|
Wanakumbi wenzangu, huu ni waraka
mpya uliotoka Rai toleo la Agosti 11. Kwa wale walio mbali na
gazeti hili, nufaikeni
nanyi.
Ahsanteni.
jabir+
Headline:Mwalimu
Nyerere, bado Rais atoke CCM tu?
Moja
ya masuala muhimu ya kinchi aliyoyazungumzia Rais Benjamin Mkapa
katika hotuba yake ya kufunga Bunge Julai 29, ni tatizo la rushwa.
Alieleza mengi ya kuonyesha hatua thabiti alizozichochea katika
serikali yake katika kupambana na tatizo hilo.
Maelezo
yake yalitanguliwa na maneno mazito: mojawapo ya mambo niliyosema
nitayavalia njuga nilipoingia madarakani ni vita dhidi ya rushwa.
Yapo mengine mengi, lakini wapo wanaotaka uongozi wangu
utathminiwe kwa kigezo kimoja tu cha rushwa, wakidhani sikutimiza
ahadi yangu. Si kweli. Rushwa bado ipo, kama ilivyo katika nchi
zote duniani kwa viwango tofauti, lakini katika miaka 10 iliyopita
tumefanya kazi kubwa sana kupambana nayo.
Kutoka
hapo, Rais anataja hatua yake ya kuunda tume ya kuchunguza mianya
ya rushwa iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba, ambayo matokeo
yake, anasema, ni kufanyika mabadiliko katika sera, miundo ya
taasisi na sheria ili kuziba mianya ya rushwa. Amezitaja sheria
sita zilizotungwa katika azma hiyo zikiwemo Sheria ya Maadili ya
Viongozi Nam. 5 na Sheria ya Ununuzi wa Vifaa vya Serikali Nam.3
zote za 2001.
Serikali
imeongeza bajeti ya Taasisi ya Kuzuia Rushwa (TAKURU) mara 600
kutoka sh milioni 15 za mwaka 1996/97 mpaka sh bilioni 9 mwaka
2004/05. Idadi ya watumishi pia imeongezwa wakiwapo 700 kutoka
185. Taasisi ina waendesha mashitaka na wapelelezi na imefungua
ofisi zake katika Mikoa yote na Wilaya 93 Tanzania Bara kusogeza
huduma karibu na wananchi.
Kwa
hiyo tumeongeza bajeti, tumepanua mtandao na tumeongeza uwezo wa
utendaji, yaani upelelezi, kuendesha mashitaka, kuhamasisha jamii
na kutoa ushauri kwa Serikali. Juhudi hizo za Serikali zimewezesha
kuchukuliwa hatua mbalimbali kwa waliojihusisha na vitendo vya
rushwa.
Ameendelea
akisema watumishi 456 wa umma walionywa au kukaripiwa kwa barua,
362 walisimamishwa kazi, 403 walifukuzwa au kustaafishwa kazi kwa
manufaa ya umma na 138 walifikishwa vyombo vya dola. Kuanzia mwaka
1995 mpaka 2004, tuhuma 11,434 ziliripotiwa TAKURU, kati yake,
9,891 zilichunguzwa. Tuhuma 975 zilipelekwa mamlaka husika ili
zichukue hatua, kesi 367 za rushwa zilifunguliwa mahakamani na 174
zimeamuliwa. Kwa kuwa mapambano ya rushwa si ya Serikali pekee,
TAKURU imeanzisha na kukuza ushirikiano na zaidi ya taasisi 16
zisizo za kiserikali.
Hizi
ni takwimu muhimu. Si tu katika kuona namna serikali
inavyoshughulikia tatizo la rushwa, bali pia kuwafahamisha
wananchi namna shughuli za serikali zinavyokwenda. Ni wajibu wake
Serikali kuwa wazi kwa wananchi inaowaongoza kwa sababu kama ina
nia nzuri, haina cha kuficha na Serikali iliyo wazi kwa wananchi
wake, inajiaminisha kwao. Huwa nikisema humu kwamba kujieleza,
tena mapema, huondoa shaka.
Rais
Mkapa amezungumzia suala hili la uwajibikaji kwa serikali kabla ya
kugusia suala la rushwa katika hotuba yake. Serikali inayojiamini,
na inayowajibika kwa wananchi, inakuwa wazi kwao. Haina sababu ya
kujificha. Kiongozi aliyejiridhisha kuwa jambo fulani ni la
manufaa kwa wananchi wake hana sababu ya kuogopa kuwa mkweli, na
kueleza kwa nguvu za hoja, kwa nini sera, mikakati na mambo fulani
ni ya lazima.
