Author :
Maalim Khamis
Date:
Tue, 29 Feb 2000
Subject:
SALMINI BADO ANA KETE
Wapendwa wananeti,
kwanza sina budi kuungana na umma wa wazanzibari wenzetu popote pale
walipo katika kuuunga mkono uamuzi muhimu kabisa kupata kutolewa na
halmashauri kuu ya CCM( kwa serikali zake tawala) kwa ajili ya manufaa na
maslahi ya wazanzibari. Busara kubwa iliyofanywa na Halamashauri hiyo baada
ya kuona kuwa hakuna njia yoyoye itakayomwezesha Salmini asimame kwa mara ya
tatu, zaidi ya ile ya ubabe na ghasia, ambayo ingeiletea Zanzibar maafa
makubwa. Hongera halmashauri kuu ya CCM kwa kuukubali ukweli huo kwa mara ya
kwanza katika historia ya Zanzibar.
Lakini kwa wakati huo huo, ninaunga mkono maoni ya Dk. Yussuf Salim
kuhusu hatma ya Salmin Amour. Itakuwa si busara kumdharau rais Salmin Amour
kwa wakati huu. Na vile vile itakuwa pia si busara kushadidia ripoti za
vyombo vya habari vya Tanzania bara dhidi ya Salmin. Kwani maslahi ya vyombo
vya habari hivi na washirika wao wa uongozi wa serikali ya Muungano sio
maslahi ambayo sisi wazanzibari tunayatarajia, yaani kupigania heshima ya
visiwa vyetu .
Yaliyotokea katika Halmashauri kuu ya CCM yanapaswa yawe funzo na onyo
kwa sisi wazanzibari, ya kuwa Dola, Nchi na Taifa huru ambalo sisi
tunalililia kila siku bado lina kazi ya kulitetea. Ukweli kwamba hatma ya
nchi bado inaamuliwa Dodoma, na ukweli kuwa rais wetu (hata iweje!)
anavyodhalilishwa pamoja na kuwa yeye anawakilisha maslahi ya wazanzibari
milioni moja, nchi mshirika sawa katika muungano, sio jambo la kushangilia
hata kidogo. Tujaribu kutofautisha safu za dhamana za kisiasa na watu wenye
dhamana hizo. Ni kweli kuwa Salmin Amour mwenyewe ndiye mhusika mkuu katika
mambo yote haya. Lakini ni wajibu wetu kulinda na kuheshimu na kutetea sare
zinazowakilisha utaifa wetu na utambulizi wetu.
Ninapendekeza tutoe mwito kwa wananeti na kumpelekea Rais Salmin Amour
ujumbe utakaomfanya afahamu kuwa sisi wazanzibari kila siku tumekuwa
tukimsihi atetetee maslahi ya wazanzibari wote kwa jumla na kutetea haki na
utaifa wa Zanzibar, na kuwa ikiwa sasa yeye amekwishafahamu, basi sisi
hatutamtupa kamwe katika kutetea maslahi ya utaifa wa Zanzibar katika
kurekebisha muundo wa Mungano wake ulio sasa na Tanzania Bara. Rais Salmin
bado anayo kete ya kucheza, sasa ni wakati bora kabisa wake yeye kujaribu
kuunganisha maslahi ya wazanzibari wote, bila ya kujali chama, au itikadi.
Ninatoa mwito kwa wenzetu wa CUF kumkaribia Salmin Amour kwa maslahi mya
wazanzibari wote. Inshallah, pengine matokeo ya mkutano wa Dodoma umekuwa
ndiyo njia ya kuleta mafahamiano baina ya wazanzibari wote. Tafadhalini
tusitupe nafasi hii. Inaweza ikafungua kurasa mpya ya maslahi ya wazanzibari
katika muungano.
Ikiwa Salmin Amour kweli anapigania maslahi ya wazanzibari wote, basi
atuonyeshe wazanzibari. Mwache aweke kando sakata za kisiasa baina yake na
CUF na amwalike Seif Sherriff Hamad katika mazungumzo ambayo, pindipo
yakitokea, basi huenda ikailetea zanzibar afueni mpya ya siasa.
Ninaomba tena kwa wazanzibari wenzangu. yaliyotokea Dodoma hayamgusi
Salmin Amour tu! Bali yanatugusa sote wazanzibari katika kutetea uhuru na
heshima ya visiwa vyetu.
Mungu Ibariki Zanzibar.