|
Wapendwa Wanaukumbia
wenzangu;
Kawaida
inaendelea. Ufuatao ni Waraka mpya uliotoka wiki iliyokwisha baada
ya kuchapishwa ktk gazeti la RAI la Agosti 18. Ni faida kubwa kwa
wale walio mbali na yanakopatikana magazeti ya Habari Corporation.
Wengine nanyi nia nafasi ya kuusoma kwa makini na kwa
karibu.
Jabir
Idrissa+
Headline:
Uchafu wa Daftari usafishwe haraka tupate Uchaguzi
Huru
Waraka kutoka
unguja
Kama kuna
suala linalovunja moyo wananchi wa Unguja na Pemba, visiwa viwili
vikuu vinavyoiunda Zanzibar, ni tabia za kiutendaji za Tume ya
Uchaguzi Zanzibar (Zanzibar Electoral Commission, ZEC). Na kwa
bakhti mbaya, yanayotendeka kadiri siku ya uchaguzi inavyosogea
karibu, ni ushahidi wa hofu walizokuwa nazo wananchi hawa tangu
awali.
Sehemu
kubwa ya wananchi walikuwa na wasiwasi kama tume hii inayoitwa
huru, itatimiza matumaini yao na upatikane uchaguzi huru na wa
haki na utakaofanyika katika amani na utulivu. Yule asiyewafahamu
vizuri Wazanzibari, anaweza kudhani kwamba hofu yao hiyo inatokana
na upumbavu tu wa kupenda kutabiri.
Sivyo.
Kama kuna watu wasiofaa kuitwa wapumbavu ni wa Zanzibar. Hawana
sifa hata moja za kupewa jina hilo. Hawa ni watu makini kiasi
usichoweza kukadiria wewe unayejenga imani ya kuwabez. Hawa si tu
watu makini tu peke yake, ni watu wenye hekma na busara kubwa,
watu wastaarabu na wavumilivu wa kweli.
Sifa
yao kubwa ni kutosahau, na hususan kile kilicho kibaya. Wanasamehe
wakosaji wao lakini katu hawasahau makosa dhidi yao, iwe
ametendewa mmoja wao kama mtu binafsi, familia yake au kwa ujumla
wao kama watu wa jamii moja wanaotofautiana kwa asili yao. Kwa
hakika, yale mambo yanayowaunganisha watu hawa wa asli tofauti,
ndiyo hasa wasiyopenda yaharibiwe. Kuyaharibu haya ni matukio
yanayochefua hisia na imani zao.
Kwa
hivyo, Wazanzibari si wasahaulifu wa maudhi, au uhuni, kedi na
kejeli za aina yoyote walizopata kutendewa na watawala tangu
ilipoanza historia yao kama taifa. Kila palipotokea jitihada za
kuwatenganisha walikataa. Ndio maana mpaka leo watu hawa wamebaki
wamoja licha ya kuendelea kwa jitihada za kuwatenganisha.
Ni
kwa sababu ya fikra dhaifu tu za baadhi ya viongozi wao tangu huko
nyuma, wanaonekana karne hii kama ni watu waliogawika mno. Ni
siasa mbovu na zisizo mwelekeo zilizobomoa misingi ya umoja wao.
Hili ndo tatizo lao Wazanzibari: hawajapata uongozi madhubuti kwa
miaka mingi ya historia ya nchi yao Zanzibar, licha ya maamuzi na
dhamiri zao kutaka iwe hivyo.
Sote
tunakubaliana, kama nchi, Zanzibar imepitia vipindi tofauti vya
utawala na mfumo wa siasa za ushindani si mgeni kwayo. Ulikuwepo
miaka ya 1960 kabla ya Januari 12, 1964 yalipofanywa mapinduzi ya
kuungoa utawala wa Kisultani. Serikali iliyoundwa baada ya hapo,
ilikataa mfumo huu lakini ilikataa hatua nyingi za kupanua
demokrasia ya watu. Ilikuja enzi ya giza nene. Kukitokea kila
kituko. Ah, yamepita haya, kuyarudia ni kichefuchefu kingine na
msingi wa mada hii ni kuzika vichefuchefu vya namna
ile.
