Waraka Kutoka Unguja
March 17, 2005
By
Jabir Idrissa
Wanaukumbi wenzangu, ifuatayo ni makala ya kila wiki
katika gazeti la Rai. kwa kufahamu baadhi yenu hampati nafasi ya
kulisoma gazeti hili, nawatilia hii makala mpate kufaidika na
yanayotokea kwetu Zanzibar. Ahsanteni.
Jabir idrissa+
Kichwa
cha habari: Hivi tuendelee kutiana misukosuko ya maisha hadi lini
Z'bar?
Niliahidi wiki iliyopita kutumia
safu hii leo kuibana Polisi kama taasisi ya kulinda usalama wa raia
na mali zao ikiwemo jukumu kuu la kusimamia utekelezwaji wa sheria za
nchi. Ahadi yangu ilitokana na imani ya kuwa taasisi hii imekuwa
haitekelezi majukumu yake ipasavyo wakati mwingi.
Imani
hii haikuja leo wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu, nimekuwa nayo
zamani ndio maana huko nyuma taasisi yenyewe iliona makala zangu
kupitia gazeti la Mtanzania, na kabla ya kuingia hapo.
Kipimo changu cha utendaji kazi wa taasisi ya Polisi wala
hakitumii vigezo vigeni. Ni kutizama tu namna inavyoyachukulia na
kuyashughulikia matukio mbalimbali. Kumepata kutokea mauaji ya raia
wasio na hatia, wengine ndani ya mamlaka ya taasisi hii lakini
hakutolewi maelezo ya kuridhisha, basi huwa nalaumu na kushauri
utendaji wa kweli.
Lakini pia nimepata kupima utendaji
wa Polisi kwa kutizama inavyoshughulikia matukio yenye mitizamo ya
kisiasa, na hususan yanapokuwa yametokea upande huu wa Zanzibar. si
jambo geni kwangu kuitia taasisi hii katika mtihani wa kuibana
iwajike kikwelikweli kwa kufuata sheria za utendaji wake na za nchi.
Iwajibike katika usawa si kwa kubagua matukio.
Nimepata
kutamka wazi mara kadhaa kwamba Polisi huwa inajibadili na kuwa sasa
taasisi ya kutumikia wanasiasa wa chama tawala badala ya kutekeleza
majukumu yake kwa uadilifu unaohimiza usawa kwa vyama vyote vya
siasa. Polisi inajitambulisha kuwa ni taasisi ya kutumika kutekeleza
matakwa ya utawala badala ya kufanya maamuzi kwa kuzingatia sheria.
Na hii kutumika kukidhi matakwa ya kisiasa ya chama tawala, CCM,
haipatikani mpaka kwanza 'waumizwe' wananchi, viumizwe vyama vya
upinzani, waumizwe viongozi wa upinzani.
Niliposema
waraka uliopita ya kuwa taasisi hii imedekeza kwa muda mrefu vitendo
vya fujo mitaani vinavyofanywa na wakereketwa wa CCM kiasi cha
kujiona wako juu ya sheria, nilikuwa nalenga hali inayotokea Zanzibar
kipindi hiki. Walimzoesha mbwa kuingia mwilini na sasa anawafuata
hadi wanapoingia msikitini.
Fujo tupu mitaani, vurugu
haziishi kwenye maeneo wanayokaa zaidi wafuasi wa upinzani. Imeanza
kuwa fasheni kwa wiki ya pili kutokea vurugu eneo la Amani penye
Ofisi Kuu za CCM Mkoa wa Mjini Magharibi. Kwanini patokee vurugu hapa
kama Polisi wanapalinda. Jumapili walikuwemo ndani ya jengo na silaha
zao, zitatokeaje vurugu wakiwemo ndani kama si kuishiwa maarifa
katika utendaji kazi?
Wala hali hii haiji kwa bahati
mbaya. Si bahati mbaya asilani. Kwanini magari mawili ya Polisi
yalikaa mbele ya geti kuu la uwanja wa Amaan kabla ya mkutano wa
Chama cha Wananchi kumalizika? Wanamlinda nani pale, raia wanaopita
au pale ndio wanalinda Ofisi ya CCM, iliyo mita 100 hivi kutoka hapo?
Lakini kwanini pale uwanjani wawepo halafu na ndani ya jengo la CCM
wawemo tele na silaha nyingi?
Na kwanini suala la vurugu
za kisiasa ndani ya Mkoa sasa ziwe ni tukio la kushughulikiwa
kihabari na Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI)
Makao Makuu ya Polisi Ziwani? Kwanini isiwe Kamanda wa Polisi Mkoa
(RPC), George Kizuguto tunayejua ndiye mwenye dhamana ya ulinzi wa
raia mkoani? Vurugu hizi ni kubwa kuliko za kusambaratisha biashara
za raia wema pale Jua Kali usiku wa manane? Mbona operesheni ile
ndiyo ilitia hasara kubwa raia wa nchi hii walioajiri baada ya
serikali yao kushindwa kuwajengea uwezo kielimu wakakabili mazingira
ya utandawazi?
