Waraka Kutoka Unguja

April 1, 2005.


By


Jabir Idrissa


Wanaukumbi, someni makala hii ya Waraka kutoka Unguja iliyochapishwa katika gazeti la Rai la Machi 31. Zaidi ni kwa faida ya walio nje ya nchi na wengine walio mbali na yanakofika magazeti nchini TZ.   Mwanaukumbi mwenzenu, Jabir Idrissa+   Headline yake: Twasubiri Utawala Bora kweli, Tume yetu uamuzi ni wao

 

Kupitia ukurasa huu huu, nimewaletea visa na vituko vya kupwa na kujaa vinavyohusiana na yanayotokea wakati wa uandikishaji watu kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK). Mengine yametokea bila ya kusahau maafa ya kupotea roho za watu, raia wenzetu wawili, chanzo kikuu cha hayo kikiwa ni utawala wa mabavu.

 

Roho ya Juma Omar Juma, mwanafunzi wa shule ya msingi ya Ng’ombeni Mbuyuni, mjini Mkoani ilikatika ghafla kwa sababu ya matumizi yasiyo lazima ya nguvu za dola kwa ajili tu ya kulinda maslahi ya utawala. Alipigwa risasi na askari wa Kikosi cha KMKM aliyekwenda na wenzake kituo cha uandikishaji wapiga kura kwa nia ya kuzuia upinzani wa wenyeji wa eneo la Mkoani waliosimama kidete kuzuia wageni kuandikwa hapo.

 

Roho ya pili ni ya Kamanda wa Valantia Pemba, Mohamed Suleiman aliyeuawa kwa kuchomwa kisu kifuani usiuku wakati akitoka nyumbani kwake kwenda Msikiti wa Chachani mjini Chake Chake kushiriki sala ya Isha. Wengi wanakihusisha kifo chake na masuala ya uandikishaji kwa vile kikosi anachokiongoza, KVZ, ni moja ya vikosi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, vinavyotumiwa kuvuruga daftari. Uvurugaji ninaousema hapa ni ule unaotekelezwa kwa mtindo wa kuhamisha huku na kule askari wa vikosi hivyo kwa madhumuni ya uchaguzi tu.

 

Kwa bahati mbaya (sana) kwa sababu ya kutojali haki za raia na kutozingatia misingi ya utawala wa sheria kwa vitendo, muuaji wa Juma hajabanwa pamoja na kujulikana. Hapo hapo, watu saba walikamatwa wakihusishwa na kifo cha Kamanda Mohamed, akiwemo muathirika wa matumizi ya dawa za kulevya, mwenyeji wa mjini Unguja. Walikamatwa kivarange tu na labda miujiza itawatia hatiani. Wangali wakisota gerezani Wete tangu walipokamatwa Disemba 5.

 

Tunazungumzia utawala wa sheria wa vitendo si nadharia. Serikali inayofuata utawala wa sheria inajionyesha si kwa kelele na viongozi kujinasibu kwenye viriri. Utawala wa sheria au utawala bora ni kutenda haki kwa kila raia hata pale serikali ikibidi kuumia. Askari waliomuua aliyekuwa Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa nchini, Kanali Imran Kombe na ushahidi ulipothibiti wakatiwa hatiani na serikali kutakiwa kulipa mamilioni ya fidia, ndio malipo ya haki ya kutoheshimu sheria. Na Serikali haina isipokuwa kulipa tu wakati ukifika. Hii ndio utawala wa sheria.

 

Yetu ina mwaka wa ngapi inashindwa kumsaidia Mzee Abdalla Shariff wa Shakani haki aliyopewa na Mahakama? Kuondolewa kwa wavamizi wa ardhi anayoimiliki kisheria kunahitaji kupeleka vifaru vya jeshi si wanaoitwa FFU ambao huenda na kunusa wavunja sheria; watoto na wanawake wenye bakora, na kupindisha gari wakirudi kituoni kamanda wao akisema “du mnaona moto ule na silaha walizokamata.” Aibu tupu kwa Polisi wanotumwa kila baya.

