Waraka Kutoka Unguja
April 28, 2005
By
Jabir Idrissa
Pateni waraka uliochapishwa katika Rai ya Apr28.
Someni
mfahamu maana mengine hayapatikani katika news coverage za
kawaida.
Jabir Idrissa+
Waraka
kutoka unguja
Headline: Mauaji ya ovyo ndo hatima
aliyoikusudia Mzee Karume?
Hatujachoka. Ni
uhakika ya kuwa ujenzi wa nchi na ustawishaji watu wa Unguja na Pemba
ungali mbali. Ni mbali kwa sababu kila jitihada za kuitupa Zanzibar
nyuma inaonekana. Ingawa utawala ungependa hata kupitia safu hii ya
waraka, upigiwe debe kwamba uko dhatini kuinua hali za watu,
hayajaonekana matokeo ya kupigiwa mfano. Bado.
Kulingana
na ahadi zilizowahi kutolewa wakati ule wa kampeni, hali halisi ya
utekelezaji wake, namna hali za watu zilivyo, namna maisha ya watu
yanavyojongomea na kuonyesha wamo katika lindi la umasikini, bado.
Maendeleo fulani yanaonekana wazi, yapo, lakini hakuna kitu kizuri
kwa uongozi kama kuwashinda watu nyoyo zao kupitia kuwaunganisha,
kuwajengea upendo na kuachia utamaduni wao udumu. Iwe yote safi,
nyanja hii ya kudumisha utamaduni wa watu wa kuishi kwa utulivu na
kusaidiana, upo katika mtihani mkubwa.
Hivi
ninavyoandaa, kuna kundi la watu waliokataliwa kuandikishwa kwa
sababu ya siasa za chuki na za ubinafsi zinazopaliliwa na utawala.
Kuna malalamiko ya wananchi wa kindakindaki wa Unguja na Pemba
kunyimwa haki ya kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura
(DKWK) kisiasa tu huku wakishuhudia wageni fresh kutoka
kwingineko wakipitishwa mezani na kuandikwa.
Inashangaza
kuona siasa petu zinageuzwa njia ya mkato ya wakubwa kutimiza dhamira
zao za kutenga watu, za kunyanyasa watu, za kugawa watu, za
kuwagonganisha kwa nasaba za watokako na kadhalika. Wakubwa wamegeuza
mtaji watu wasioshabikia chama wanachokifanya wao ni mali yao. Basi
huwajengea chuki na siku hizi tunaona waziwazi wakitumia vyombo vya
dola kutetea madaraka yasiwatoke. Si vizuri hata
kidogo.
Nikidhani na kwa hakika ndivyo
ninavyoamini, ukimtaka mtu akufuate upande wako, apende ukipendacho
wewe, basi utumie lugha nzuri ya kumpendezesha na kumtia imani ya
kuwa unamhitaji kikwelikweli. Nyendo zinazoelekeza watu katika
mirengo zinapaswa kuwa nyofu na siyo zilizopindapinda zikionyesha
zimegubikwa na mikikimikiki inayoambatana na vitisho vinavyofanywa na
mawakala wa ulinzi na usalama. Popote penye vitisho nia huwa ni
kujengea watu nidhamu ya woga, na penye nidhamu hiyo, hapeshi fitina
na ndani ya fitina ni jamii kuvutana siku hadi siku. Haifai.
Leo
wakati tuna zaidi ya mwaka tangu kutokea milipuko ya mabomu nilopata
kuipachika jina la milipuko ya kishetani na umma wa Zanzibar na
Tanzania kwa jumla, pamoja na ulimwengu mzima, ukisubiri ripoti ya
waliohusika nayo, milipuko mingine imeanza. Ati bomu litegwe na
wapinzani na kila siku likose shabaha. Bomu linavunja sentimita
chache za ukuta usiku wa saa 2 ambao kwa muda sasa hukosi wafuasi
ndani ya maskani za Chama cha Mapinduzi (CCM). Ajabu ya
mwaka.
