Waraka Kutoka Unguja
September 15, 2005
By
Jabir Idrissa
Headline:
Kampeni ya kubomoa umma itaikifisha z'bar wapi?
Kampeni
kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 30 mwaka huu zimeanza. Wiki ya
pili inakatika tangu Septemba 5 kampeni ilipoanza baada ya Tume
ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kupitisha majina ya wagombea.
Kama
ilivyotarajiwa, tayari kampeni zimekumbwa na uhalifu. Yale yale
yaliyokuwa yakitokea wakati wa uandikishaji wa wapiga kura kwenye
Daftari la Kudumu, ya watu kuvamiwa na kujeruhiwa kwa mapanga na
marungu, yameanza kutokea.
Yanatokea
hayo, huku mitaani wengine wakipanga kuhujumu raia kwa sababu ya
picha za wagombea, kila chama kikidai uhalali wa kubandika za
wagombea wake na vingine kujiona ni vyenyewe tu vyenye haki ya picha
za wagombea wake kudumu.
Zote
hizo ni fitna za uchaguzi ulio huru, wa haki na unaotakiwa kufanyika
kwa amani na salama. Nchi yetu sote tusisahau, itatusuta.
Kama
vile haitoshi, kwenye majukwaa ya kampeni, kumeanza visa pia.
Wanasiasa wanatumia fursa hiyo adhimu ya kusikilizwa na watu, kulipua
mabomu bila ya sababu za msingi. Wapo wapotoshaji wa mambo,
wadanganyaji watu na watoa kauli za kutisha watu.
Cha
kushangaza ni kwamba hayo yanafanyika wakati vyama vinavyoshiriki
uchaguzi, vimetia saini makubaliano yanayoitwa maadili au misingi
mahsusi kwa lengo la kuhakikisha hatua iliyobaki ya kuelekea upigaji
kura ikianzia na kampeni inafanyika kwa utulivu na heshima na
hatimaye Zanzibar inapata viongozi watakaokuwa na thubutu ya kujitapa
kuwa wametokana na uchaguzi madhubuti.
Zanzibar
ipate chama madhubuti kitakachounda Serikali imara na itakayokuwa
Serikali ya watu, kwa ajili ya watu na kwa manufaa au maslahi ya
watu. Serikali itakayoongoza watu si kutawala watu, itakayojali haki
za kila raia na kila sehemu ya jamii kwa usawa na bila ya kutumia
ubaguzi wa aina yoyote ile. Nchi inahitaji Serikali madhubuti
itakayoheshimu haki za binadamu na itakayokuwa mfano wa utawala bora
na utawala wa sheria. Kila mtu atumikie sheria siyo mwingine au kundi
fulani liwe juu yake.
Hali
inaonyesha nchi inapita katika kipindi kigumu kweli. Kipindi kigumu
kwa sababu wakati huu tunapaswa kufikiria maendeleo yetu mtu mmoja
mmoja na ya nchi kwa jumla. Hata hivyo, baadhi yetu tungali na mawazo
ya umimi na mtizamo wa kuwa watu fulani tu ndio halali wa kuongoza
nchi na wengine, wao ni watizamaji tu.
Tunaposema
vyama vimekubaliana kuendesha kampeni za kistaarabu na zinazojali
msingi wa utaifa wa nchi yetu, vipo vyama vinavyoamini kwamba tungali
katika zama za kutiliana fitna kwa kutajana majina mabaya majukwaani.
Mwanasiasa anatumia sehemu kubwa ya muda jukwaani kwa kutoa maelezo
yanayolenga mtu katika namna ya kumchonganisha na umma. Dalili ya
kukosa hoja?
Muflis
kwa sababu anafahamu fika anachotakiwa kukizungumzia ni sera za chama
chake na vile zitakavyotumika kubadilisha hali ya maisha ya
Wazanzibari na nchi yao (kwa maana ya ustawi zaidi) katika nyanja za
kiuchumi na huduma za kijamii. Hilo ni kwa chama kinachoomba ridhaa
ya kuongoza kwa mara ya kwanza.
