Waraka Kutoka Unguja
August 25, 2005
By
Jabir Idrissa
Headline:
SMZ twataka Daftari safi kwa Uchaguzi safi
Wiki
iliyopita nilianza kwa kusema kwa bakhti mbaya, yanayotendeka kadiri
siku ya uchaguzi inavyosogea karibu, ni ushahidi wa hofu walizokuwa
nazo wananchi hawa tangu awali. Na baada ya kueleza mengi ndani ya
mada kuhusu daftari la kudumu la wapiga kura la Zanzibar,
nilihitimisha hivi:
Naamini
Wazanzibari hawakubali uchaguzi usite wala hawakubali uende bila ya
Buku (daftari). Hawakubali manyuva. Uchaguzi ufanyike tu tena akwa
Daftari safi ya shuka. Itakuaje? Idumu amani na utulivu na uchaguzi
huru, wa haki na wazi.
Kwa
yaliyotokea na yanayotokea, inazidi kupandikizwa hofu ndani ya akili
za Wazanzibari. Wanaendelea kujiuliza wanaweza kuvuka salama uchaguzi
huu? Waamini itaendelea kuwa uchaguzi wa mazonge na shaghalabaghala?
Waamini ya kuwa utawala na watawala hawajawa tayari bado kuona nchi
inapata uchaguzi madhubuti, inajenga msingi mzuri wa kupatikana amani
ya kweli, kupatikana haki kwa urahisi na huduma kwa
ufanisi?
Tukubali
kwamba hofu inazidi kwa sababu kila kukicha wanasikia na kushuhudia
kauli za kuvunjana moyo. Kauli zinazoashiria mazonge na
shaghalabaghala. Ni kwa sababu mambo yanazidi kufunuka na mitego
iliyo ikitengenezwa kwa malengo, inaonekana kuvuna
kilichotakiwa.
Tunazungumzia
Daftari la wapiga kura wa Rais wa Zanzibar, wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi na madiwani. Tushajua mpaka sasa kwamba ndani ya daftari
kuna majina machafu yasiyotakiwa kubaki kwa sababu kubaki kwake ni
kutishia umadhubuti wa uchaguzi wetu. Kwa uhakika hili sasa
tunalifahamu, na kilichotarajiwa na umma, ni hatua zinazochukuliwa
kusafisha uchafu huu ndani ya Daftari.
Kitu
kimoja hakijafurahisha umma. Kitendo cha suala la usafishaji wa
uchafu huu kutoelezwa bayana na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC). Tume
hii ina wajuzi, ina wataalamu waliobobebea katika Sheria, Teknolojia,
Utawala, Hesabu, Uandishi wa Habari, na isitoshe, watu waliojaa
hekima na busara kubwa, lakini bado taaluma hizi hazijatumika
ipasavyo kuthibitisha kuwa taasisi hii imepewa watu makini. Watu wa
kujenga matumaini ya Zanzibar kuondokana na uhuni na uzandiki. Uwazi
na ukweli ingali tatizo kwa tume yetu. Hili ni tatizo
sugu.
Pamoja
na kupiga debe na kukumbusha mara nyingi juu ya umuhimu wa Tume
kufanya shughuli zake kwa uwazi, bado kuna mtindo wa Siri Kali (SK).
Kila uamuzi siri, kila hatua siri, kila taarifa siri, kila hati siri.
Basi hivyo tu, Kila Kitu Siri (KKS). Utendaji wa ajabu tunaendelea
kuushuhudia ndani ya tume hii. Utendaji unaoiweka tume kuwa moja ya
Taasisi muhimu za kinchi zisizowapa wananchi kile walicho na
wanachotaka kukipata: uchaguzi huru, wa haki na katika amani ya
kweli.