Yale yale ya kwamba lisiloweza kutokea
popote duniani, huweza kujiri kwa petu Zanzibar. Milipuko inayokwepa
watu kwa maksudi imeanza upya. Inajulikana wazi nani anaisuka na
kuifanikisha isipokuwa kwa sababu Dola inataka inayoyataka
kushuhudia, hakuna wa kuidhibiti. Hakuna maana dola ndivyo itakavyo,
itokee milipuko halafu wakamatwe wasioshabikia CCM. Balaa, balaa na
fadhaa tupu.
Kwanini inakuwa nongwa watu kupenda
upinzani? Sioni tatizo kwa sababu napenda demokrasia na katika
demokrasia ya kweli (si ya majukwaani na ofisini tunapokaribisha
mabalozi) lazima chama tawala kipate chama makini cha kukipinga.
Kisipopingwa kitakuwa kinalala tu huku kikishindwa kutekeleza ahadi
na majukumu yake ya kuongoza watu. Watu wanataka kuongozwa siyo
kutawaliwa. Si tulifukuza Usultani ili tusitawaliwe? Mbona kuna
nyendo za kutawaliwa raia.
Raia anapokuwa hana
raha na maisha kwa sababu ya hofu ya kuchukuliwa na polisi na hawa
vijana wa kisasa wa Janjaweed (askari wa vikosi vya SMZ wasio
mafunzo ya kweli) au raia anapojisukuma kurudi nyumbani ikiingia tu
magharibi kwa sababu ya kuhofia kukutana nao vijana hawa kwenye
maeneo yao ya maskani, si dalili ya ushuwari bali hofu kuu iliyotanda
akilini mwake. Raia wanashambuliwa kama watoto wadogo na wanaporipoti
vituoni mwa Polisi wanageuziwa vibao; wanabambikizwa mashitaka. Si
ishara njema bali uasi wa Dola kwa wananchi wake. Na lini wananchi
walioasiwa na vyombo vya kuwalinda watatoa ushirikiano?
Inakuaje
kila uchao ni watu wa mrengo wa upinzani tu ndio wachafu wa kufuata
sheria. Hii tabia ya kuwa kila siku kutokee matukio ya fujo kwenye
nyumba zao hata kuchomwa moto na kuteketezewa mali zao huku
wakishuhudia wahujumu wao wakichekelea kwenye maskani ndio nini? Ndio
kutesa kwa zamu huku kulikopata kusemwa na waheshimiwa wajumbe wa
Baraza la Wawakilishi? Nilipata kuuliza katika safu hii; raia
watatesa lini wao na hawana bunduki? Sikupata jibu ila nafahamu fika
bunduki haishindi umma, watatesa nao.
Kunatokea
matukio yanaacha maswali mengi kuliko nguvu ya kuyajibu. Kwanza
nakumbukia kauli ya Serikali kuhusu mauaji ya Juma Omar Juma ya kule
Ngombeni Mbuyuni, Mkoani Pemba. Kujigongagonga kutupu kusiko na njia
wala dalili za utawala kujifunza kwamba yanayofanyika si halali na
hayawezi kujenga jamii nyofu. Juma inaelezwa kafa katika mazingira ya
kutatanisha maana alikuwa aingie shule mchana si asubuhi alipokutwa
na risasi ya moto; inaelezwa kuwa baada ya kufa alichukuliwa
harakaharaka na watu wa chama cha siasa na jeneza alimobebwa
likazongwa vitambaa vya bendera ya chama.
Hivi
nani asiyejua kati ya viongozi wa juu wa nchi ya kuwa Juma
alisokomezewa mbalini kwenye mtaro wa maji machafu? Kwanini alitupiwa
huko kama si kwamba asionekane abadani kwa sababu angebururwa na maji
ya mvua yaliyokuwa yakivuka kama treni iliyo mwendoni. Kwa hivyo
utawala ulitarajia Juma angebaki hapo kwenye mtaro kwa maisha yake
yote ya akhera? Kuchukuliwa na wenye imani ili kumsitiri ilikuwa
kosa? Ninaamini ingetaka, Serikali ilikuwa na uwezo wa kulinda mpaka
awe amechunguzwa mwili wake nini sababu ya kufa kwake. Haikutaka,
haikutaraji kwa sababu ingeumbuka!