Kwa
chama kinachotawala, chenye kuongoza watu tayari na kinachoshindana
ili kibaki kwenye madaraka hayo, kinapaswa kueleza kimepiga hatua
gani kutimiza mambo hayo kwa mujibu wa vile kilivyoahidi wananchi
katika Ilani yake ya uchaguzi uliopita, wapi kilikosea na wapi
kinakusudia kupaimarisha ili kuonyesha uwajibikaji kwao. Chama hiki
ndicho kinakuwa na changamoto zaidi kwa sababu kuna vipimo vingi
kwake kukionyesha kama ni kina dhamira ya kweli ya kujenga nchi na
wananchi wake.
Kipo
madarakani, na kwa sababu tunazungumzia Chama cha Mapinduzi (CCM),
kule kuwa kwake kwenye utawala wa nchi kwa miaka 41 ni nafasi nzuri
ya kujilabu lakini kwa hoja zinazoendana na uhalisia wa mambo. Kila
kitu kinaonekana. Kama Serikali ya CCM imekifanya hakuna haja ya
malumbano, kinaonekana. Nimepata kusema kama maendeleo yanaonekana
hakuna sababu ya kupigiwa debe kwa sababu kila mtu anayaona.
Kama
ni barabara imejengwa, kila mtu anaiona, kama tangi la maji
linaonekana, kama ni skuli na vifaa vya kisasa kulingana na wakati
tulionao wa sayansi na teknolojia, vilevile. Kama ni kituo cha afya
au hospitali na uhakika wa dawa na umadhubuti wa madaktari na
wafanyakazi wengine ni sawa, kama uwanja wa ndege na vifaa vyake, au
uwanja wa michezo, vyote vinaonekana si vipo?
Katika
kueleza mafanikio ya Serikali inayoomba ridhaa ya wananchi,
ilitarajiwa hicho kuwa ni kitu rahisi kisichohitaji kuitisha mkutano
na kuchukua watu kutoka kisiwa kimoja na kuwapeleka kisiwa kingine.
Kule uendako kuna watu na kama wamesaidiwa katika jitihada za
kuondokana na umasikini wa kipato, umasikini wa miundombinu,
watamsikia muombaji kura. Hakuhitajiki mzo wa bunduki kuhutubia watu
hawa.
Basi
ingetarajiwa kampeni za uchaguzi zingeanza vizuri kwa sababu
tunapaswa kuamini kuwa kila chama kina nia thabiti ya kutaka uongozi
wa nchi kwa maslahi ya umma si maslahi ya taifa. Chama kinataka
ridhaa ili kiwatendee watu yale wanayoyataraji siyo yale
yanayotarajiwa na chama chenyewe.
Ilani
ya uchaguzi ya chama inatakiwa kutizama mahitaji ya jamii kulingana
na mazingira wanayoishi. Umma wa Wazanzibari hauhitaji sera za njozi
bali thabiti zitakazowezesha watu kutoka katika balaa la umasikini,
ujinga na maradhi. Watu wanahitaji sera makini za kuwapatia makaazi
bora, maji safi na salama, kupata uwezo wa kununua
wanachokitaka.
Lakini
unaweza kuwa na sera nzuri zikashindwa kutekelezeka kwa sababu
tunakosa umadhubuti katika viongozi. Wakiwa legelege watatoa Serikali
legelege na hatimaye, mipango legelege na huduma legelege. Ilani
inatakiwa kutandika misingi ya kuijenga upya nchi iliyovurugika
kutokana na mifarakano isiyokwisha. Panataka tafakuri Zanzibar ipo
wapi; kwenye umoja madhubuti au mgawanyiko wa aibu? Ilani itizame
hapa na kuendeleza umoja uliopo, si hivyo ijenge msingi wa
kuunganisha watu waliofarakana. Ilani ya uchaguzi ni muongozo wa
chama kuipeleka nchi kwenye neema si kuzidi kuitia katika
shida.
Haya
ndiyo mambo muhimu ya kuzingatiwa na vyama vya siasa
vinavyojitayarisha kuchukua hatamu ya kuongoza nchi. Safari hii
tunavyo sita vyama namna hii. Hivi ni vyama vilivyosimamisha wagombea
urais wa Zanzibar.