Wajibu
huo (wa Serikali kuwasiliana na wananchi), katika nchi ya
kidemokrasia, unatokana na haki ya wananchi kufahamishwa, na haki
yao ya kusikilizwa, kwa mambo yanayowagusa au kuwahusu. Wajibu huo
wa Serikali kuwa wazi kwa wananchi wake ni jambo la lazima kwa
Serikali ya Kidemokrasia, si jambo la hiari. Faida mojawapo ya
kuwa na Serikali iliyo wazi kwa wananchi ni kuimarisha dhana ya
uwajibikaji na nidhamu katika kazi za Serikali. Tumeanza lakini
bado safari ni ndefu. Wengine Serikalini bado wanadhani kila kitu
cha Serikali ni Siri Kali; hata madhambi yao yawe siri. Hayo ni
makosa makubwa, lakini itatuchukua muda kubadili fikra na mitazamo
ya kila kiongozi. Lakini lazima twende mbele, kamwe tusirudi
nyuma.
Serikali
ya Tanzania lazima iwe ya wananchi, inayotokana na ridhaa ya
wananchi, inayowajibika kwa wananchi, na isiyoogopa kuwa wazi
kwao. Kwa upana zaidi, tukijumuisha na wanasiasa, lazima sasa
tujenge uwezo si wa kuwa wazi zaidi tu, bali pia wa kuelekeza
siasa zetu kwenye mambo ya msingi na kutafuta ufumbuzi wa matatizo
ya wananchi.
Ajenda
mbili hizi ni nzito. Rais Mkapa ametusalimia Watanzania kwazo
akitukumbusha wajibu wetu, mtu awe ndani au nje ya serikali.
Uamuzi wake kushirikisha taasisi zisizo za kiserikali katika
mapambano ya rushwa, maana yake ni kutambua umuhimu wa sekta
nyingine zaidi ya Serikali katika kutekeleza majukumu ya
kuongoza.
Kazungumzia
Rushwa na Utawala Bora. Hii ya pili, kama ilivyo ya kwanza,
nimekuwa zikiijadili mara kwa mara katika safu hii. Ni jambo la
kufurahisha kiongozi wa juu kama Rais kujadili masuala haya kwa
sababu hali inazidi kuwa mbaya upande wa Zanzibar. Kila kitu ni
siri na kinafichwa. Hata shughuli za Serikali, nazo Siri Kali(SK).
Hata mradi wa Vitambulisho vya Wakaazi nayo eti siri. Kumbe hata
siri nayo hutoka wakati ukifika. Mradi uko kweupeni na wakuu
wanajitahidi kutumia fedha nyingi leo kuufahamisha kwa wananchi.
Bado kazi ipo.
Ndiyo
haya husema Utawala Bora si maneno matamu, ni vitendo na kuonyesha
ujasiri katika kutenda huko. Nakusalimia Dk. Mohamed Gharib Bilal
Mwenyezi Mungu akujaze kheri. Suala la nyumbani libaki kuwa la
nyumbani, lakini la Serikali, hapana; lazima wananchi
wafahamishwe. Wakishafahamishwa, na iwe mapema si magharibi
imeingia, watafahamu na haziji shaka tena kwa sababu ukieleza kitu
mapema unaziba mizaha na fununu. Usiposema unaitengeneza na
unachochea wananchi kuwa wakaidi. Waamini vipi wakati
hawakufahamishwa mpaka gazeti limeandika (si lazima iwe kwa
vitambulisho). Inasikitisha una serikali ambayo gazeti linaaminika
kulikoyo.
Rais
Mkapa anasema serikali ya kidemokrasia haiwezi kuogopa kuwa wazi.
Kwa hivyo anatuambia ya kwetu Zanzibar si ya kidemokrasia.
Uthibitisho mwingi. Si yenyewe tu, hata taasisi zake zikiwemo
zinazoambiwa zi huru kama Tume ya Uchaguzi (ZEC) inafanya mambo
sirini. Orodha za majina ya wapiga kura pia siri. Kwenye vituo,
majina wanasiasa wanasema yamo mikobani. Jamani haya majina si ni
ya watu, yakifichwa wasiyaone ndio nini?
Maana
yake Serikali inaogopa majina yakiwa wazi yataonekana. Lakini ni
lazima yaonekane kwa sababu ni majina ya watu hai, labda kama
wamekufa. Na aliyefariki dunia hatakiwi kuwemo kwenye daftari la
kudumu, sasa hofu iko wapi? Kama majina yanafichwa na mtu
asipoliona lake atafutiwe mkobani, ina maana kuna siri. Ipi
hiyo?
