kila siku ili dawa ziweze kufanya kazi
yake barabara. Insulin haina gelatine na kuna patikana vidonge bila ya
gelatin.
Inaendelea
Chakula cha kila siku
Inafaa tukumbuke tena kwamba ugonjwa wa kisukari ni ugonjwa wa shahamu
vile
vile.
Mtu anaweza kuendelea kula chakula chake cha kawaida ili mradi anakumbuka
kwamba ni suala muhimu sana kupunguza utumiaji wa mafuta, siagi, samli na
margarin.
Mtindo wa kumimina mafuta moja kwa moja katika sufuria au kikaangio si
mtindo
wa busara hata kidogo. Ni jambo la maana na busara kutumia kijiko cha
kulia
katika kupima kiasi gani cha mafuta mtu anatia katika mapishi: hakikisha
kwamba unatia kijiko kimoja cha kulia kwa kila mtu mmoja katika ukoo.
Chakula cha kuchemsha ni cha siha zaidi kuliko cha mikaango kwa sababu ya
upungufu wa mafuta.
Afadhali kula chapati/mkate wa kusukuma wa ngano nzima upikwao mkavu bila
ya mafuta kushinda ule unaokaangwa kwa mafuta.
Epuka pilau na wali wa nazi na afadhali ule wali wa maji.
Hakikisha kwamba unaitoa, kuikeketa na kutupa shahamu yote ya nyama kabla
hujaitia chunguni.
Idadi ya milo ya kila siku
Si busara kula rundi la maakulati bora kupendelea kula milo midogo midogo
ya mara kwa mara. Njia hii inasaidia kupunguza uzito wa mtu vile vile na
kuifanya insulin kufanya kazi kwa kasi au bora zaidi.
Tahadhari na kukwepa chai au mlo wa asubuhi kwa vile unahitaji kuanza siku
ukiwa na chochote tumboni. Baada ya mlo wa asubuhi unaweza kuendelea kula
mara mbili zaidi kwa kutwa ikiwa umezoea kula hivyo. Lakini hakikisha
kwamba unakula kiwango kidogo kidogo, tofauti na ulivyozoea. Kula ndimba
kubwa kubwa
asoruka paka hazina tija kwa siha yako.
Inawezekana kuwa huna njaa baina ya nyakati za kula, lakini inafaa
utambuwe
kwamba ni vyema ukila vitu vidogo vidogo vikavu kama ya ngano nzima na ule
pamoja na tunda moja. Ulaji huu wa udoho udoho utakufanya usiwe na njaa
kali wakati wa milo mikuu na kwa hivyo utakula kidogo zaidi.
Matunda
Matunda ni chakula bora, lakini mengi yao yana sukari nyingi, kwa hivyo ni
vizuri kula si zaidi ya mawili-matatu kwa siku ukihakikisha kupunguza
ulaji
wa zabibu, embe, ndizi mbivu, matunda makavu kama tende, zabibu kavu,
zeituni
kwa vile matunda haya yana sukari nyingi.
Maziwa na mitindi
Maziwa yana sukari-ya-maziwa (lactose) , kwa hivyo mtu anahitajiwa asinywe
zaidi ya nusu liter kwa siku, hii ina maana maziwa ya aina mbali mbali
kama
mtindi na yoghurt bila ya matunda.
Vidonge vya utamu haviathiri kiwango cha sukari katika damu kwa hivyo mtu
anaweza kutumia vidonge hivi kwa kutayarishiya maakulati badala ya kutumia
sukari ya kawaida. Vidonge hivi viko vya aina tafauti kwa mfano saccharin
(sakkarin), cyclamate, acesulframe, aspartame (Nutra-sweet) n.k.
Cyclamate na acelsulframe zinaweza kuchemshiwa bila ya kuharibu ladha.
Nutra-sweet inapoteza ladha yake tamu ikiwa itachemshwa au kubekiwa kwa
zaidi
ya dakika chache. Sakkarin inageuka kuwa chungu ikiwa itachemshwa zaidi ya
digrii 70 kwa muda mrefu.
Epuka na vitu vilvyo tiwa ladha ya utamu kwa matumizi ya sorbitol na au
fructose kwa vile vina ongeza sukari katika damu.
Inafaa mtu anywe vinyaji vilivyo punguzwa utamu au kutiwa utamu wa vidonge
yaani vinyaji bila ya sukari. Hakikisha kusoma kama sharubati fulani ina
sukari au haina sukari.
Epuka na vyakula vya utamu-utamu kama vile haluwa, jelebi, laddu-laddu,
peremende-pipi, asali, matunda ya kuchemsha, jamu, makeki-keki, kashata
n.k. na ujizoweshe kula vyakula visivyo vitamu tamu.
Mboga-mboga ni vyakula bora na haziongezi sukari katika damu :
mabilingani,
mabamia, vitunguu, squshi, kebeji, kerot, tungule/nyanya, tango,
koliflower, fiwi, kisambu, mchicha n.k.
Njegere, kunde, mbaazi, maharage, njugu mawe, muhogo, ndizi mbichi,
majimbi, viazi vikuu ni vyakula vyenye mizizi mizizi ambavyo vinateremsha
sukari
katika damu. Tahadhari na ndizu mbivu, za mkono wa tembo, boga na viazi
vitamu.