Nimesema
unapojifunua, unaondoa hofu wananchi. Unaondoa uwezekano wa kujengwa
hisia za ajenda ya siri katika taasisi yao. Ndio jamani, Tume ni
Taasisi ya Wazanzibari maana ndio wanaoilipia. Viongozi na
wafanyakazi wa Tume wanalipwa kwa fedha ya wananchi kupitia njia
mbalimbali ikiwemo ya kodi. Basi inatakiwa Tume iwarudishie wananchi
hawa fadhila kwa kutenda shughuli zao kwa uwazi na kwa haki. Waione
tume si tu inatenda maamuzi ya haki na kwa uwazi, bali pia maamuzi
yenyewe yanafanywa kwa wakati muafaka. Hayacheleweshwi.
Baba
unapofika nyumbani ukakuta chakula hakijakamilika kuandaliwa unafoka.
Kwanini? Ni kwa sababu si haba ulipoondoka bajeti imekaa vizuri, kila
kitu kimetimia, sasa ziko wapi sababu za chakula kuandaliwa. Ina
maana umetimiza wajibu wako, isipokuwa mwingine hakutimiza wake.
Hakuwajibika. Sasa kufoka kwako ni kumzindua ya kuwa awe mtimiza
wajibu wake na kwa wakati. Unalazimika kurudi tena kazini kwako bila
ya kula kwa sababu hakikukamilishwa na mwenye wajibu wa kukiandaa.
Kosa zito.
Basi
Tume ya Uchaguzi nayo ni hivyo hivyo. Inapochelewesha uamuzi au
taarifa muhimu kwa wananchi, itambue inawakosea kwa sababu imeshindwa
kutimiza wajibu juu yao. Wao ndio walipaji hivyo wanataka kuiona
faida ya kulipa kwao. Nilipata kusema Tume ina waandishi mahiri wa
habari wanaoweza kutengeneza taarifa za kwenda kwa umma kupitia
vyombo vya habari tele tulivyonavyo. Watumiwe basi ili wajisikie
wamekwenda pale kufanya kazi yao waliyoisomea kuliko kuwabebesha
makaratasi ya kutoa nakala bila ya mambo yenyewe kufikishwa kwa
walaji. Walaji wa taarifa za shughuli za Tume hakuna isipokuwa,
wananchi. Haifai kila wakati kuwakalisha njaa wakati wana uhakika
ghalani chakula kinamwagika ovyo.
Mpaka
naandika waraka uliopita, hakuna maelezo ya Tume kuhusu fununu za
kusimamishwa mkataba ilioingia na kampuni ya Waymark Infotech ya
Afrika Kusini. Hata sisi tunajiingiza tu bila ya kupata uthibitisho
rasmi wa Tume hii. Lakini tufanyeje na tunayasikia yanasemwa nje ya
milango ya taasisi hii, wakati wenyewe wapo hawataki kuyasema kwa
bayana? Tutaendelea kuyasema kwa njia hiyo waionayo wao ndio sawa
kuliko wao kutupatia taarifa za uhakika zitakazoua
uvumi.
Jumapili
kukafanyika halfa ya utiaji saini wa Waraka wa Maadili ya Uchaguzi
Zanzibar. Alhamdulillah, wakubwa wa Tume wakawepo pale. Nililazimika
kushuhudia hafla hii kwa sababu kubwa moja: nitapata fursa ya kuwaona
wakubwa hawa na kuwauliza kulikoni mambo yenu yanasemwa nje bila ya
kauli yenu wakati ndio tuliowapa mdomo? Na kweli, Mwenyezi Mungu
kanisikia. Wakubwa wote walikuwepo na tukawauliza swali hili.
Cha
kufurahisha nao wameamka vizuri walikuwa laini kuliko siku nyingi
sijapata kuona. Mwenyekiti Masauni Yussuf Masauni na Makamu Jaji
Agostino Ramadhani wakasema si haba. Nawapongeza wakubwa hawa kwa
kuamua kueleza japo katika harakaharaka na katika kuchelewa ile
tunayoilaumu kwa nguvu zote. Waswahili twasema kupata hakuna kudogo.
Tulilalamika pale kwamba mbona hatuwasikii Tume kusema kwa wakati
mambo yanapoharibika?