Sasa
itakuaje wananchi wasiamini kwamba kuna mchezo mchafu umeandaliwa
katika kuyatoa majina ya wapiga kura? Ndio huo usirikali anaousema
Rais Mkapa. Halafu ni wa nini? Wananchi wana dhana tu si uhakika.
Kwa hivyo, Tume, ili kujiridhisha mko wazi na hamsimamii mchezo
mchafu, yatoeni hadharani majina ya wapiga kura badala ya mtu
kutumia saa mbili za kuhangaikia jina lake. Muda huu ni adhimu
watu wautumie kuhangaikia chakula.
Inatia
moyo Rais Mkapa aliingia vizuri akitoa ahadi na leo anatupa maneno
yanayomuweka katika nafasi ya kuondoka vizuri. Ila anaondoka na
mtihani mgumu kwa tulivyozoea; uchaguzi mkuu wa Zanzibar. Huu ni
mtihani kwake Rais na kwa sababu amekwishaambiwa namna vya
kuushinda, ili aishi vizuri maisha ya ustaafu, namuachia mwenyewe
na mambo yake. wanasiasa wa upinzani wanamwambia: Tembea juu ya
maneno yako Rais Mkapa.
Amenikuna
kuzungumzia rushwa leo. Ameikuta imestawi alipoingia na anaondoka
ikiwepo, lakini ikiwa imezidi kustawi licha ya juhudi nyingi
alizochukua kama inavyoonyesha katika hotuba yake. Kazi bado ni
ngumu kwa sababu wakati anazungumzia rushwa ndani ya serikali na
taasisi zake, hali halisi inaonyesha mbaya katika chama chake,
CCM.
Tatizo
la rushwa alilitumia kama bilhamu ya kuomba kura akijua kweli ni
tatizo. Leo anaondoka rushwa imeingia ndani kabisa ya chama cha
siasa dhamana wa dola. Tusemeje? Hiki ni chama cha rais na chama
ambacho Mwalimu Julius Nyerere alisema ndicho kitoe tu rais si
kingine, lakini kinanuka rushwa ndani ya viongozi wake wakiwemo
hawa wanaohangaika kutafuta ubunge na uwakilishi.
Chama
hiki kilitumia mwanya wa tatizo la rushwa kutengeneza Ilani ya
Uchaguzi mwaka 1995 na kutamka kuwa serikali itakayoundwa baada ya
uchaguzi, itakuwa haina huruma wala aibu na wala rushwa: watoaji
na wapokeaji.
Kwa
kuwa rushwa ilikuwa na ingali tatizo kubwa nchini petu, wapiga
kura wengi, kama si wote, waliamini serikali, yeye rais akiwa
kinara, itasimama na maneno yake kwa kuonyesha kwa vitendo, si kwa
maneno tu peke yake, ujasiri wa kupambana na wanaoipalilia.
Haikuwa tabu wapiga kura kuamini tatizo la rushwa litatoweka
kutokana na ahadi zilizotolewa na mgombea na chama chake. Ndipo
mgombea huyo alipochaguliwa kwa asilimia 61.
Mengi
ya mfano huo yalitendeka kabla ya kutolewa ripoti ya uchunguzi wa
ukubwa, chanzo na mbinu za kutokomeza rushwa. Ni rais mwenyewe
aliyeunda tume ya uchunguzi wa suala hili, lakini ripoti yake
ikapata mtihani mkubwa: ilionekana kama ingefaa isiwepo maana sasa
mapambano ya dhati dhidi ya wala rushwa, hususan watu wakubwa
kiserikali, ilionekana ni kazi ngumu kuliko. Rais ameanza
kuzoeleka si mpya tena kama ilivyokuwa pale mwanzo.
Wakati
ule Rais alipata kusema ofisa akituhumiwa tu kuhusika na uovu wa
rushwa, hata kama kutakosekana ushahidi wa kumfungulia mashitaka
mahakamani, serikali yake itamchukulia hatua za kumuondoa kazini
kwa kuwa itakuwa amekwishaharibu sifa ya serikali inayostawishwa.
Serikali ya uwazi na ukweli. (Alikanusha haya, sijui kama bado
anakanusha).
Kidogo
kidogo kasi hiyo ikaanza kufifia na tukaanza kushuhudia kauli za
kutofautiana na dhamira halisi ya mapambano ya kutokomeza rushwa
nchini.