Ukiitizama
Zanzibar ya muongo wa 1990 na tulionao wa 2000, utagundua ya kuwa
imekuwa ikiongozwa na watu wa namna yake kwa vigezo vya ubabe,
ubinafsi na unafiki juu ya vingi. Uongozi usioruhusu uhuru wa
kweli wa watu wake kuamua yanayowahusu, licha ya kujua kwamba haki
yao hii ya kufanya uamuzi wa mwelekeo wao imetandikwa katika
matamko ya kimataifa na hata katika Katiba ya nchi yao.
Hivi
karibuni, nilikutana na mgeni mwenye asili ya Ulaya. Aliniuliza:
Hivi unafikiri (mimi) nyinyi (Wazanzibari) hamna watu ndani ya
visiwa vyenu hivi wanaoweza kuwaongoza vizuri. Nilipotaka kumjibu
haraka alishangaa na kunizuia. Akaendelea: sipendi unijibu haraka.
Alitaka nitafakari swali lake kwa sekunde chache ndipo nimjibu na
jibu liwe na ufafanuzi mpana. Nilikataa rai yake ya kutumia
sekunde kwa sababu hapakuwa na sababu hiyo. Lakini pili, nilikuwa
tayari kutoa jibu lenye ufafanuzi. Kwanini?
Naam.
Tangu nianze safu hii Agosti mwaka jana, nimekuwa nikihangaika
kutengeneza hoja zenye mwelekeo wa kuiingiza nchi yetu katika
utawala unaojumuisha watu wenye hekima na busara. Watu wanaoogopa
aliyewaumba, watu wanaotembea na maneno yao, watu wanaojali utu,
watu wenye uchungu na uzalendo wa kweli na nchi yao. Nimekuwa
nikipiga kampeni nzito (si ya kisiasa ivyo, ya kifikra) ilengayo
katika kuipatia Zanzibar hatima njema).
Wanaodhani
napiga siasa humu wanacheza. Si mwanasiasa mie isipokuwa kijana
mbichi niliyejifunza nikatambua na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu,
amenipa thubutu ya kusaidia wananchi wenzangu watambue utu wao,
utamaduni wao, utaifa wao. Watambue dhamira za kuumbwa kwao japo
si katika mtizamo wa kidini hasa. Watambue ukweli kwamba
kinachowaunganisha ni uzanzibari wao, utanzania wao na historia
yao kama nchi.
Katika
kuwatandikia misingi ya kufahamu elimu hii ya utambuzi wa asili
yao, utu wao na utamaduni wao na kile rafiki yangu mmoja hupenda
kunieleza tukikutana; taarikh (tarehe), ndio huwa
ninadadisi hili na lile, kati na kati, nikizindua viongozi wenye
dhamana ya kuongoza wenzao mwenendo mwema wa kuufuata. Nazungumzia
watu kuheshimiana, kupendana, kutakiana mema badala ya mabaya,
kustahmiliana na kusaidiana.
Naingia
katika kuchochea watu wenye misimamo ya kijinga ya kujijali wao tu
ndio wazalendo wa kweli wa Zanzibar, wabadilike kifikra kwa sababu
nchi hii ilikuwepo hata kabla ya wao, lakini pia historia yake
haiwezi kutumika
kuendeleza chuki na hasama miongoni mwa Wazanzibari. Tunao wale
waitwao wahafidhina wa kutupwa wanaotaka watu waamini kwamba wao
tu wana haki zote.
Hawa
ni watu wa hatari kwa sababu misimamo kama yao ndiyo iliyozibomoa
Rwanda na Burundi. Ndizo zinazoitafuna Zimbabwe kwa kuamini kila
mpinzani ni wakala wa Waingereza. Uhuni mtupu mwanasiasa kusimama
jukwaani akiita jamii moja ndani ya nchi iichukie nyingine. Eti
jamii hiyo ndiyo yenye hatimiliki na Zanzibar. Mimi wa jamii moja
lakini mbona sioni ulazima wa kujitambulisha kwayo kwa sababu
sijathibitisha kuwa ni fakhari kuwa hivyo?