Mwenyekiti
anasema wanaachia magazeti yaseme yatakavyo. Si mshasema nyie maana
nyinyi ni mafundi wa kutengeneza uongo. Mnaandika mambo hata bila ya
kutuona hata mnathubutu kudanganya watu kudai mmemuuliza nani na nani
sijui wakati si kweli aliyetajwa alikuwa nje ya Zanzibar. Acheni nyie
acheni haifai. Hatukumuachia hapo, tulimwambia Tume nanyi mseme
matatizo na mafanikio yenu badala ya kukaa kimya. Mkisema mapema
mnaondoa uvumi na taarifa potofu. Basi hata zinapotolewa potofu pia
mnabaki kimya tu sasa watu waseme nini kama si kuyaamini. Na si
muwaite wanaoandika uongo muwarekebishe.
Basi
Tume inasema: Mkataba wa Waymark wa kuhakiki majina ya wapiga
kura walioandikishwa ni kweli umetakiwa na Serikali usimamishwe kwa
sababu utaratibu wa kiserikali haukufuatwa japokuwa hiyo ni Taasisi
huru. Tume haitoki kuwa ni taasisi ya kiserikali ambayo inapotaka
kuingia kwenye mikataba na kampuni za nje inapaswa kushauriana na
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yeye ndiye atakayeiwakilisha kutetea
kilichofanyika. Baada ya yote, Mwenyekiti anasema wamepata barua ya
uamuzi kutoka Serikalini, msainiji akiwa Mwanasheria
huyu.
Serikali
imeamua mkataba uvunjwe kwa sababu hakuna mantiki ya uhakiki wa
majina kufanywa nje ya nchi na wataalamu wa nje ya nchi. Hiyo si kwa
maslahi ya nchi iliyo huru na yenye heshima yake inayopaswa
kuheshimiwa. Mzee Masauni na Makamu wake wakasemaje? Walijadili
uamuzi wa Serikali Agosti 20 na wangetoa uamuzi stahiki jana. Uamuzi
wenyewe ni wa kupiga hatua kutoka hapo si kurudi nyuma. Ndio maana
yake. Hatuwezi kurudi nyuma bali kwenda mbele.
Mwenyekiti
alisema kitu kizuri pale cha kwamba kazi ya uhakiki ni muhimu
ifanyike kwa vyovyote vile kwa sababu itajenga imani kwa wananchi. Na
kweli, Ofisa wa Kibalozi wa Uingereza, Andrew Massey alituambia wiki
iliyopita kwamba kuhakiki daftari ni hatua ya lazima na muhimu kwa
sababu inachochea wananchi kujenga imani na daftari na hiyo ni namna
pekee ya kuwajenga imani kwamba wanaweza kupata uchaguzi
mzuri.
Daftari
madhubuti litatoa uchaguzi na matokeo madhubuti. Bila ya umadhubuti
katika kumbukumbu za wapiga kura, hupati uchaguzi madhubuti kwanza
umma kufahamishwa kuhusu daftari ni hatua ya lazima kwa sababu ni
haki ya umma kulifahamu daftari lilivyo. Daftari si mali ya mtu au
kikundi chao, mali ya umma, alituambia waandishi wa habari na
wawakilishi wa vyama vya siasa waliokusanyika ukumbi wa Baraza la
Habari Tanzania (MCT) Ofisi ya Zanzibar, pale mtaa wa Shangani.
Ilikuwa katika mjadala wa masuala ya uchaguzi kwa uzoefu wa
Uingereza. Tunacho cha kujifunza.
Leo
daftari lina uchafu na ndio uliotakiwa usafishwe ili liwe madhubuti
na liwe njia ya kupatikana uchaguzi madhubuti, Tume imejigonga na
Serikali imeingia tele. Serikali inajaribu uhuru wa Tume ya Uchaguzi.
