Waraka Kutoka Unguja
September 1, 2005
By
Jabir Idrissa
Headline:
Muradi uhakiki wa Daftari unafanywa, Tume kaeni
kimya!
warakaSpt01
Khabari
ya Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK) inazidi kuwa muhimu. Tume
ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) bado haijataka kusema huku ikijua fika ya
kuwa inatakiwa iseme ili wananchi wanaoilipa wajue nini kinaendelea
kuhusu suala hili.
Umma
unachokifahamu mpaka sasa ni kwamba Serikali imetamka kuvunjwa
mkataba wa uhakiki wa majina yaliomo katika Daftari la Wapiga Kura
kufanywa nje ya nchi na wataalamu wa kampuni ya Waymark
Infotech ya Afrika Kusini. Isitoshe, Serikali kupitia Waziri wake wa
nchi katika Ofisi ya Waziri Kiongozi, Ali Juma Shamhuna, imesema
kuanzia sasa itagharamia shughuli zote za uchaguzi.
Inasema
imeamua kuchukua hatua hii baada ya kubaini kuwepo ajenda ya siri kwa
wafadhili wanaosaidia shughuli za uchaguzi mkuu. Wafadhili hawa,
Canadaa, Denmark, Jumuiya ya Ulaya (EU), Finland, Sweden, Norway,
Uholanzi na Uingereza, wanaambiwa na Serikali yetu tukufu kwamba
wanakula njama na vyama vya upinzani kuingilia uchaguzi huru, wa haki
na unaotakiwa kufanyika katika hali ya amani na utulivu.
Wakati
bado Tume haijataka kutoa kauli yake na kuzidisha hofu waliyonayo
Wazanzibari, kuna matukio ya kutia moyo yanatokea nchini petu
Zanzibar.
Siku
chache baada ya Serikali kutoa kauli yake kuhusu uhakiki wa Daftari
la Wapiga kura, nchi wafadhili nao walisemaa. Haikutosha tu kusema,
waliamua kufunga safari kuja Zanzibar na kuonana na viongozi wakuu wa
Serikali. Wakitaka kupata ufasaha wa kauli hiyo na mantiki yake nini
hasa.
Basi
walikuwa Balozi Mdogo wa Uingereza, Mike Kroll pamoja na Balozi
mwenzake kutoka Norway. Walikutana na Waziri Shamhuna na Sauti ya
Tanzania Zanzibar (STZ) ikarusha taarifa kwamba Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar imesisitiza msimamo wake wa kuachiwa kugharimia uchaguzi
yenyewe.
STZ
imekariri mazungumzo ya Waziri na mabalozi hao ikisema kwamba nia ya
uamuzi wa Serikali ni kutaka kuhakikisha uchaguzi mkuu wa Oktoba 30
unafanyika kwa uhuru, kwa haki, na katika mazingira ya amani na
utulivu. Hakuna kingine.
Lakini
wapashaji wa khabari wanasema kulikuwa na mengi yaliyosemwa na pande
zote mbili. Tunaambiwa kwamba Mabalozi hawa walimtaka Waziri atoe
uthabiti wa msimamo wa Serikali kuhusu suala la wafadhili kusaidia
shughuli za uchaguzi. Kwamba ni hakika kabisa Serikali haihitaji
msaada wa wafadhili? Hii maana yake ni wafadhili kutaka Serikali itoe
msimamo wake kwa maandishi kwa kuwa wafadhili hawakuamua tu kusaidia
Zanzibar kufanikisha uchaguzi wake.
Wafadhili
walifanya mazungumzo na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, walizungumza
na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kwa undani (sana) kuhusu
utekelezaji wa Muafaka uliofikiwa na kusainiwa na Chama cha Mapinduzi
(CCM) na Chama cha Wananchi (CUF), vyama vyenye udhibiti mkubwa zaidi
wa siasa kwa Zanzibar. Kwa hivyo baada ya mazungumzo na wafadhili na
serikali hizi mbili, palifanywa makubaliano ya wafadhili kusaidia
utekelezaji wa Muafaka.