Kwa
sababu siamini atokaye Unguja ndiyo mbora, nawaona watokao Pemba
ndugu zangu kama wa damu vile. Nachukia jitihada zozote za
kunitenganisha nao. Pemba kujitenga na Unguja haiwezekani kwa
sababu historia imewajenga na anayenuia kuifuta, huyo ndiye adui
wetu. Walipokuwa na hata leo wakisimama wanasiasa na kuchochea
utenganishi wa jamii hizi mbili, ninawaita wehu wakubwa kwa sababu
kilichojengwa na aliyetuumba hakibomoki kwa kauli ya mwanasiasa
huyu. Lakini imani yangu hii, ina maana tu kama hakuna jitihada za
kutaka kulazimisha kujitenga huko.
Halafu
anapotokea mwingine akajaribu kutenganisha Wazanzibari kwa sababu
ya vyama vya siasa, huyu ni mwehu mwingine maana vimeanzishwa kama
hatua ya kujenga hoja za kisiasa katika jitihada za kutuongoza
vizuri. Chama cha Mapinduzi (CCM) kilipokubali maoni ya wachache
kutaka mfumo wa vyama vingi, kilisema maoni ya wachache nayo yana
haki ya kuheshimiwa. Si kwa sababu ya wengi ni mabaya, bali ya
wachache hayakwepeki ili kwenda na dunia.
Leo
napata matatizo kuamini CCM, au niseme baadhi ya viongozi wachache
wa chama hiki, kama ilikusudia kwa dhati yake kuleta mageuzi ya
kidemokrasia nchini. Niamini vipi wakati nashuhudia (sina maana
ninaona kwa macho kila kitu) matukio yasiyoijengea Zanzibar
hatima? Matukio ya kuudhi watu, matukio ya kukejeli utu wa
Wazanzibari, matukio ya kuangamiza umoja wao, historia na
utamaduni wao. Haiwezekani na ndio maana lazima akina sisi
tuendelee kuwatia darasani wahafidhina.
Ni
ukweli kwamba ni kazi ngumu kuzungumza nao kwa sababu wamejipa
nguvu hata kuliko za Firauni. Wamesahau alishindwa na jeuri yake,
na kutoweka kupitia kifo kibaya. Lakini nakiri hawa ni Firauni wa
uhakika kutokana na matendo yao. Kuna uhuni unafanyika na sura
yake inakuja kuonyesha kuwa kama hawakushiriki kwa mikono yao,
basi kwa fikra zao. Wanayasababisha matukio machafu.
Yule
mgeni ndipo nilipomwambia kwamba mbona kuna madazeni ya watu wenye
hekima na busara wanaoweza kuiongoza Zanzibar? Wapo na wengine
wamo ndani ya CCM. Tatizo lao wamegubikwa na mtindio wa akili kwa
kuwa kila wakiamka wanakutana, wanapanga na kutekeleza nao.
Wachache hao wenye thubutu ya kuchanganyika, wanayaona matokeo
yake. Hawapati taabu ya kununua vitu madukani au kusaidiwa
wanapokuwa na shida za kifamilia au za kikazi. Wanaonyeshwa utu
kwa sababu nao wanaujali. Wanaamini ni mazingira tu
yaliyosababisha huko waliko lakini kila kitu kinawezekana. Hata
CCM inasema kila kitu kinazungumzika. Tatizo ni kweli
yanazungumzika? Yakizungumzwa na muafaka kuwekwa, yanatekelezwa
kwa udhati wa moyo? Hili ndo tatizo letu.
Tunao
watu wanaoweza kuongoza vizuri nchi na ikapata baraka. Katika
upinzani kuna watu makini ukichanganya na waliomo ndani ya CCM
wenye moyo na uzalendo wa kweli, nchi inaendesheka. Nilipata
kusema wanaoona hawawezi waachie ili wananchi watengeneze
mustakbali wao. Waachie kwa sababu Wazanzibari wamechoka
kuendeshwa puta ja punda asiyekuwa na haki ya kusema nimechoka.
Wao wanaweza kusema na wanasema ila, uhafidhina
unawanyonga.
Turudi
ZEC kwa sababu imekumbwa na wahafidhina hawa wasioitakia nchi
mustakbali. Mawazo ya kuwa hii nchi ni kwa ajili yao tu yanazidi
kutinga fikrani mwao. Hawajatulia kwelikweli kwa sababu wangali
wakiamini kwa kuiingilia Tume ya Uchaguzi, yao yatakuwa. Hizi ni
dalili za muflis. Mfalme ana pembe lakini wao hawana maana
zimefujika na hazipigi tena. Zikipiga zinapiga ukuta, zikitumiwa
zinagonga mwamba. Nguvu ya umma inasimama.
