Author :
Farouk Abdulla Amour
Date:
Thu, 29 Jun 2000
Subject:
UHURU NA UMOJA/UMOJA NA UHURU
Sheikh Machano,
Assalaam Alaaykum,
UHURU NA UMOJA/UMOJA NA UHURU
Kwanza ni wajibu wangu kukushukuru kwa kunizinduwa, kuzinduwana ni wajibu
wetu. Ni ndivyo kabisa ya kwamba wazee wetu wakati wa kuwania Uhuru kutoka
kwa Muingereza ilikua kauli yao ni “UHURU NA UMOJA”. Ama maelezo yangu kwa
mie kusema “UMOJA NA UHURU” badala ya “UHURU NA UMOJA” ni kufuatana na
msingi ule ule wa lengo kuu la tangu kuasisiwa Umoja wa Zanzibari – Zanzibar
Nationalist Party – (ZNP), au kama inavyojuulikana na wengi wetu – Hizbu,
lengo lilojengeka katika nguzo mbili muhimu nazo ni:
1. UHURU
2. UMOJA
Umoja wa Wazanzibari (Hizbu) umejengeka katika nguzo mbili hizi kwa imani
yake kuwa matengenezo yote ya nchi yamefunganika na mawili haya, yaani bila
ya Uhuru na Umoja hapana maendeleo yoyote yale. Uhuru ni lazimiko la maisha
kwa kutengeneza nchi, vile vile Umoja ni lazimiko la maisha katika
kutengeneza nchi. Mawili haya ni ya lazima kupatikana kwa matengenezo ya
nchi, moja pekee haliwezi kusaidia katika matengenezo ya nchi. Ni vidole
viwili, kimoja hakivunji chawa.
UHURU MWANZO
Kama tunavyofahamu kuwa: “politics is the art of possibility”. Kutokana na
hali hii ni busara kurekibisha tanga kufuatana na upepo, lakini sio
kubadilisha safari na makusudio kwa kufuata upepo au kukimbia mawimbi.
Unabadilisha mbinu kulingana na hali lakini hubadilishi makusudio kwa
kisingizio cha hali.
Wakati wa kuwania Uhuru kutoka kwa mtawala wa Kiingereza ilitangulizwa Uhuru
kwa imani ya kwamba Uhuru ndio ufunguo na nyenzo ya kuleta Umoja wa
Wananchi. Mkoloni alikuwa mbioni kuwagawa wananchi, kwa hivyo kuweza
kujenga Umoja wa Wananchi ilikuwa ni muhimu na dharura kuung’oa utawala wa
kikoloni. Utawala wa Kiingereza ulikuwa ni afadhali kuliko mtawala wa leo.
Utawala wa Kiingereza ulikuwa una demokrasia, kulikuwa na magazeti nchini,
aliruhurusu vyama vya siasa; pia aliruhusu harakati za kuwania Uhuru ili
kumtoa yeye mkoloni. Kutokana na hali hii ilidhihiri la mwanzo na la haraka
ni kudai Uhuru na kumng’oa mtawala ili tuweze kujenga na kudumisha Umoja wa
Wananchi. Kutekeleza hili ndio sauti zikawa UHURU NA UMOJA, imetangulizwa
UHURU kwa umuhimu wake wakati ule.
UMOJA MWANZO
Baada ya kuvamiwa nchi yetu na kutiwa chini ya utawala wa mwalimu kwa
kisingizio cha muungano ilidhihiri ya kwmba la mwanzo ni UMOJA. Mtawala wa
leo – mwalimu (unyerere) ni muovu zaidi kuliko mtawala wa jana – Muingereza.
Mtawala wa leo ni dikteta wa hali ya juu kabisa. Mara tu baada ya
kuivamia nchi yetu na kuitia chini ya utawala wake alivifunga vyama vyote
vya siasa na jumuia zote zile nchi, ameyafunga magazeti na njia zote za
utangazaji zikawa chini ya hukumu yake yeye mtawala. Mtawala wa leo baada
ya kuwauwa wananchi kadhaa wa kadhaa wakiwemo viongozi wa ASP aliamua
kuifunga hata hii ASP, chama ambacho kimemsaidia kufikia katika utawala wake
huu muovu. Baada ya kutenda hivi mtawala wa leo alizidishi mbinu zake za
kuwagawa wananchi mafungu mafungu na kuwa mbioni kuwafarikisha kwa kila
mbinu. Kutokana na hali hii ilidhihiri kuwa la mwanzo na la haraka ni UMOJA
WA WANANCHI, kwa hivyo basi, ndio tunaposema “UMOJA NA UHURU”, tunatanguliza
UMOJA , kwa umuhimu wake hii leo. Haya ni kwa imani yetu sote ya kwamba
bila ya Umoja wa Wananci hatutoweza maisha kumng’oa huyu mtawala dikteta.
