Waraka Kutoka Unguja

April 21, 2005

By

Jabir Idrissa

Nilisahau kuwatilia waraka wa wiki ilopita. upitieni huu leo ili kesho, niwatilie waraka wa wiki hii inokwisha ambao tayari umechapishwa katika Rai. Naamini itawasaidia mlio mbali na magazeti ya Tanzania kujua yanayotokea kwetu Z'bar. Karibuni.

Jabir Idrissa+


Headline: Hadithi ya Kinuni, ya Maalim ushahidi wa aibu Z'bar

Waraka kutoka unguja

"Heko," wanasema wacheza bao pale mshindani anapogusa mtaji au kutakasha vizuri. Katika uandikishaji unaoendelea Mkoa wa Mjini Magharibi kumekuwa na heko nyingi lakini hizi si za kucheza au kutakasha vizuri, ni za matatizo yaliyozidi kipimo na kuonyesha wenye mamlaka wasivyotaka mabadiliko.


Wanaona muda wa mabadiliko haujafika hivyo wangali na haki ya kucheza shere na kuonyesha vitimbi na manyanyaso kwa raia wema kila waipatapo nafasi. Si lazima wafanye kwa mikono yao na huwa hawafanyi wao, bali hutumia mawakala wao. Basi mtandao wa wenye mamlaka unapita kila mahali. Umejaa tele ndani ya mfumo wa utendaji wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC).


Itakuwa unajiuliza kwamba hivi chama tawala kinaweza kuwa ndicho kinachoshajiisha shere na vitimbi wakati huu? Mbona chao ni chama kilichosaini Muafaka na Chama cha Wananchi (CUF) mwaka 2001 na kukubaliana kuendesha siasa bila fujo bali taratibu na misingi ya siasa za kidemokrasia ndiyo ya kuzingatia? Kwamba yale maafa yaliyotokea baada ya uchaguzi mkuu wa 1995 na 2000 yatoshe kuwa ni fundisho la ubaya wa siasa za chuki na fujo na huwa si jawabu ya migogoro ya kisiasa.


Vyama vimekubaliana ndio, lakini kukubaliana ni jambo moja na kuheshimu na kutekeleza makubaliano yenyewe ni jambo jingine. Hali inavyokwenda ni ushahidi wa kuwa wenye mamlaka hawajakubali kidhati Muafaka japo ndio wa mbele kulaumu wapinzani wao. Katika makubaliano yanayohusisha chama chenye dhamana ya Dola (nchi), ndicho kinachokuwa na wajibu mkubwa zaidi kwa sababu kinashika taasisi za kidola zilizo muhimu katika ufanikishaji masuala mbalimbali ya kinchi: ndicho chama chenye mamlaka ya uongozi wa nchi.


Unapoona viongozi wake wanaratibu mipango ya kupeleka wapiga kura bandia (bandia kwa maana ya kutokuwa na haki ya kuandikishwa humo wanapopelekwa) vituoni ili waandikishwe kuja kupiga kura, magari yao na hata ya Serikali yakitumika, unapata picha gani? Hivi hawa ndo wamekubali kidhati Muafaka, wanauheshimu kuwa ni njia ya kuondokana na migogoro, na wanausimamia ili kuhakikisha unatekelezwa kwa vitendo si maneno matupu? Hali inaonyesha dhahiri hawajakubali na hawauheshimu Muafaka kama tutakavyoendelea kuona mbele.

Wenye mamlaka kwa hakika hawajatulia kwa sababu hawataki nchi iende mbele katika namna ambayo kila mwananchi, bila ya kumbagua yeyote kwa namna yoyote ile, anaguswa na mafanikio yake, bali ile tu kwamba wao tu ndio waguswe na mafanikio hayo ndiyo dhamira yao wanayotaka iendelee hivyo. Maana yake wao, wanajiona, wana haki zaidi ya wengine na ni sahihi basi hao wengine kuwaamulia kila kitu. Hakuna haki, uhuru wala nini kwa wengine bali wao tu peke yao. Zanzibar ni yao tu wao na wawatakao. Haiwezekani.


Haiwezekani kwa sababu nchi ni ya wote waliomo ndani yake hata wageni. Wana haki zao kwa mujibu wa sheria na Katiba. Serikali na vyombo vyake wanapaswa kuzisimamia zipatikane, nao walindwe na mali zao. Na hii ndio kazi na jukumu kuu la Jeshi la Polisi. Ndiyo maana tunasema hata ile Operesheni Dondola ya IGP Omari Mahita, ilitakiwa itekelezwe katika misingi ya kuheshimu jukumu hilo, si kupalilia fujo kwa kusindikiza vijana wa kiharamia na kuachia wapige watu vituoni na majumbani mwao. Na bado wanaokamatwa kwa matukio hayo ni wanaoonekana si wapenzi na makada wa CCM tu. Wafuasi wa CCM safi sana!