 

Leo tuna raia wangapi vituoni waliokamatwa siku kadhaa nyuma bila ya kusomewa mashitaka mahakamani. Saa 48 za kisheria zimefutwa? Inakuaje Polisi inavunja nyumba ya raia asiye na silaha usiku wa manane na kumfungulia kesi ya uzembe na ukorofi kwa kumkuta na panga au kisu au shoka au mtaimbo? Mzanzibari bila kisu, panga, mtaimbo, shoka, mkuki, jembe na nyundo? Na waliogawa mapanga mchana kweupe huku mawaziri wa SMZ wakichekelea; wanaouza zana hizi za kazi mpaka chini ya miguu ya wapita njia mjini; na ile dhana ya kuwa Zanzibar ni nchi ya wakulima na wakwezi? Itakuwa imekufa kwa sababu awaje mkulima au mkwezi bila ya kisu au panga? Awaje mkulima wa maweni bila mndu, mtaimbo na mkuki?

 

Utawala bora huku magazeti yanayoikosoa serikali yanafungwa na waandishi wake kujengewa chuki? Bali yanayochonganisha watu yanaishi baada ya kupewa leseni haraka haraka. Leo Zanzibar si sheria, mtu azitegemee kumlinda na au kupata haki bali mapenzi ya mtu. Si elimu na maarifa inayompatia kijana kazi, bali ukereketwa. Mpemba leo si mali kitu ila karafuu zake? Leo tunafundisha vijana uharamia halafu twasema tuna utawala bora na kwamba utawala bora hauji miaka minne. Waja hata kwa miwili, dhamira tu!

 

Hatujaufikia wala hatuufikii kwa hata miaka 100 kwa mtindo huu uliojaa utani wa nguvu. Tutaendelea nao utawala wa mabavu na ushetani iwapo wenye hatamu za uongozi wa Serikali hawataki kuwa mfano katika ufuataji sheria bali kulalamikia wapinzani tu hata pasipo sababu ya kweli.

 

Changamoto iliyobaki kwa Rais Amani Abeid Karume kuthibitisha kama anaongoza serikali inayoheshimu sheria ni kuchukua hatua ya kumvua sare askari wa KMKM aliyemuua Juma, afunguliwe mashitaka kwa kuwa upo uhakika ndiye aliyehusika na yule ofisa aliyeamuru Juma atwangwe risasi naye awajibishwe kwa kukiuka sheria hata za uaskari. Si zipo sheria za wakati na mtu gani wa kufaa hupigwa risasi ya kumuua? Kama hilo ni gumu kama la mtu kujua lini atakufa, basi na wale watu saba wanaosota gerezani waachiwe.

 

Kama yote hayafanyiki, iko siku muuaji wa Juma na wengine wasiokuwa na hatia, watalipa damu na roho za Muumba, na wale watu saba watajadai haki yao wasipothibitika kuhusika kumuua Kamanda Mohamed.

 

Hawataki bado watawala kukubali hali halisi; kuamini ya juzi si ya jana na hata ya jana si ya leo tena mwiko kwao. Ni kazi yetu kuzidi kuwapigia baragumu ya kuwa kwa tulipo leo, haiwezekani kurudi nyuma tukaishi kama walivyoishi babu na bibi au baba na mama zetu miaka ya khamsini na sitini. Watambue na lazima wafike mahali wajue hasa kama ya leo ni ya leo hayawezi kulingana na ya juzi na jana. Leo tunazungumzia ubinafsishaji, tuna utawala bora, tuna utandawazi.

 

Hata kipindi hiki tu cha kitimtim cha Chama tawala kutafuta wagombea urais, tunapata misamiati mipya tusiyopata kuisikia kipindi kama hiki mwaka 1995 wala 2000. Tuna uendelezaji wa mafanikio ya Serikali ya CCM kwa ari mpya, kasi mpya na nguvu mpya. Ni sauti ya mabadiliko ya kumridhisha binadamu Mtanzania kwa mahitaji muhimu ya kimaisha. Ndio kupea kwa binadamu. Binadamu wa yale mafuvu yanayogunduliwa leo, si tuliyepo leo, ni tofauti kwa mengi.