Kusambaratisha biashara za raia masikini
wale ambao hadi leo hawajapatiwa eneo la kufanyia biashara kama vile
si raia kitu, ni hasara. Kuvunja maghala ya bidhaa za wafanyabiashara
kando ya Soko Kuu la Mwanakwerekwe na kuzitia kwenye magari ya wazi
baada ya kuwapiga walinzi, ni hasara nyingine hii.
Hasara
iliyowapata wafanyabiashara kwa sababu bidhaa zao ziliibwa na
walioendesha operesheni safisha mji na kupelekwa kusikojulikana kwa
magari yenye walinzi wa kipolisi na wa vikosi labda vya Valantia au
Mgambo, yakianzia kituo cha Polisi Mwanakwerekwe na kuelekea Kwa
Mchina, ni kubwa si mchezo. Na bado ilifanikiwa kutokana na mipango
iliyoandaliwa na ofisi ya RPC Kizuguto, chini ya mwamvuli wa Baraza
la Manispaa la Mji wa Zanzibar. Mbona kazi nzito ile ilifanikiwa
isiwe hii ya kujenga mazingira ya kuvuruga akili za watu mitaani
mjini Unguja?
Au RPC Kigutuo amekwenda likizo na hakuna
ofisa wa kushika nafasi yake kihabari mpaka waandishi tuitwe kwa DCI
saa 8 mchana kuelezwa tukio la kihuni lililotokea zaidi ya saa 12
zilizopita. Unaitwa saa nane mchana ili iwe nini? Sisi waandishi
bwana tunafanya kazi kwa muda. Au ni makusudi ili tusipate kuwabana
wakubwa wa Polisi kutaka ufafanuzi?
Na leo Polisi iite
waandishi pale vurugu zinapokuwa na mwelekeo wa kuwa zilipangwa na
wenyewe zitokee: zimeandaliwa mapema ili kukidhi matakwa ya wakubwa.
Na bado unaambiwa eti hakuna mtu aliyeumia wakati watu kadhaa
wamepigwa na kuumia. Hiki ni kitanzi kwa Polisi kama taasisi, na
haiwezekani muendelee kukaa nacho. Kitoeni shingoni mfanye kazi zenu
kwa ufanisi, msemwe vizuri na wengi si watu nusunusu.
Vurugu zitokeazo kwenye mitaa kwa wiki ya pili sasa ni mpango
madhubuti usiokuwa wa bahati mbaya, kwa namna nionavyo. Mpango
maridadi uliobuniwa kuzusha hofu miongoni mwa raia hasa wanaodhaniwa
hawaipendi CCM. Raia ambao haki zao zinategemea huruma ya mtu si
sheria na kanuni. Raia ambao hawana la ukweli wala nini, kwao ni
kuonekana waongo tu na watungaji sababu ili ionekane eti wanaonewa.
Wataalamu wa masuala ya kijamii wanaziita vurugu kama
hizi state-organized chaos. Watumishi wa umma wanatumwa kubuni na
kutekeleza mipango ya kuhujumu baadhi ya raia wema (kwa sababu zao
wao, wanawaona adui raia hawa) ili tu kundi fulani au watu aina
fulani wapate kutiwa katika msukosuko na vyombo vya dola. Utawaona
watumishi hawa baadhi wanakuwa mbele au nyuma wakisimamia utekelezaji
wa mipango hii ya hujuma dhidi ya raia wema.
Ikitekelezwa
mipango namna hii, wahusika katika utawala wanatumwa kutoa matamko ya
kulaani vurugu au matukio ya uharibifu wa mali, nyingine huwa za
umma, na utasikia waziwazi wakitaja kwamba chama fulani cha upinzani
au wapinzani ndio waliohusika.
Kufahamu zaidi hoja hii,
niwakumbushe ya milipuko ya mabomu; nikiita mabomu ya kishetani
ambayo mpaka leo ripoti ya uchunguzi wake umma na ulimwengu
unaisubiri. Inajulikana matokeo ya uchunguzi ule lakini itolewe wapi
wakati hakuna mtuhumiwa aliye nje ya mfumo wa dola? Ndio maana
tunaendelea kuisubiri mwezi wa 12 kamili leo.
Natuendelee
tu kuisubiri maana labda akina Afande R.M waliopewa kazi ya
kuchunguza ikiwemo kutumia mbwa wanusaji, hawajamaliza kazi ya
kuiandaa. Haitatokea siku kwa utawala huu tulonao ikatolewa hadharani
ripoti ile. Naweza kutia dau la shilingi mia moja, haitoki labda
yatokee mabadiliko na wake watu wenye utashi wa kuona demokrasia na
utawala wa sheria vinafanya kazi kwa kuonekana si nadharia.