Makubaliano
haya hayakufanywa kwa maneno matupu, palikuwa na mkataba wa
kuthibitisha kwamba pande hizi husika, Serikali na Wafadhili,
wamekubaliana kushirikiana katika hatua ya kufanikisha uchaguzi wa
Zanzibar. Uchaguzi si siku ya kupiga kura tu, la hasha. Uchaguzi ni
hatua kubwa inayoanza mbali. Unapozungumzia hatua (kwingineko wanaita
mchakato) katika uchaguzi, hata ukataji wa majimbo ya uchaguzi ni
shughuli ya uchaguzi.
Uandikishaji
wapiga kura ni sehemu ya hatua ya uchaguzi. Wanasiasa kuchukua na
kurudisha fomu za kuomba uteuzi wa Tume ya Uchaguzi zikiwa tayari
zimejazwa na kuambatanishwa wadhamini kwa idadi inayotakiwa kutegemea
na nafasi mtu anayoiomba, ni sehemu ya hatua za uchaguzi, wanasiasa
kuteuliwa kugombea ni sehemu ya hatua za uchaguzi.
Hatua
ya vyama na wagombea wao kufanya kampeni ya kuomba kura kwa wananchi,
upigaji kura, uhesabuji wa kura, utangazaji wa matokeo ya kura kwa
maana ya matokeo ya uchaguzi wenyewe, ni hatua zinazokamilisha
mtiririko mrefu wa shughuli nzima ya uchaguzi.
Kwa
hivyo, yapo makubaliano ya maandishi yaliyowekwa na Wafadhili na
Serikali zetu. Makubaliano hayo yanaleta maelewano ya wafadhili
kuingiza fedha kupitia Tume ya Rais ya Pamoja ya Usimamizi wa
Utekelezaji wa Muafaka (Joint Presidential Commission on Muafaka,
JPC). Fedha zote zinazohusu msaada wa nchi wafadhili kwenye masuala
ya uchaguzi zimekubaliwa kuingizwa kwenye mfuko wa JPC.
Ndani
ya mfuko huo, ndiko Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar inapata fedha zile
ambazo Wafadhili wameahidi kutoa kama mchango wao katika kufanikisha
uchaguzi mkuu Zanzibar. Palipotokea matatizo ya ubadhirifu wa fedha
za Wafadhili katika JPC, pamoja na mambo mengine, iliamuliwa na
Wafadhili na Serikali, kwamba fedha za uchaguzi ziingizwe moja
kwa moja katika akaunti ya ZEC.
Tume
ya Uchaguzi inapolalamika haina fedha, tutambue kwamba si zile
zilizoahidiwa na Wafadhili. Zi hizo jamani, ni fedha ilizoahidi
Serikali yetu tukufu kutoa kwa ajili ya kuchangia gharama za
uchaguzi. Serikali ina mchango ilokubali kuutoa usiopungua sh bilioni
1.6. Taarifa zinaonyesha kwamba mpaka Serikali inatoa tamko la kuwa
tayari kugharimia yenyewe uchaguzi wote, ilikuwa imeipatia Tume ya
Uchaguzi sh milioni 110 tu. Kiasi hicho hakijafikia nusu ya mchango
wake kwenye ufanikishaji hatua za uchaguzi. Shilingi milioni 110
katika sh bilioni 1.6 maana yake ni asilimia 11 tu ya mchango wote
inaotakiwa kuutoa.
Kitu
kimoja sina ubishi nacho: kwamba Serikali yetu tukufu inazo fedha za
kutoa lakini haijaona kama ni muhimu kuzitoa. Kwanini nasema na
ninaamini inazo? Ndio inazo kwa sababu inafanya matumizi mengi
mbalimbali yasiyo muhimu kwa mbwembwe nyingi. Kuna mambo mengi
yanafanywa kwa gharama kubwa lakini hayana ulazima wowote
kulinganisha na hali halisi. Lakini ndiyo Serikali yetu tusemeje kama
inatueleza bila hofu kwamba fedha nyingi zinakwenda kwenye miradi ya
maendeleo kwa hivyo wafanyakazi wavumilie mishahara inapochelewa?