 

Lililo bora ni kutafuta yatakayotusogeza mbele na kuwa sambamba na mataifa yenye dhamira za dhati kuendeleza watu wao, yenye kujenga misingi ya kweli ya uongozi yenye maslahi na nchi na watu wake, uendeshaji unaozingatia umuhimu wa raia kwanza ndipo mgeni, uendeshaji unaojali haki na usawa wa watu bila ya ubaguzi kwa rangi, kabila au dini. Tu katika zama inayohitaji uendeshaji wa nchi unaoshirikisha kila raia hata aliye nje ya serikali na nje ya nchi muradi ni raia mwenzetu.

 

Tunasema tena kwamba dunia ingali kubwa kama zamani lakini leo kumeongezeka kitu kwayo; dunia i kama kijiji kutokana na maingiliano ya watu na mataifa yaliyowezeshwa na kasi ya ajabu ya ukuaji wa sayansi na teknolojia. Leo watu wanasafiri juu angani kuchunguza kuna nini. Wanashinda na kula mwezini kama vile mungu hayuko tena kumbe sivyo. Ni ujanja wa kisomi wa watu kutaka kuweka rekodi za mafanikio ya kitaaluma badala ya kushinda kwa babu kutafuta madaraka na vyeo. Kwenda kwa mganga leo kutafuta cheo? Lakini tutafika lazima tupate mabadiliko ya kujenga nchi zetu.

 

Na katika yote hayo, ukweli na uwazi ni msingi. Hata katika siasa, kama fani, lazima washiriki wawe wakweli; na kuwa mkweli kunaanza kwa mtu na nafsi yake kabla ya kutoka nje. Siasa za kileo si za kale katika vigezo vingi na lazima nasi tuingie na tuogelee hasa kwa sababu hatuwezi kuishi kwa kujitenga.

 

Sote tunakumbuka uandikishaji ulianza Novemba 29 katika Mkoa wa Kusini Pemba na kwamba keshokutwa Mkoa wa Mjini Magharibi unaanza. Mkoa huu, kama ilivyokuwa jiji la Baghdad wakati wa vita vya kusaka silaha za maangamizi nchini Irak, ndio mama wa vita vyote. Takwimu zinabainisha kwamba una asilimia inayozidi 42 ya kura zote za Zanzibar. Kwa hivyo kila chama kinautegemea kwa mavuno.

 

Bado kauli ya Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Mjini, Borafia Mtumwa Silima ya kuzuia wenye wa Pemba kuandikisha kura wilayani kwake haijafutwa, na tunaona mikakati ya kutekeleza amri yake inavyofanywa. Tuna Operesheni Dondola ya Polisi. Makumi ya wenzetu wako na Polisi hivi tunavyozungumza wakisubiri huruma ya dola kurudi makwao na kuhangaikia riziki. Wanasubiri huruma ya dola maana wengi wao wamekutwa na visu au mapanga yakiwemo yaliyoota kutu kwa kutotumika kwa miaka, wamekutwa na jembe au nyundo, wamekutwa na mtaimbo au mkuki na shoka.

 

Wamekutwa na zana hizi za mkulima na mkwezi. Kosa la jinai leo Zanzibar kukuta mtu ana kisu nyumbani kwake. Uhuni mkubwa kiasi cha masheha sasa kulindwa usiku kucha. Wanalindwa kwa sababu wamesababisha chuki dhidi ya raia badala ya kuwasaidia kuendesha maisha yao na kuipunguzia serikali mzigo wa kuondoa umasikini.

 

Tu katika nchi ambayo japo mfumo wa vyama vingi ni ruhusa ya kikatiba, kutokuwa mfuasi wa CCM ni kosa la jinai, unakamatwa, unatiwa katika mtihani, anachukuliwa mkeo kama mtekwa nyara mpaka mume upige ripoti kituoni. Siku moja tu mume kuondoka nyumbani shida je wiki anayotiwa korokoroni, nani analisha watoto zake? Serikali inapunguzia raia zake umasikini? Mashudu!!! Inawaongezea. Wengine zamu zetu hazijafika tutakamatwa tu na kufunguliwa kesi za kuteka nyara wanawake kama ilivyokuwa mwaka 2000. Mwandishi ameteka nyara mwanamke? Salam zako Ally A. Saleh wa BBC.