CCM,
chama tawala, kimemsimamisha Amani Abeid Karume; Chama cha Wananchi
(CUF) kinaye Seif Shariff Hamad; Democratic Party (DP) yupo
Abdalla Ali Abdalla; Jahazi Asilia wao ni Haji Mussa Kitole; National
Reconstruction Alliance (NRA) wanaye Simai Abdulrahman Abdalla na
Sauti ya Umma (SAU) wamempa dhamana Mariam Ahmed Omar, mwanamke
pekee.
Nilieleza
awali kwamba kampeni ya fitna, uzandiki na vitisho imeanza. Kama vile
hatujajifunza kitu muda wote tangu tuanze hatua ya uchaguzi.
Tunaendelea kushuhudia vitisho si tu kwa wanasiasa wanaogombania,
bali kwa raia wasio na hatia. Tunashuhudia umma wa Wazanzibari
ukilazimishwa kuishi katika hofu kuu.
Wanasiasa
wanapotaka kukisema kitu lakini wanajua kuna ukuta unawazuia,
hutafuta njia ya kusema wakianzia na maneno ya kuonyesha hawana nia
mbaya ya kuruka ukuta ule. Nami sikusudii kufanya kampeni ya kumtakia
yeyote kati ya hao wagombea sita au vyama vyao kushika dola. Umma
unajua unachohitaji. Langu ni masikitiko ya namna mambo
yanavyokwenda.
Tunacho
chama dola tunachotaraji kiwe mbele katika kuheshimu yale maadili na
misingi ya uchaguzi huru, wa haki na katika mazingira ya amani na
salama. Mbona hali haiendi hivyo? Mbona kuna wingu na hivyo giza nene
la kufika huko tutakako? Tupo kwelini au tunadanganya? Hatudanganyi
tunajidanganya tukidhani hatuonekani. Tuko wazi kila kitu
kinaonekana.
Picha
tu za wagombea inakuwa nongwa kuzivumilia? Watu wazima wanapanga
namna ya kuharibu picha za wagombea. Kama vile hawana kazi ya
kufanya, wanajadili namna ya kubomoa picha za wenzao. Wanajadili
namna ya kuziharibu halafu kutafuta wachawi. Mtu mzima anamwambia
aliyekutwa anatoa picha za wagombea bila ruhusa akabadili maneno. Eti
aseme alitishiwa kuuawa kwa kisu. Kwani zikiwepo picha za wagombea
wote sehemu, ndio wa kushinda atashindwa? Mgombea hashindi kwa uzuri
wake, bali anavyoutizama umma kama binadamu?
Watu
wazima wanapanga namna ya kuvuruga mkutano wa mpinzani wake. Mkutano
wa kampeni kwa ajili ya kuomba kura unapangiwa njama uvurugike, bado
mwanasiasa anajitokeza na kutamba jukwaani yu katika chama kinacholea
demokrasia. Demokrasia gani ya kuharibu mkutano wa kampeni.
Demokrasia inahimiza uvumilivu kutokana na kukubali hali halisi ya
mambo. Kuvuruga mkutano kwa kutumia watoto wanaochipukia, ndio
uvumilivu?
Bado
hatujajifunza kitu miaka 13 ndani ya mfumo wa vyama vingi. Uvumilivu
ni neno muhimu la kutiwa akilini mwa kila mtu, awe kiongozi wa chama
au mwanachama, awe raia tu asiye chama cha kukipenda. Uvumilivu
unapoondoka akilini, kinachofuata ni hamasa na hatimaye
uhuni.
Inakuaje
mtu na akili yake amfundishe mwingine kuchukua jiwe, kubeba nondo au
rungu lilovishwa misumari na kuagiza uharamia dhidi ya raia.
Upunguani wa hali ya juu katika nchi yenye historia kubwa ya
ustaarabu na upendo miongoni mwa watu wake. Ndani ya jamii ya watu
wanaoishi tangu zama wakipendana na kuelewana licha ya kutofautiana
kidini na kiasili, wachochewe kuvurugana.