Fedha ya mshahara kuhamishiwa kugharimia mradi wa maendeleo?
Tunaambiwa familia za wafanyakazi si muhimu mbele ya azma ya Serikali
kuleta maendeleo ya barabara na maji? Mtajaza nyinyi.
Serikali
haijatoa kauli kwa maandishi ya kutowahitaji Wafadhili kusaidia
uchaguzi. Kama si kweli tutaelezwa kama tulivyoelezwa kupitia tamko
kama tulilolishuhudia ndani ya STZ wiki iliyopita. Ni kwa sababu hiyo
bado Wafadhili wanafuatilia ufanikishaji hatua za uchaguzi mkuu
Zanzibar. Hawajatoka maana hawajaambiwa watoke. Waliingia kwa ruhusa
ya maandishi watatoka kwa ruhusa ya maandishi. Kauli ya Serikali ni
maoni tu.
Nilisema
na kauli ingalipo kwamba Wafadhili wawepo wasiwepo, Serikali ipige
kifua kugharimia isipige, Daftari la Wapiga Kura lazima lisafishwe
kama kweli tunataka, umma, na Serikali ya CCM inataka, uchaguzi uwe
madhubuti, kwa maana ya huru, wa haki na wa amani na utulivu. Kuwa na
daftari madhubuti ni njia ya kuwa na matokeo madhubuti ya uchaguzi.
Uchaguzi madhubuti hutanguliwa na Daftari madhubuti la wapiga kura.
Lazima umadhubuti upatikane kwanza kwenye Daftari ndipo uje uchaguzi
madhubuti na matokeo madhubuti. Hakuna namna nyingine, kama
alivyosema Andrew Massey wa Ubalozi wa Uingereza nchini. Ni haki kwa
umma kupatiwa Daftari safi, lakini ni wajibu wa Serikali kufanikisha
hilo. Kwa sababu haki inakwenda na wajibu kwanza, basi wajibu
unatakiwa utimizwe ili haki ipatikane.
Okay!
Tume ya Uchaguzi haitaki kusema lakini inasema. Niwaambie ukweli
inasema Tume kwa njia zake. Zipo taarifa za kutosha ya kuwa kazi ya
uhakiki haijasimama kusema la haki. Inaendelea. Wataalamu wa Waymark
wapo wanaendelea kufanya kazi hii wakishirikiana na wataalamu wa ZEC.
Ndio wanaifanya kwa sababu ni kazi muhimu kufanywa kwa maslahi ya
kweli ya umma. Uzoefu wa demokrasia za Kiafrika unaonyesha kuna
maslahi ya umma na maslahi ya taifa. Ya umma ni yale yanayohusu watu,
lakini ya taifa ni yale yanayohusu watawala. Ndivyo
nionavyo.
Serikali
inaposema haijaona umuhimu wa uhakiki kufanywa nje ya nchi inatizama
maslahi ya taifa si ya umma. Kuhakiki majina ya wapiga kura
hakuhitaji wataalamu kuondoka Zanzibar na Buku lenye majina 500,000
na zaidi, ni kitu cha kufungua kompyuta na kuelekeza mshale
panapotakiwa, na mtu unakuta majina yote, moja baada ya jingine.
Unalitazama utakavyo na unaliona kama lina kasoro au vipi. Kwa hivyo
hata aliyeko Marekani na Uchina, akitaka analitazama Daftari letu
huko aliko badala ya kulazimika kufika Maisara ya kufungua mitambo ya
Tume. Wanasema majina yapo kwenye vidole tu kutokana na teknolojia
iliyokua.
Maslahi
ya umma ni yanayotaka majina yatizamwe tu iwe isiwe ili machafu
yatoke kwenye Daftari. Hapa ndipo tutapata Mtu Mmoja Kura Moja.