 

Siondoki kabla ya kuigusa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) chini ya uongozi adhimu wa Mwenyekiti Masauni Yussuf Masauni. Khadithi ya takwimu za tume kwa wanaoandikishwa kuingia katika DKWK la Zanzibar. Vituko na hila ambazo wenyewe wanasema kulalamikia ni kukurupuka maana bado kazi ya kuzifanyia kazi haijesha. Tume haijasema nini kinasubiriwa hadi leo kubandika orodha za majina ya walioandikishwa hata yale ya Mkoa wa Kusini Pemba, miezi mitano tangu uandikishaji umalizike.

 

Na kama hata za miezi mitano hazijabandikwa, hizi zilizomaliza mwezi uliopita na zinazoanza keshokutwa zitaja bandikwa lini? Tuelezwe labda inasubiriwa mpaka mwisho wa uandikishaji ndio takwimu za nchi nzima zibandikwe kwa pamoja, pingamizi zitolewe kwa pamoja nchi nzima, na mahakama zishughulishwe kwa pamoja nchi nzima. Kwa hapa ndipo tutapata takwimu sahihi za kuzitegemea kuingizwa kwenye buku. Mhh ni ngumu!!

 

Watu wanalalamikia takwimu kwa sababu haziendi na hali halisi. Hazifungamani wala hazitengamani. Ni maji ya ziwa na bahari, ya tofauti ingawa yote ni maji; ya bahari yatakuwa na chumvi hata iweje kwa sababu ndio asili yake. Wataalamu wa takwimu wanasema penye watu 100 wa kutosha kuwa watu wazima wa umri unaozidi miaka 18, kwa kulingana na hesabu ya ukuaji wa idadi ya watu, basi watu angalau 50 ndio wapite umri huo. Inapokuwa watu 60 na ushei haieleweki.

 

Mfumo wa takwimu ndivyo ulivyo. Zisipoendana hazifichi zitajionyesha, zitajidhihirisha hasa pale tunapoambiwa makisio ya Tume yametokana na takwimu za Sensa ya Watu ya 2002. Hebu tuangalie hapa. Katika kituo cha Skuli ya Cheju, makisio ya watu kuandikishwa ni 971, wameandikishwa 1,163 (asilimia 119); wametoka wapi watu 192 na Cheju si kijiji cha wavuvi kwamba ilipopita Sensa walikuwa dago. Kiuto cha Dungabweni makisio ni watu 1,520 walioandikishwa ni 2,106 (asilimia 139); wametoka wapi watu 586 napo si kijiji cha wavuvi; Skuli ya Jendele makisio ni watu 907 walioandikishwa ni 1,386 (asilimia 153); wametoka wapi 479 na Jendele si kijiji cha wavuvi kama ilivyo Marumbi walikozidi watu 315 kutoka makisio ya 561 (asilimia 156), bali wakulima wa mpunga ambao itakuwa walinakiliwa Sensa ilipopita maana waliamka kwao.

 

 Lakini hata kwenye vijiji vya wavuvi kama Pongwe, Michamvi, Uroa, Ukongoroni, Bwejuu, Paje, Jambiani na kwingineko, baadhi yake takwimu zimepungua isivyo kawaida na kwingine zimezidi pia huku katika baadhi ya sehemu hizo kukiwa na malalamiko mengi ya watu kukataliwa kuandikishwa kwa amri za masheha. Mfano halisi ni Michamvi: makisio ni kuandikishwa watu 750 lakini wameandikishwa 602 (asilimia 80), watu 148 wako dago hawakuandikisha? Kijiji cha Pongwe makisio ni watu 318 walioandikishwa ni 912 (asilimia 287); watu 594 walikuwa dago wakati wa Sensa?