Njia inayotumia si nzuri kwa sababu inajieleza kwamba Tume ni huru
lakini papo inaiingilia inapofanya maamuzi yake. tumesikia tamko la
Serikali kupitia Mheshimiwa sana, Ali Juma Shamhuna. Amewarukia
wafadhili na watendaji wa Tume, kwa hakika amewadhalilisha wote kwa
pamoja na mmoja mmoja anaposema kuna ajenda ya siri imetengenezwa na
wafadhili kwa kushirikiana na Tume.
Tangu
lini taasisi ya kiserikali ipange njama na wafadhili dhidi ya
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar? Imeanzia wapi njama hii hata leo iwe
ya pili? Wanaofanyiwa njama wako wapi kwamba wasijue kinachoendelea,
wasifahamu nini kinafanyika ndani ya Tume ya Uchaguzi wanayoilipa?
Serikali haina watu mle ndani ya Tume? Hainao kweli? Si wengi
wakubali. Serikali ina watu wake mle wanajulikana. Hawajifichi hata
wenyewe wapo.
Lakini
serikali inapohoji wajibu wa Tume ijiulize pia inatekeleza wa kwake
na kwa wakati unaofaa? Mara ngapi Serikali imetoa kauli kuhusu lawama
kwamba haiipatii Tume fedha ilizoahidi kuipa kwa ajili ya shughuli za
uchaguzi? Haijui kwamba wahasibu wa Tume hupanda na kushuka kutwa
nzima mara chungu nzima kuhangaikia fedha? Haijui kwamba inatakiwa
kuipa tume fedha kwa wakati ili itimize huo wajibu wake wa kutumikia
umma? Kwani umma haujui kwamba Mwenyekiti amewahi kumfikia Rais
kulalamikia fedha? Umma unajua hili na majibu ni yale yale:
Tutajitahidi kuwapatia fedha kwa wakati. Zimepelekwa kwa wakati?
Mbona ubandikaji majina ya walioandikishwa ulisimamishwa dakika za
mwisho baada ya kutangazwa ungefanyika? Sababu ni moja tu: Tume
haijapatiwa fedha kwa ajili ya kufanikisha hatua muhimu hiyo ya
kulihakiki daftari.
Wazanzibari
tunaambiwa leo kwamba Serikali hairuhusu uhakiki kufanywa nje ya nchi
na eti Waymark waliondoka na majina 30,000 badala ya 10,000
waliyotakiwa kuyachunguza. Hawa ni wataalamu wanaoshirikiana na
wataalamu wa teknolojia waliopo Tume kwa hivyo majina hayakuibwa
yametolewa. Kama hawakupewa kihalali nani amehoji kati ya Serikali na
Tume yenyewe? Tuambiwe badala ya kulaumiwa wataalamu.
Na
kama Serikali ilihoji basi tuioneshee kidole tume haikusema kwamba
imehojiwa mapema kabla ya kusaini nao mkataba. Serikali nayo ina
wajibu kuufahamisha umma pale mambo yanapoonekana yanakwenda kombo.
Njia hii Serikali kutoa taarifa baada ya mambo kuharibika, kama
inavyosema, ni mbinu za kizamani za kutatua matatizo. Serikali yetu,
labda tuseme yetu tukufu, inatuambia kwani nchini hakuna wataalamu wa
kufanya uhakiki ule, au kwamba mbona wapiga kura milioni 16 wa
daftari linalosimamiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
wamehakikiwa hapa hapa nchini, kulikoni majina yasiyozidi 500,000
yahakikiwe nje.
Tuendelee
kuambiwa basi hao wahakiki wa majina ya NEC ni wepi? Jamani ni
hawahawa Waymark na kwa utaalamu unaodaiwa haupo Tume? Kwa
kuwa mpaka sasa sijasikia kauli thabiti ya Tume kuruhusu majina
yachukuliwe nje ya nchi kwa uhakiki, nakubaliana na Serikali hakukuwa
na haja hiyo. Na kwa sababu NEC walifanya uhakiki ndani ya nchi,
kadhalika hoja ya serikali ni nzito. Lakini bado, nini maana ya
kukosoa kasoro hii dakika hii wakati majina hayakuchukuliwa
jana?