Nyenzo pekee ya kumng’oa mtawala dikteta ni Umoja wa Wananchi. Hakuna
nguvu yoyote ile itakayoweza kumng’oa mtawala dikteta isipokuwa Umoja wa
Wananchi. Bila ya Umoja wa Wananchi tutaendelea kufarikishwa baina yetu na
tutaendelea kutawaliwa kwa hivyo la mwanzo la dharura ni Umoja wa Wananchi.
HIZBU INGALIPO
Ni ndivyo iwapo nitajiuliza mbona kila mara ninataja Hizbu (ZNP), kwani hii
sio imepigwa marufuku na haipo tena? Nikijijibu suala hili nitasema kuwa
laa, Hizbu ipo wala hapigiki marufuku wala haifutiki. Hivi ni kwa sababu
Hizbu sio mtu wala watu, wala chama; Hizbu ni fikra, fikra za kizalendo.
Hizbu ni mimi, hizbu ni wewe na yeye na yule, sote sisi ndio Hizbu.
Kutokana na hali hii ndio ilivyo ya kuwa Hizbu haitokufa milele, na kama
wanavyosema wazee ya kwamba hata akibakia Muhizbu mmoja tu basi Inshallah
Zanzibar itatengenea – Amin.
TUWACHE MFARAKANO
Wazanzibari leo kilio chetu ni kimoja tu nacho ni UMOJA WA WAZANZIBARI,
kutokana na hili ndipo tunapowataka nduguzetu walioko katika uwongozi waache
kuleta sababu za mfarakano na tujenge Umoja baina yetu kwa maslaha ya nchi
yetu na vizazi vyetu. Adui mkubwa wa Zanzibar leo sio matawala mambo leo,
adui mkubwa wa Zanzibar ni yeyote yule mwenye kushirikiana na matawala
kuleta na kukuza mfarakano baina ya Wazanzibari. Yeyote yule mwenye
kusaidia kuleta mfarakano basi huyo ndio muovu mkuu wa Zanzibar na ni wajibu
wa Wazanzibari kumuepuka na kuwa mbali nae kwani huyo ni muovu menye
kupanda uovu. Ni wajibu wa Wazanzibari hivi sasa tukikabiliwa na uchaguzi
wa kuchaguwa Wawakilishi na Raisi, ni wajibu tuhakikishe kuwa mabwana
tutakao wachaguwa ni hakika wataleta Umoja wa Wazanzibari, kama tunashaka
juu ya hili basi bwana huyo hatufai, tusibahatishe; lakini ni lazima
tuhakikishe kuwa bwana tunaemchaguwa ataleta Umoja wa Wazanzibari. Katika
kuchaguwa hakuna kubahatisha kuna hakika, kwa sababu kura ndio nyenzo pekee
ya kutufikisha kwenye matarajio yet, kwa hivyo ni wajibu tuwe na hakika
kuwa kura zetu tunawapa mabwana wenye uwezo wa kutufikisha kwenye mahitajio
yetu. Mahitajio ya Mzanzibari leo ni moja nalo ni Umoja wa Wananchi.
Tafadhali tuwe na hakika – majuto mjukuu.
Vile vile tunapopima kuchaguwa tuhakikishe kuwa tunaemchaguwa anamjuwa
Mwenyezi Mungu Mtuukufu, anaujua mlango wa msikiti. Kumjuwa Mwenyezi Mungu
ndio kipimio kikubwa cha mwenye kufaa kubebeshwa dhamana ya uwongozi. Bila
ya kumjua na kumcha Mwenyezi Mungu basi kitu gani kitamzuia bwana baada ya
kupewe uwezo kutenda vile anavyopenda, hakipo hata kimoja. Kizuizi pekee ni
imani, sio nguvu zozote zile, bila ya imani hakuna kutekeleza majukumu ya
uwongozi. Kutokana na hali hii ndio maana mabwana waovu wanapotwambia kuwa
tusichanganye siasa na dini, yaani dini ndio imani, na bila ya imani ni
kuwa bila ya kizuizi cha kukulinda kutenda khiana na kuvunja amana na
ahadi. Kwa hivyo wanavyotaka wao ni kuwa hatuna imani ili tusitekeleza
amana. Tukimchaguwa bwana asiemjua Mwenyezi Mungu na kumpa amana basi sisi
ndio wakosa na hesabu ni juu ya shingo zetu. Sisi tuna dhamana na amana ya
vizazi vyetu, kwa hio ni lazima tutekeleza amana hii kwa kumuwakilisha bwana
muaminifu kutekeleza kwa niaba yetu wajibu wa dhamana tulizochukua sote
sisi.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu Mtuukfu atujaalie uwezo wakuchaguwa waongozi wema
ambao wataweza kutekeleza amana kwa niaba yetu – Amin.
Wa Billah Tawfiq
Farouk