Chama kinachojiheshimu hakiwezi kuachia viongozi wake hata iwe wa ngazi gani waratibu mipango ya kuvuruga masuala muhimu ya kutekeleza demokrasia kama hili la uandikishaji. Viongozi wa CCM si wanyama bali binadamu kama tulivyo wengine. Wanafahamika na maana wanaishi mitaani kama wanavyoishi wengine, wana jirani wana ndugu wana jamaa zao. Unapowakuta wanaratibu mipango ya hujuma kwa raia walio vituoni lazima ushangae. Lakini kwa muda mrefu, wananchi hawawashangai tena kwa sababu imekuwa tabia.


Katibu wa moja ya wilaya za Mkoa wa Mjini Magharibi, aliongoza wenzake na kufika kituo cha kujiandikisha wapiga kura cha Kinuni, Jimbo la Mwera, nyuma yao liko kundi kubwa la vijana. Wakawatenga kando wasiingie eneo la kituo ila wachache mno. Wakafanya mawasiliano, na ghafla hali ya kituo ikabadilia. Viongozi wa upinzani waliokuwa waangalizi hapo wakamkabili msimamizi wa kituo. Alisikiliza hofu yao na kupiga stepu mbili tatu hadi walipo akina Katibu na kuwaambia waondoke kituoni na makundi yao.


Katibu akamaka "tuondoke". Haiwezekani, sisi ndo twenye nchi hii si wengine." Na kweli, haikuchukua muda makundi yakaitwa naye yaingie ndani ya kituo. Vijana waliobeba mapanga, nondo na marungu wakiwa wanatoka nje ya jimbo hilo, wakajipenyeza kwenye foleni kama vile wanataka kuandikishwa. Masikini. Ikatoka amri wapige watu katika foleni na wakapiga huku Polisi wenye bunduki wakiangalia.


Watu kumi wakaumizwa kwa silaha zile za kikulima na wangali hospitalini wakiwa na majeraha vichwani na kila mahali. Mmoja ameshonwa nyuzi 40 kichwani. Maharamia wakaondoshwa kituoni kwa kutumia magari ya viongozi. Siku ile nilisema ya Kianga ya kutia moto nyumba za raia kwa sababu za kisiasa. Nyumba ya kwanza ilitiwa moto chini ya amri ya Mbunge, mtunga sheria kiongozi wa watu.


Mnaona? Wahalifu wanalindwa na kuengwaengwa huku raia wema wakidhalilishwa na kutiwa ulemavu na hizi ndio siasa za wenye mamlaka Zanzibar. wanakaa majukwaani wakisifia wanasimamia sheria ifuate mkondo huku wakilihifadhi na kulisha wahalifu wakubwa. Huu si Muafaka bali uhuni ni siasa za kijambazi alizoziita aliyekuwa Makamu wa Rais, Dk. Ali Omar Juma akizungumzia upinzani. Angekuepo angeona si upinzani leo bali chama alicho akikipenda. Mwenyezi Mungu amrehemu aliko.


Tuna wenzetu wenye mamlaka hawa, ni watu wazima na wenye akili timamu ila yote haya wayasimamiayo kutekelezwa, ni dalili za wazi ya kuwa Mambo Ni Magumu (MNM) na kutulia haiwezekani. Lazima kupangwe shere ndiyo watapata utulivu wa muda maana utulivu kamilifu kwao inaonyesha umefika mwisho. Dalili hizi ni za kuanguka mbuyu mshindo huwa mkubwa. Ndivyo walivyoanguka akina Hitler, Cheusescu na wababe wengineo. Tunataka mbuyu uanguke kwa salama kwa sababu hauna pa kushika tena.


Nimekuwa na jambo na Polisi kwa sababu hawatendi haki. Hawazuii uhuni dhidi ya raia isipokuwa kuahidi kufanya uchunguzi tu kila siku. "Tunafanya uchunguzi" ndio mbiu yao huku raia wakiteseka kama vile wako ukimbizini. Aibu kubwa maana imethibitika Dondola si ya kulinda sheria bali wahalifu. Ukiuliza wakuu si tuseme tu kuwa Polisi imeelemewa na ulinzi wanasema "ah hiyo si kweli hatujafikia huko bado tunafanya kazi yetu." Mpaka lini?


Safari hii Dola ikapata aibu ya mwaka. Hesabu zikaangukia pabaya. Kwa sababu wenye mamlaka wanaona kila jambo ni rahisi kulitenda, walipanga mpango wao na kutumia mawakala wao. "Mzuieni mzee asiandikwe na sababu ni moja tu 'hana sifa ya ukaazi.'" Maalim Seif Shariff Hamad anasema leo kwamba alijua mpango huo mapema na wakisubiri siku tu utimizwe. Kwa miaka 17 anaishi Mtoni Kidatu lakini Afisa Uandikishaji kituoni, Suleiman Ame Vuai, anaidhinisha Katibu Mkuu huyu wa CUF asiandikishwe maana hana sifa ya ukaazi. Kwake yeye, sifa ya ukaazi ni mtu kutoondoa mguu kwenye nyumba yake kwa miezi 36, miaka mitatu. Anajisifu amepita kidato cha nne mwaka 1980.