Ukila chizi hakikisha kwamba haijajaa shahamu yaani iwe ya kiasi cha 18%
ambayo itakuwa na shahamu ya kiasi cha gramu 18 kwa kila gramu 100 za
chizi. Kwenye pakiti unaweza kusoma kiasi cha asili mia cha shahamu kwenye
chizi.
Samaki ni wenye manufaa makuu kisiha na aina zote zinaruhusiwa
Usile mayai zaidi ya 2-3 kwa wiki.
Wasia wa Chakula bora
Punguza utumiaji wa mafuta, siagi, samli na margarini
Kula udoho udoho na viwango vidogo vidogo
Kula mboga mboga kwa wingi, ama za kuchemsha au mbichi
Kula vyakula vya mizizi mizizi
Kula vyakula vyenye ngano nzima na chapati za ngano nzima
Pale inapomkinika soma kwenye paketi/chupa kuhusu kuwemo au kutokuwemo
sukari ndani
Maakulati/machopo chopo
Ikiwa mtu atafuata mapendekezo ya hapo juu, anaweza mara 1-2 kwa mwezi
kula
maakulati kama vile kwenye shughuli, maaliko, sherehe yenye vyakula
vyenye
mafuta/siagi na sukari kwa wingi.
Mengineyo
Matatizo
Baadhi ya nyakati mtu anaweza kufikwa na maafa kama misiba, matatizo ya
kifamilia n.k. Na kwa hivyo mtu hupendelea kujiliwaza kwa kula zaidi au
kupoteza hamu ya kula kabisa. Hali hizi zina athiri ugonjwa wa kisukari na
kwa hivyo mtu inambidi aendelee na kula kama ilivyopendekezwa ingawa mara
nyengine inaweza kuwa ni vigumu.
Magonjwa mengine
Hutokea kwamba mtu anapata magonjwa mengine juu ya ugonjwa wake wa
kisukari, anatakiwa aendelee na matibabu yake ya kisukari kama kawaida. Na
anategemewa apime sukari katika damu mara kwa mara zaidi kuliko kawaida
kwa vile magonjwa
mengine yanaweza kuifanya sukari ikapanda zaidi ingawa matibabu
yanaendelea
kwa kawaida. Kwa hivyo kumbuka kuwasiliana na tabibu wako pindi sukari
ikipanda.
Safarini
Jambo la mwanzo kumubuka kuchukuwa dawa yako na kipima sukari chako.
Ramadhani
Ikiwa unapata insulin na kisukari chako kina matatizo kurekibishika ni
bora
uepuke na kufunga
Ingawaje ikiwa unahisi uko timamu na umedhibiti utibabu wa kisukari chako
unaweza kuendelea na kufunga. Ikiwa unakula vidonge, ingefaa kuvila baada
ya futari na kwenye daku. Inayumkinika kwamba dozi ya dawa zako
ikabadilika kwa hivyo wasiliana na tabibu wako.
Macho
Nenda kwa mganga wa macho mwaka mara moja, ambae atachunguza hali ya ndani
ya
maicho yako kwa kutumia kama kijidarubini. Ikiwa kwa muda mrefu sukari
yako
imekuwa juu katika damu, inawezekana ukatoka damu kutoka mishipa ya damu
ndani ya jicho na kutawanyika ndani ya jicho. Ikiwa hali hii haijatibiwa
mapema inaweza kusababisha upofu !!!!
Viganja vya miguu (feet)
Mara kwa mara wagojwa wa kisukari watapata vidonda katika viganja/nyayo za
miguu kati ya wale wenye kisukari. Kuna hatari kwamba vidonda havitapona
ikiwa vitapuuzwa, kwa hivyo chukua hadhari kubwa na vidonda hivyo.
Unapopata kidonda nyayoni/miguuuni kiangalie kidonda hicho kwa makini na
kama
hakiponi kama kidonda cha kawaida kwa muda wa siku chache wasiliana na
tabibu
wako haraka.
Unapo tawadha chunguza kama kuna alama ya wekundu-wekundu miguuni/nyayoni,
alama ambazo hatimae huweza zikawa vidonda, hususana kama viatu vina bana.
Sigara
Wavutaji sigara wameonekana kuwa na hatari ya kupata heart attack mara
tatu
zaidi ya wale wasio vuta sigara. Kwa hivyo kama unavuta, wacha kuvuta na
kama
huvuti usianze kuvuta.
Udume/Uume
Kati ya wanaume 6-8 katika wanaume 10 wenye kisukari cha aina ya 2 hupata
matatizo ya kupungua kasi ya uume ikiwa sukari damuni imekuwa iko juu kwa
muda mrefu. Usione haya, wasiliana na tabibu wako ambae atakushauri kuhusu
uwezekano tafauti wa matibabu.
Kumbuka kwamba una wajibu mkubwa na ugonjwa wako wa kisukari na wewe
mwenyewe
ndiye mwenye dhamana ya mwanzo kabisa na matabibu bila ya shaka matabibu
wako
wata kuwa tayari kukusaidia.
Ni matumaini kwamba mapendekezo haya yatakusaidia kudhibiti viwango vya
sukari na shahamu katika damu yako - kama vile vilivyodhibitiwa kabla ya
ugonjwa wako.
Mwisho wa sehemu ya kwanza
Wasalaam
Yussuf