Afrika Kusini walihangaika kwa miaka mingi kupata kitu hiki kiitwacho
One Man One Vote. Zanzibar hatuna chaguo leo kama tuko kwelini
kupata uchaguzi huru, wa haki na katika mazingira ya amani na
utulivu. Mtaalamu anapolitizama jina langu anakuta maajabu ndani. Ati
linakuja na jina jingine kwenye picha inayoonyesha uso wangu? Uso wa
mtu mmoja unakuja na majina mawili na hata matatu tofauti tofauti.
Nini hii kama si maajabu. Uthibitisho wa kuwepo watu walioandikwa
zaidi ya mara moja. Ndiyo yale ya kubainika majina zaidi ya yale
yaliyoandikwa vituoni wakati wa uandikishaji. Tukaambiwa ah hiyo ni
jambo dogo unapozungumzia takwimu. Jambo dogo Tume kutoa isabu ya
watu 499,000 baada ya uandikishaji kukamilika na ikatoke isabu
iliyozidi orodha za majina zilipobandikwa kwa uangalizi. Mimi si
bingwa wa hisabu, lakini mabingwa hawakubali. Siwezi
kubisha.
Ukisafisha
maajabu haya ya uso mmoja kukutwa na majina tofauti yasiyoendana na
alama za dole gumba, unatengeneza Daftari. Haitoshi, kumbe unaondoa
siri za watu kuzidisha idadi ya kura. Zimbabwe walipofanya uchaguzi
miezi michache iliyopita na chama cha ZANU PF cha Mzee mpigania uhuru
maarufu barani Afrika, Robert Mugabe, kuibuka na viti vingi vya
Bunge, kulikuwa na malalamiko ya kura hesabiwa kuzidi kura pigwa.
Waliopiga kura ni watu 30 lakini kilichohesabiwa ni kura 50, hizi 20
zilitoka wapi? Labda Zanzibar, twenye uhusiano mzuri unaostawishwa
kwa ziara, tunataka kufuata nyayo zao. Uchaguzi huru na wa haki una
kazi Afrika.
Yote
kwa yote. Uhakiki unafanywa na wala msishangae kuwa unafanywa kwa
sababu hata gazeti lao linalouza (sana) kulingana rekodi za
mawakala(?), limeandika likiisema Tume imeipuuza Serikali kwa
kuendelea na kazi ya uhakiki ambao kwayo gazeti na wamiliki wake
mabwana wa waandishi wa habari wenzetu maskini, ni kizungumkuti. Kama
ni kizungumkuti sawa, lakini si ni kwa maslahi ya umma? Au ni bora
maslahi ya Taifa?
Uhakiki
uendelee kufanywa maana ni muhimu. Ufanywe kwa umakini huku
tukisubiri na wale walioshinda rufaa zao mahakamani, na wale wengine
waliokwamishwa tu kwa sababu za kiufundi zisizowahusu, watangaziwe na
Tume njooni sasa muandikwe ili nao waingie katika Daftari kwa ajili
ya kuja kupiga kura ambayo ni haki yao ya kikatiba. Wanachotakiwa
kufanyiwa si upendeleo ni haki yao kama tunakubali Katiba ndio msingi
wa uendeshaji mambo yetu. La kama tuna mengine na tunaweka kando
Katiba, basi hakuna atalalamika ila Nguvu ya Umma itaja simama.
Mahangaiko kwa nchi zilizokuwa hazijataka demokrasia ya kweli, ni
jambo la kawaida. Haki haipatikani mpaka ipiganiwe. Ndani ya sahani
hii haki raia, haiwezekani.
Tume
msiseme kama hamtaki kusema. Tunawakubalia mbaki hivyo hivyo kimya
muradi kazi ya uhakiki inafanywa. Hilo la kufanywa uhakiki ndio
muhimu zaidi kuliko hili la kwamba kila kinachofanyika umma
ujulishwe. Tusipojulishwa leo tutajulishwa hata kesho mkitaka. Ndio
uzuri wa tunavyopeana dhamana, anayepewa ndiye muamuzi: akitaka
itakua asipotaka haiwi. Sivyo mbele ya muumba, atakavyo yeye huwa
wala hakuna kizuizi.
Ends.