Jitihada
zao za kutiribua Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK) zimefika
mwisho na ndivyo uchafu walioutengeneza wakiwa ufichoni unaanikwa
hadharani leo. Ujanja si kuwahi bali kupata wanasema. Lakini
wahafidhina hawajawahi wala hawajapata kitu. Inashangaza vijana
wabichi wanadhamini kupiga raia wema virungu na nondo kwa sababu
anautaka ubunge. Asahau kwa sababu nguvu ya umma
inasimama.
Uhuni
mtupu. Tunajua jawabu ya mbili na mbili ni nne, lakini kwa
wahafidhina hawa, aibu hawana kwa kuleta jawabu ya 20 tukijumlisha
kumi katika tano. Basi kiwewe kimewazidia kwa kujumlisha hesabu
zisizojumlishika. Wanacheza na takwimu kama vile ni mali yao.
Wapi? Takwimu mali ya magwiji wanaojua namna ya kuleta majibu
mazuri kwa hesabu nzuri. Na majibu mabaya huja kwa hesabu mbaya.
Acha waambiwe ni machuruchuru hawa, hawapati maana nguvu ya umma
inasimama.
Inakuaje
ripoti ya uandikishwaji watu kwenye daftari itoke elfu 499 na
kidogo baada ya uandikishaji kukamilika Aprili 29, lakini majina
yaliyobandikwa (mengine hayakubandikwa bali wahafidhina walituma
mawakala wao wayatie vibindoni kama mali yao), yazidi elfu 500
(500,000). Haya natuambiwe hayo mengine yametokea wapi? Hawa ndio
wale tulio tukiambiwa kuna vitabu vya pembeni, nje ya
kituo.
Mtakumbuka
ngangari wa Ghana, jimboni kwa Waziri Muhammed Seif Khatibu
walibaini kada mmoja wa CCM alilaghai waandikishaji wasaidizi na
kufanikiwa kuondoka na vitabu vya Tume? Mnakumbuka kulivyokuwa na
kituo cha Pangatupu? Mnaweza kurudisha memori zenu Mahonda
palipotumwa basi la Polisi? Hata Jangombe Maandalizi walifungua
kituo na meja mzima akageuka msimamizi wake. Labda kama Tume
ilifanikiwa kuharibu uandikishaji huo, ujanja wa bure.
Rudini
mjini mkumbuke ya Tumekuja na Forodhani, mwende Kusini takwimu
zilikopandiana baada ya uchafu wa wahafidhina. Tume ilipoambiwa
wakakasirika, lakini ndo ukweli watu wamezidi leo katika daftari
na nguvu ya umma inasimama.
Leo
tunaambiwa Mpapa, jimbo la Uzini kuna watu wamezidi, Kizimkazi na
Mtende watu wamezidi na Mji Mkongwe nako wamezidi karibu 3,000.
Wamezidi vipi? Ofisa mmoja kati ya waliosimamia uandikishaji
anatamba eti ni kutafuta kisingizio. Kwa maoni yake, ni kasoro za
kibinadamu kumuacha huyu na yule. Anataka watu waamini anavyoamini
yeye, kwamba alikuwa makini katika kazi yake. Alikuwa muadilifu
katika kazi yake, aliheshimu sheria na taratibu alizopatiwa na
Tume. Yeye alikuwa shujaa katika kupalilia hatima njema ya nchi.
Asahau, uchafu uliopitishwa kwa kujua au kutokujua kwake, umekuja
hadharani. Kisingizio hakipo kuna kauli thabiti na nguvu ya umma
inasimama.
Vyama
vya upinzani vikilalamika kila wakati uandikishaji ulipokuwa
ukiendelea kwamba kuna michezo ya rafu inafanywa vituoni na nje
yake lakini hawakusikilizwa na wakaishia viongozi wake kubezwa
kuambiwa wanatunga mambo kwa manufaa yao. Wameitwa wachochezi kama
ninavyokumbuka baadhi ya barua za majibu kutoka Tume. Haya nani
watungaji kati ya viongozi wa vyama hivi na Tume? Nguvu ya umama
inasimama.