 

Hebu tuchukue namna nyingine: Kituo cha Skuli ya Machui; makisio ni watu 696, walioandikishwa ni 1,060 (152); watu 364 wametoka wapi na hiki ni kijiji cha wakulima? Skuli ya Ubago makisio ni watu 441, walioandikishwa ni 1,402 (asilimia 318); ziada ya watu 961 imetoka wapi? Skuli ya Kiboje makisio ni watu 693 walioandikishwa ni 923 (asilimia 133); hawa 230 wa ziada wametoka wapi? Skuli ya Uzini makisio ni watu 561 walioandikishwa ni 914 (asilimia 163), hawa wametoka wapi? Umbuji makisio ni watu 766 walioandikishwa ni 952 (asilimia 124), wametoka wapi 186? Pagali makisio ni watu 363 walioandikishwa ni 890 (asilimia 245), watu 530 wametoka wapi? Bambi makisio ni watu 1,336 walioandikishwa ni 2,125 (asilimia 159); ziada ya watu 789 imetoka wapi?

 

Vyote hivyo ni vijiji vya wakulima wanaoamkia nyumbani kwenda shambani hivyo Sensa iliwakuta. Sasa uwapi uhalali wa ziada ya watu iliyofikia hata zaidi ya nusu ya makisio? Na hizi tunabaini ni sehemu ambako watu wengi walipandikizwa wakiwemo vijana wa makambi ya CCM na watu wasiokuwa na sifa wakiwemo watoto waliokuwa wakipelekwa vituoni kwa magari. Hayo ni maeneo yenye ufuasi mkubwa wa CCM hivyo kuingiza wageni ni rahisi. Panya ajitawala pasipo paka!

 

Vipo vijiji idadi haikufikiwa kwa sababu wengi wa wenyeji walikataliwa kwa kuaminika ni wafuasi wa upinzani. Mfano Michamvi walikoandikisha asilimia 80 tu. Zipo taarifa kwamba Katibu wa Jimbo wa CUF alipigwa na vyombo vya dola kiasi cha kuumizwa vibaya kwa sababu ya kusimama kidete kulinda haki. Chwaka waliandikisha asilimia 90, Mwera Pongwe asilimia 83, Mwera waliandikisha asilimia 81, Pete waliandikisha asilimia 82 na hususan Bwejuu waliandikisha watu 1,738 kutoka makisio ya watu 2,392 (asilimia 73). Bwejuu, Wilaya ya Kusini, kama ilivyo Ndijani, Wilaya ya Kati walikoandikisha asilimia 88, ni watu kama Naila Majid Jidawi tu wenye ubavu ndio walifanikiwa kuandikisha.

 

Tutizame kidogo kituo cha Kitogani: makisio ni kuandikisha watu 543, wameandikisha 1,073 (asilimia 198). Hapa kuna kambi ya Kikosi cha Zimamoto, pitio kuu la wasiohusika kama zilivyo kambi nyingine za vikosi vya ulinzi.

 

Hii ndio picha inayopatikana kutokana na takwimu zilizotolewa na Tume baada ya uandikishaji wapiga kura Mkoa wa Kusini Unguja. Zinapingwa inakuwa nongwa, wapingaji wanaambiwa hawana cha maana bali kuleta vichekesho tu. “Unaonekana hukuwa na la kulieleza katika barua yako, badala yake umekuwa ukifanya vichekesho tu” ni majibu katika barua ya Mwenyekiti Masauni akimjibu Katibu Mkuu wa CUF, Seif Shariff Hamad, mgombea pekee wa chama hicho kwa nafasi ya urais Zanzibar. anaambiwa amekurupuka angesubiri uchunguzi kwanza. Malalamiko yanatolewa majibu yanachefua (si hapo tu ndio mtindo wa Tume barua zake nyingi za majibu kwa viongozi wa upinzani zina lugha mbaya ajabu kama si wadau wa uchaguzi) je yasipotolewa kutakuwa na uchunguzi wa kweli? Wamesema takwimu za Tume zinaisuta. Tunaiona changamoto kubwa inayo taasisi hii kujisafisha.

Ends.