Inafurahisha
Serikali yenyewe imekiri hakuna muda wa kutosha wa uhakiki wa
daftari. Bado serikali haijatoa jibu la kuondolewa majina machafu
kwenye daftari kwa sababu njia ya Mahakama ishakamilika na bado
serikali haikutoa kauli ya kuwathibitishia wananchi wale kuwa
wataandikishwa kabla ya siku ya uchaguzi. Isitoshe, wangapi waliopewa
haki ya kuruhusiwa kuandikwa? Hivi tuseme Serikali haijui kwamba kuna
watu kwa maelfu walizuiwa kujiandikisha kutokana na vituo kuhodhiwa
na mawakala wao? Serikali inataka kujivua lawama za uhuni uliotokea
wakati wa uandikishaji? Imechelewa kwa sababu kila kitu
kilijidhihirisha vituoni.
Kwa
mfano, kitendo cha kuwazuia masheha kufika mkutano wa Tume, Mkuu wa
Mkoa kumrudisha Sheha aliyekuwa ameondolewa kituoni na Tume kwa
sababu ya kutokuwa muadilifu, kuvamiwa watu wa Kinuni na Jangombe,
kujeruhiwa kwa mapanga Mzee Juma Muhunzi, kuchomwa moto viwanda vya
mbao Kidimni, Nyerere na Kinazini. Yote haya yalitokea na serikali
haikutoa kauli yake. Hakuna aliyekamatwa. Tukubali uhuni mwingine ni
kazi ya dola.
Nani
anafadhili kambi za vijana wanaojitambulisha kuwa ni wakereketwa wa
CCM, chama dola? Kama si Serikali ni lini imekubali kwamba kambi hizi
zinazalisha uharamia ukiwemo huu wa kupiga watu waliostarehe bukheri
wa afia kwenye baraza zao? Tunaposhuhudia matukio ya kihuni mitaani
mwetu usiku na mchana huku serikali ikikaa kimya tusemeje? Ndio
utawala bora huu na utawala wa sheria? Hii si ni Operesheni Dondola
kuwarudia raia wema wakati tuliambiwa ni ya kuwalinda? Lazima tufike
mahali kila mtu aseme ukweli. Kama sisemi ukweli basi ni jukumu la
Serikali kueleza ukweli kwa wakati.
Shughuli
zote za uchaguzi kugharimiwa na Serikali. Ni jambo zuri lakini hili
nalo linazua maswali mengi kuliko nguvu za kuyajibu. Leo Serikali
yetu tukufu inazo fedha za kutosha kugharimia uchaguzi, leo? Kumbe
kama tunavyoamini wengi, inazo fedha ila inazitoa inapojisikia. Siku
wakubwa wanapoamka vizuri wanaifikiria Tume siku wanayolala bwi na
kuamka nao nongwa. Zinapotakiwa fedha na Tume hazipatikani ila
inapotaka Serikali inatoa, huu ni ujanja na kibri na Serikali adilifu
haipaswi kuonyesha kibri katika suala la kutimiza wajibu wake. Ifanye
tu bila ya kujidai.
Kauli
ya Serikali kuhusu Daftari ni kichekesho cha mwaka. Kauli yake kuhusu
kugharimia uchaguzi ni kituko pia. Lakini upande mwingine naipongeza
Serikali kwa kuona inayo njia ya kutokea. Ipo kumbe njia ya kuzidisha
mazonge kwa sababu kwayo, nina hakika Daftari litabaki chafu na maana
yake uchaguzi utakuwa mchafu. Serikali imetoa ahadi ya kulisimamisha
Daftari kuhakikiwa na inatuambia kuwa acha tu tuende kwenye uchaguzi
bila ya Daftari madhubuti. Wataalamu weshasema Daftari Madhubuti
Uchaguzi Madhubuti vinginevyo mazonge matupu. Tunasubiri ukweli
utadhihiri na Nguvu ya Umma inasimama.
Ends.