Watu
waliumizwa vya kutosha 2001, wameumizwa vya kutosha ndani ya
utekelezaji wa Muafaka uliozaliwa kutokana na maumizaji yale. Watu
wameumizwa wakati uandikishaji ukiendelea vituoni, watu waliuawa
kinyama kwa mtutu na visu. Mali za watu zilihujumiwa wengine
hawajasimama tena kibiashara, wazee kwa vijana walitiwa kwenye
mitihani kimaisha na wahuni. Haijatosha tu? Aibu na
ajabu.
Zanzibar
lazima turudi kwenye mstari. Kila mtu arudi. Ajiweke nafasi ya kuwa
miongoni mwa wale walioongoka si katika wale aliowaghadhibikia Mola.
Tumeumbwa kupendana na kusaidiana si kuhujumiana. Kama tuhujumiane
tofauti yetu na wanyama mwitu iko wapi? Tunakubali madaraka ni
matamu, lakini gharama ya kuyahakikisha ndio iwe kuhujumiana? Kwa
kumtusi mwenzio, kwa kumchonganisha, kumharibia jina mwenzio, kwa
kusema ya nyumbani kwake, kwa kutumia historia kummaliza? Ni
upotoshaji usio na sababu wala tija.
Ningekuwa
mimi ningezungumza mazuri matupu niliyoyafanya bila ya kusahau
kueleza kasoro kwa sababu zinajulikana kuwa zilinisaidia kukwamisha
azma ya kuiletea jamii neema. Kasoro ni kupotea njia ambako ni kujua
njia, maana zimenifunza namna ya kubadilika na leo nina ari mpya na
nguvu mpya lakini ndani ya fikra mpya na kwa hakika za kileo si za
kale za mwaka 47. Leo nitende mambo kwa ustadi zaidi kwenda na
teknolojia.
Hii
ndiyo kuungama, nasi tunapaswa kuungama kwa kutoukiuka ukweli japo
unauma. Ni sawa tu kama ulipanda kokwa ya papai, wewe uliye
madarakani, na wewe uliye nje unahitaji kuingia ndani, usitaraji
kuvuna mbaazi. Zipo hadithi za kokwa ya chungwa kuzaa danzi lakini
hiyo ni miujiza si uhalisia. Ni katika Mola kuonyesha yeye ndiye
yeye.
Tatizo
langu siku zote limekuwa ni kuona tuna Serikali iliyosahau majukumu
yake kwa umma. Sigusii uchumi wala huduma za jamii, nabaki hapa
kwenye usalama wa raia. Ni udhaifu mkubwa wa kiuongozi, unapokuwa na
Serikali isiyojali amani ya raia zake. Kujali kuwe kwa vitendo si
maneno tu ya amani na utulivu huku raia wengine wanajiona bora kuliko
wenzao. Wanachukua rungu na mapanga kupiga wenzao, wanachoma nyumba
za raia wenzao, wanahujumu mali za wenzao, na haiwi chochote. Sasa
huu si utawala bora wala wa sheria. Huo ni ushahidi wa utawala mbovu.
Raia ndiye mchangiaji mapato ya serikali ili iwe kujiendesha,
ukimhujumu ndiyo unajenga maisha yake au unambomoa? Ukimbomoa ndio
unazalisha mapato?
Wagombea
tuzungumzie siasa, tuzungumzie sera, tujikite katika masuala ya
kujenga nchi na jamii. Tuache fitna majukwaani, tuache uongo na
uzandiki, tuache matusi na kejeli, tuache uchonganishi, tuache
kumalizana kwa chuki. Tuitumie vizuri historia, tujenge kutokana
nayo. Tujenge hoja na tuitie nguvu hoja ili ikubalike. Tusilipue
mabomu hayatusaidii.
Yote
haya yamehimizwa kwenye maadili au misingi mahsusi ya kuleta uchaguzi
mzuri ambayo vyama vimesaini. Tuyaheshimu basi kwa maslahi ya umma.
Tutimize wajibu wetu kwa umma tunaotaraji kuuongoza kwa kuuletea
neema.
Ends.