Sisi Waislam tunaamini kazi ya Mwenyezi Mungu haina makosa,
akitaka inakua hakuna wa kuzuia asipotaka haiwi hakuna wa
kushinikiza, ndio maana hata tunapoomba dua ya kutaka mema, huwa
tunategemea ukubalifu wake. Hapa si kama Zuia Uhuru ya miaka ya kabla
ya 1963. mtu azuie uhuru lakini si atakayo Mola.
Wengine
mnaweza mkawa mnajiuliza "huyu kawa kichaa leo" kwa kuamua
kuropokaropoka tu humu, au amechukua hulka za kasuku kutoa maneno
aliyolishiwa. Asilani abadani sijapata kulishiwa na siko tayari kwa
sababu kichwa changu bado "kinaona mbali" hakihitaji
kutengenezewa mada. Wala sijafikia hali ya kuchanganyikiwa na
kuhitaji kwenda Kidongochekundu (mfano wa Mirembe kwa walioko
Tanzania Bara). Niko fiti.
Kama hamuamini kuna hujuma
hupangwa kwa makusudi kwa nia ya kutia baadhi ya raia katika
msukosuko, nikupeni ya mwandishi wa vitabu wa Kimarekani, Charles
Evers, mwenye asili ya Mississipi. Katika kitabu chake alichokiita
Have no Fearkilichochapishwa mwaka 1997 na John Wiley & Sons
Incl.; anasema katika ukurasa wa 5-6: niache alivyosema kwa
Kiingereza nitatafsiri.
But when the police and the
politicians wink at these killings and cover them up - that's worse
than violence. That's state-sponsored terrorism. And that was
Mississipi in my childhood. Cops killed Negroes all the time and
called it justifiable homicide.
(Lakini pale polisi na
wanasiasa wanapochekelea mauaji haya na kutoyashughulikia - hiyo ni
hatari zaidi kuliko ghasia. Hiyo ni ugaidi uliopangwa na dola. Na
hiyo ndiyo Mississipi ya utotoni kwangu. Polisi walikuwa wakiua
Waniga (Wamarekani weusi) siku zote na wakihalalisha (mauaji hayo).
Bado hatujashuhudia mauaji tangu yale ya mwanafunzi Juma
Omar Juma yaliyotekelezwa na mlinzi wa kidola Disemba 3, mwaka jana
Mkoani Pemba, lakini naona hatuko mbali na huko. Kama utawala
utaendelea kukubaliwa mambo yake na taasisi ya Polisi tunayoitegemea
kwa ulinzi wetu na mali zetu, mauaji haitakuwa jambo lisilowezekana.
Tunapoelekea kwenye uandikishaji mkoani Mjini Magharibi penye zaidi
ya asilimia 40 ya wapiga kura, makubwa tunayasubiri kutokea.
Ufanyeje utawala wakati Mambo Ni Magumu (MNM)? hata ingekuwa mimi
kama sijataka kubadilika na kuwa wa kukubali hali halisi ya mambo,
nikiwa niendelee tu kubaki mhafidhina wa kutupwa, lazima nitumie
mbinu zote ili kulinda utawala wangu kwa sababu nisipofanya hivyo,
jamaa watanikwapua kwenye utawala. Wakishanikwapua pale nitakula wapi
wakati pale ndio pekee pananipatia riziki yangu na wanangu na lile
kundi dogo la mawakala zangu? Ndio maana nitashikilia kusema
nitashinda kwa kishindo kingine na sababu ni moja tu "chama hiki
kina watu wanaokiunga mkono."
Itabaki kuonekana
kwamba Zanzibar pangali mahali pasipo shwari, bali kila wakati raia
zake watiwe katika mtihani wa kuhofia maisha yao kama vile kuishi si
haki yao ya msingi. Mohamed Ali Maalim leo anahangaika kujiuliza hivi
atamaliza lini kufuatwa na Polisi kila panapotokea hali ya wasiwasi
mjini wakati hana kosa. Hajapata kuthibitishwa ni mkosaji wa jinai
hata mara moja, licha ya kukamatwa mara kwa mara, lakini bado
anafanywa chambo.
Na hafuatwi mchana kweupe, usiku wa
manane maana ndipo atapojua kwamba kuna dola inayohitaji kuheshimiwa
na kutetemekewa kila wakati. Jamani dola ipi hii inayotia hofu raia
kila wakati kama si namna ya utawala utumiao sheria za mwituni? Ndio
huendelea kusema lazima ifike wakati tubadilike sote, kila mmoja na
kwa ujumla wetu, ili tujenge Zanzibar ya kukaliwa kwa utulivu na
watoto zetu. Si hivyo, haya natuendelee kutiana kwenye mitihani ya
kimaisha.
Ends.