Nilipata
kueleza katika makala za uchambuzi miaka ya nyuma, kwamba kijana
wa Manyoni, mkoani Singida, alinifichulia siri ya watendaji wa
TAKURU. Walimtia kati akakosana na Mahakama, Polisi na Taasisi
yenyewe ya Manyoni. Alifunguliwa kesi bandia ya wizi wa vitu vya
gari ya Padri. Polisi hawakuwa na ushahidi lakini wakala njama na
Padri kumhilikisha. Hakimu, Polisi mpelelezi na wakuu wao
wakamuandama. Chuki alizojengewa nao zilimsukuma atoke Singida
ende Dodoma kutafuta wa kumlalamikia.
Akanikuta
nikiwa ofisi za Business Times Ltd (BTL) Dodoma wakati ule.
Akaeleza ya kupwa na ya kujaa. Nikatumia ujuzi kuyatoa na
nilimpigia Msaidizi Mwandishi wa Habari wa Rais kumhimiza
afuatilie. Kama alifuatilia au laa, anajua kwa sababu hakunieleza
kitu. Ninaamini yule kijana aliendelea kusakamwa kwani hata TAKURU
Dodoma haikumsaidia na Mkurugenzi wa Operesheni Makao Makuu
hakuwajibika ipasavyo. Maofisa aliowatuma Dodoma na Manyoni nao
hawakuwajibika, walimfuata Padri na Hakimu kutaka Kitu Kidogo
(KK). Kama walipewa sijui, lakini chuki hazikwisha dhidi ya kijana
huyu.
Ni
kweli mvuto wa mikakati ya kupambana na rushwa imepungua na leo
kiasi kinachodaiwa cha rushwa na wakubwa ni kikubwa mno lakini
wadogo ndio hubanwa haraka. Tunajua kumbana mkubwa kwataka meno,
lakini kwanini vyombo visishughulike tukaona? Tunaona watendaji wa
vyombo hivi wanavyojigongagonga linapotokea suala la
kufuatiliwa.
Hata
leo nasoma habari za Stephen Kazi, aliyemaliza ubunge wa jimbo la
Mwanza Mjini akiilaumu TAKURU kwa kushindwa kudhibiti vitendo vya
rushwa vilivyokuwa vikifanywa na baadhi ya waomba kuteuliwa na CCM
kugombea uchaguzi ujao.
Mdudu
rushwa anasemwa kutumika (sana) katika utaratibu wa CCM kupata
wagombea wake. Utaratibu wa wagombea kupatikana kwa njia ya
kupigiwa kura za maoni na wanachama wa majimboni, umeonyesha kwa
mara nyingine mwanya ulioshindikana kuzibwa na inatia hofu kama
kweli CCM imekomaa kisiasa. Kukomaa kisiasa ni kujenga utaratibu
unaochochea uwazi badala ya kuchochea rushwa
kutawala.
Zanzibar
haikuachwa nyuma katika uovu huu. Taarifa za wajumbe wa kupiga
kura za maoni kugaiwa simu za mkononi na fedha za kuanzia pamoja
na chakula cha kuacha nyumbani, ni nyingi. Muombaji mmoja
alifungua duka (au alitenga idadi fulani ya simu dukani kwa mtu)
na kugawa simu kwa waliopitia kwake. Ukipata tu memo aliyoisaini,
umeibua simu ya fedha. Na huyu kashinda kura na pengine ataingia
Bungeni. Mwingine aligawa simu siku nyingi kabla ya kura.
Mkinihitaji tu nipigieni kwa sababu nyumbani si kuzuri kwenu
kunifuata, naambiwa muombaji mwingine wa ubunge
amesema.
Waziri
mmoja aliyeshinda kura aliahidi kitita kikubwa mtu aliyetaka
kuchukua fomu kupingana naye. Mwambieni nitampa milioni 4.5 na
gari ndogo asichukue fomu, naambiwa ametuma mpambe wake atoe
ujumbe huu. Kashinda kura na ataingia Baraza la Wawakilishi
pengine. Ni wengi hawa nafasi imekwisha.
Kwa
nukta hii, ni jambo la wazi tukisema sehemu kubwa ya washindi wa
kura za maoni ndani ya chama tawala, wamehonga na ndio watakuwa
wawakilishi wa wananchi katika Bunge na Baraza la Wawakilishi.
Sasa Mwalimu Nyerere akija leo, atasemaje? Bado Rais atoke
CCM?.
Ends.
|