Nguvu
ya umma inasimama kutaka kujua ukweli wa uchafu ndani ya Daftari
la Wapiga Kura. Umma wa Wazanzibari unataka uelezwe, kwanza, wale
waliorudishiwa haki zao na Mahakama baada ya kunyimwa kihuni,
wanaandikishwa lini na vipi? Na je wale waliokosa lakini bado ni
haki yao kwa sababu Mahakama iliwageuka kutokana na matatizo ya
kiufundi yasiyowahusu, na ambao ndivyo Rais Amani Abeid Karume
alivyosema wapewe haki zao wote baada ya kukiri kasoro za
kiutawala, wataingiaje kwenye Daftari?
Mambo
haya ni rahisi isipokuwa uhuni tu wa baadhi ya watu kujiona wao ni
bora kuliko wenzao. Yote haya yaliulizwa lakini wapi, majibu ya
Tume yakawa tunachunguza, tunafuatilia, tunapitia, tunatafakari,
tunashughulikia, tuna. Hivyo tu huku mambo yanaharibika na leo
yapo hadharani. Pengine walidhani hawataadhirika. Kwao ni sawa na
pundamilia kujificha kwenye minjugu, akisahau yu mrefu mno asoweza
kujificha hapo. Shingoye i nje, kefu mgongo wake. Mambo hadharani
leo na kila mtu anaona. Hawajali kuvunja moyo wahisani wanaotia
fedha za walipa kodi makwao. Huu ni ukosefu wa fadhila na kutojali
jasho la watu.
Haya
tunasubiri Tume itafanya nini wakati tukipata taarifa kwamba
imeridhia matakwa ya utawala kutakiwa iondoe mkataba ilioingia na
kampuni ya wataalam ya Waymark ya Afrika Kusini wa
kuchambua majina ya walioandikishwa ili kutambua yale machafu.
Sitaki kuamini Tume hii yenye wanasheria wajuzi kama Jaji wa
Mahakama ya Rufaa na mtu mwenye hekima na busara kubwa kama
Mwenyekiti Masauni Yussuf Masauni ilikosa kuwajibika hata kuamua
kuusaini.
Naweza
kuamini ninapoambiwa ya kuwa kila kitu kiliangaliwa kwa undani, na
kila kifungu cha mkataba kilijadiliwa kabla. Sina sababu ya
kuamini makamishna wa Tume na watendaji wao walikosa uadilifu kama
inavyodaiwa kuwa wameuza uhuru wa nchi yetu kwa kutia mkataba na
kampuni ya nje. Na tangu lini tukawa wazalendo wa kutoa zabuni kwa
wazalendo? Mbona nyingine hazitolewi hivyo? Iwe hii tu
kwanini?
Tumelijua
tatizo lao wahafidhina: kisu cha kule kinakata kisawasawa si butu.
Asiyestahili hawezi kuingia iwe usiku iwe mchana. Kompyuta na kwa
mfumo wao, haikubali jina langu liingie katika Daftari mara mbili
eti kwa sababu ni mpiga domo gazetini. Eti hiyo iwe ndiyo zawadi
yangu. Likiingia mara ya pili jina, mtiaji ataulizwa, unataka
kufuta la awali (liliopo). Kwa hivyo ni kusuka au kunyoa.
Unakubali yaishe, si hivyo mpaka usiku usitoke kuingia mchana:
kiyama.
Kwa
panga hilo, itakuwa yale yale ya siku zote tangu 1995, Mambo Ni
Magumu (MNM). Haya, mkataba umesimama kutokana na hujuma za
wahafidhina lakini tatizo lipo bado; uchafu wa Daftari
walioupalilia kwa nguvu ya Kidumu Chama cha Mapinduzi utasafishwa
vipi? Naamini Wazanzibari hawakubali uchaguzi usite wala
hawakubali uende bila ya Buku. Hawakubali manyuva. Uchaguzi
ufanyike tu tena kwa Daftari safi ja shuka. Itakuaje? Idumu amani
na utulivu na uchaguzi huru, wa haki na wazi.
Ends.
|