Author :
Harith Ghassany
Date:
Fri 7 Jul 2000
Subject:
MABADILIKO YA KWELI
Wapenzi Wana Zanzinet
Assalam Alaykum,
Sidhani kama yupo mkereketwa hata mmoja wa CCM/SMZ ambaye anaweza kukataa
kuwa SMZ/CCM imeshindwa kuyapatia ufumbuzi wa kudumu masuala yafuatayo
yanayolikabili taifa:
1. Kuondosha rushwa nchini na ubadhirifu uliokithiri.
2. Kuzoroteka kwa:
a. Huduma za afya.
b. Elimu.
c. Kilimo.
d. Umeme na maji.
e. Mahakama na uadilifu.
Pamoja na yote hayo, wakereketwa wa SMZ/CCM wanaamini ya kuwa ASP/CCM ndicho
chama pekee kilichowaletea Wazanzibari Mabadiliko ya Kweli ambayo ni
kuuondoa utawala wa kifalme wa kiomani Zanzibar.
Sina hakika kama wanachokichukia wakereketwa wa SMZ/CCM ni utawala wa
kidhalimu au mfumo wa kiutawala wa kifalme. Hawafahamu kama utawala wa
kijamhuri unaweza ukawa wa kidhalim zaidi hata kuliko wa kifalme na kuna
aina za tawala za kifalme ambazo ni za kidhalim zaidi kuliko tawala za
kijamhuri.
Jambo muhimu ambalo wakereketwa wa SMZ/CCM na CUF inafaa walizingatie ni
kuwa mapinduzi au mabadiliko ya kisiasa peke yake hayana nguvu ya
kukabiliana na matatizo sugu ya kiuchumi na kijamii.
Baada ya mauaji na utesaji wanamapinduzi wenyewe hujikuta wamekata tamaa na
kutambua kuwa walichokuwa wakikipigania hakijenda mbele hata hatua moja; na
si hivyo tu, wameyarudisha nyuma mapinduzi yenyewe! Sababu ni mbili.
Misingi ya umaskini na unyanyasaji ipo pale pale na inangojea mabadiliko
mapya kuirudisha katika hali ile ile ya kwanza ya kabla ya kufanyika
mapinduzi na pengine hata hali ya kabla ya mapinduzi inakuwa ni vigumu
kuifikia.
Sababu ya pili ni madhila na mateso ambayo yanavunja yote yalio ya
kiungwana, yanajenga chuki ndani ya nyonyo za wananchi na kusababisha
wabadilishe msimamo wao kutoka kuyaunga mkono mapinduzi na kumuunga mkono
yoyote atakayewaahidi atawaletea mabadiliko ya kweli, ikiwa kweli au hata
ikiwa ni porojo tu la kujipatia madaraka.
Kwa sababu tafauti chama cha CUF kimeshindwa kuja na ushahidi au rekodi
yoyote kwa wapiga kura katika uchaguzi ujao wa Oktoba kwa njia ya kuonyesha
kimeweza kuleta mabadiliko ya kweli katika kuyapatia ufumbuzi hata kama ni
mdogo katika midani za:
1. Kuondosha rushwa nchini na ubadhirifu uliokithiri.
2. Kuzoroteka kwa:
a. Huduma za afya.
b. Elimu.
c. Kilimo.
d. Umeme na maji.
e. Mahakama na uadilifu.
Tumeona Hizbu Allah ya Lebanon. Hawana serikali mikononi mwao lakini wana
kila aina ya huduma za jamii kuanzia mahospitali, maskuli, na mengi
mengineyo. Vyama va upinzani Egypt vilifanya kazi kubwa sana kuwasaidia watu
waliokhasirika wakati Masri ilipopigwa na mtetemeko wa ardhi hata ikawa aibu
kubwa juu ya serikali.
Bila ya kuyapuuza mateso na madhila ya SMZ/CCM dhidi ya CUF, zipo sababu
nyengine ambazo zimekifanya chama cha CUF kisijishughulishe na kueneza
huduma za jamii Pemba au Unguja kabla ya kuingia Ikulu?
Pamoja na yote hayo wafuasi wa SMZ/CCM wanaamini ya kuwa CCM ndicho chama
pekee kilichowaletea Wazanzibari Mabadiliko ya Kweli. Wafuasi wa CUF pia
wanaamini ya kuwa chama cha CUF ndicho chama pekee kitakachowaletea
Wazanzibari Mabadiliko ya Kweli.
Haya ni masala ya imani kuwa CCM imeshafeli na ushahidi upo; CUF
haijajaribiwa kwa hivyo inafaa ipewe fursa halafu ihukumiwe.
Let us wait and see.
Wenu,
Harith Ghassany