Akili ya darasani si akili ya kichwa. Aliambiwa hakujiambia na ni yeye anayekamatwa uchawi. Kijana huyu atafanywa kafara kwa sababu ya akili zake kutotulia kwa kila aambiwacho. Wasemaji wa Tume ya Uchaguzi wanakiri alitumia ukereketwa wa kisiasa kumnyima haki Maalim kwa sababu sheria haikusema mtu asiondoke kutafuta riziki nje ya eneo analoishi. Mmojawao anasema "na ingekuwa hivyo basi wengi wangekosa sifa hiyo."


Wala hii si fitna kwa sababu kama sheria ndivyo itakavyo, basi hata Rais Amani Abeid Karume alikwenda Ulaya; Sweden, Finland na Norway mwezi uliopita baada ya kufanya safari Uchina na Uarabuni hapo kabla. Mbona hakuulizwa kuhusu safari yake hiyo kama imemkosesha sifa ya ukaazi. Kilichotokea alipofika kituo cha Kiembesamaki kujiandikisha, makarani walitetemeka hata mpiga picha akashindwa kufanya kazi yake. Waziri Kiongozi Shamsi Vuai Nahodha naye alisafiri kwenda nje aliulizwa kuhusu hilo?


Kwa mara ya kwanza nakubaliana na kauli ya wakuu wa Tume kwamba ukereketwa wa kisiasa ulitumika. Ni ukereketwa kweli kwa sababu msimamizi yule wa kituo aliamua kumsainisha Maalim isivyotakiwa katika fomu ya 2D. Muombaji kuandikishwa husaini upande mmoja tu bali yeye alitaka na upande wa pili usainiwe. Matokeo yake, ile sehemu aliyopaswa kueleza yeye na kutia saini, alimjazisha Maalim. Masikini Suleiman Vuai Ame.


Kwa kuwa kada mmoja maarufu mjini kaniambia kuwa Maalim atalazimika kufika Mahakama Kuu, nakubali kuwa ule ni mpango ulioandaliwa mapema na wenye mamlaka ili kumkomoa na kumdhalilisha kama alivyosema mwenyewe tangu pale kituoni. "Nakwambia hapati mpaka atafika Mahakama Kuu sisi hatutaki mchezo bwana hiki ni chama kinachojiamini. Nawe subiri utaona kama itaishia wilaya," ananieleza kada huyu mwenye makeke mengi kama vile chama ni mali yake.


Hawakujua kwamba kumnyima haki Maalim itakuwa pigo kwao kwa sababu dunia itathibitisha uhuni unaofanyiwa raia halali wa Zanzibar wanaokataliwa kuandikishwa na hawapewi fomu ya 2D ya kudai haki yao. Leo kila pembe ya nchi na kila pembe ya dunia kituko kile kinajulikana maana kimetangazwa na vyombo vya habari vya nchini na vya kimataifa. Tukio lile limeamsha ari mpya kwa raia kudai haki zao na lazima Tume isimame kidete kuhakikisha watu wanapata haki zao za kuandikishwa. Nimekuwa nikisema kwamba Tume ina meno na makali ila hayajaamuliwa kutumika.


Wenyewe wanaweza kusema wanayatumia vilivyo. Kuyatumia kunahitajika kuonekana hadharani. Kama tume imefukuza karani uandikishaji, msimamizi wa kituo, imewakurupusha masheha vitimbi, iyaseme haya hadharani ili wananchi wajue ni kweli inachukua hatua kukomesha uzembe na ukorofi katika kazi muhimu. Wanaoweka pembeni sheria na kujiamulia kwa utashi wao ndio wazembe na wakorofi si mtu anayepita karibu na uzio wa Vikokotoni kuelekea kituo cha kujiandikisha.


Mwalimu wa watoto wetu, Tahir Hussein Abdalla (30) analalamika ameshikishwa adabu na Polisi kwa kugusa uzio wa Stendi ya daladala. Anachukuliwa mzobemzobe na askari wasio mafunzo, na Polisi anayewasimamia anaamrisha apigwe. Nimekuwa nikiwaasa Polisi kudhibiti ukorofi na uhalifu wa kweli. Sasa kama wachukuaji wa hatua dhidi ya ukorofi na uvunjaji haki za watu, wamshughulikie askari aliyeamrisha mwalimu huyu kudhalilishwa katika tukio la Aprili 14 kituo cha Vikokotoni, ambalo limeripotiwa kwa kumbukumbu MAD/RB/1520/05 Kituo cha Polisi Mwembemadema.


Hili liwe fundisho kwa sababu kuna matukio mengi ya Polisi kushiriki kudhalilisha raia bila ya sababu. Hata baadhi ya makamanda wamo wanapita na ukereketwa wao wanapiga raia. Hivi inakuaje RPC mzima anapiga raia usiku huku akipayuka "Mnazungumza siasa hapa enh basi huyo Seif wenu hashindi chochote hatumpi." Nasisitiza mna kazi kubwa ya kurudisha imani kwa raia ili washirikiane nanyi kuzuia uhalifu.

Ends.