Lakini bado
inaumbuka hata sasa kutokana na kauli zake zinazogongana. Si wakati
ule ilipata kuelezwa kuwa alifariki kwenye msongamano wa watu
waliokuwa wakipambana kuandikishwa? Na kwani kuna mabadiliko ya
serikali? Si ni ileile iliyopata kutuambia raia kwamba mtu wa Shumba
mjini alipatwa na risasi ilipotoka juu baada ya askari yule mjuzi
kuilenga angani? Tungali tunakumbuka na ya leo ni muendelezo tu wa
mbinu chafu zinazotendwa hadharani.
Juma kauawa
kwa risasi ya askari wa Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM)
waliopelekwa kituoni kuwapa wenzao ulinzi ili waandikishwe kwa
lazima. Kwanini uchunguzi usingeanzia hapo pa kuletwa sababu ya KMKM
kuwepo pale? Si sheria askari kuwepo vituoni baki tu wale askari
polisi wawili watatu wa kuweka ulinzi tena wakiwa wameficha silaha.
Raia wa kikwetu ni watulivu hawasukumwi ja punda; kwa bakora. Ni
maridhia kwelikweli Wazanzibari ila unapowanyenyekea.
Muuaji
wa Juma atakufa tu naye na tunajua anaangamia taratibu kwa sababu
roho ya binadamu imeumbwa na muumbaji kaapa hatamsamehe anayeiondoa
bila ya haki. Eti Serikali inauliza nani kamuua Juma? Anayemjua
atuambie tutamlinda? Yetu serikali imemlinda nani siku zote? Twasema
muuaji wake tunaye khabari angalipo hai anadunda, afichwe popote,
aliyemuumba hata naye, ajua aliko na kila akifanyacho. Mauaji kama
hayo hukumu yake anaitimiza yeye Subhana. Wala hafundishwi.
Leo
kuna mauaji mengine ya kihuni yametokea: Chande Rashid Saleh,
aliyekuwa wakala wa CCM katika kituo cha uandikishaji cha Kinuni.
Kakutwa mfu akiwa amezikwa nusu yake, huku nusu ikiwa juu. Mazingira
ya tukio yanaacha maswali mengi kuliko majibu yake. Hebu tuelezwe
sababu ya Chande kuondolewa kituoni. Ni dhahiri itakuwa akikataa
kupinga kila mtu hata anayemfahamu ni mkaazi halali wa eneo lake.
Lakini uadilifu wake huo pengine ndio chanzo cha yaliyomfika.
Alitafuta rehema za muumba kuliko za siasa, akaachia haki isimame.
Mhh kosa kubwa kwa sababu bila ya rafu, bao la
kisigino.
Ufuatiliaji umebaini kuna vitisho
vimecheza ndani ya familia ya marehemu. Wamelazimishwa kuamini
wasiyoyaamini na kuyasema yanayowatia uchungu kwa kuona sivyo ukweli
ulivyo. Serikali iliyo makini kutenda haki haipati shida katika
matukio kama hayo kama inavyojitia leo. Unakamata wakala wa upinzani
wakati waliohusika wanajulikana. Ni nini kama si kudanganya watu.
Lakini watadanganywa wote mpaka lini kwa wakati mmoja?
Kama
kuna matukio ya hujuma dhidi ya raia yanatokea huku Dola ikishuhudia
bila ya kuyasimamisha, umma uamini vipi kwamba uko katika utawala wa
mabavu ambao kwa kawaida huwa hautaki haki isimame, sheria ifuatwe
kama msumeno. Kinachoendelea ni hali ya Serikali kujikosesha uhalali
katika kutawala. Raia ni muhimu alindwe ili atumikie nchi yake kwa
upendo. Asipolindwa na akiamini hasa ya kuwa halindwi kwa sababu ya
utashi wa kisiasa, afanyeje?
Inafaa ielezwe wazi
kwamba kuna mradi unatendeka ndani ya Jeshi la Polisi:
kunabuniwa hujuma isiyodhuru mamlaka ya nchi, kwa makusudi tu ya
kukamata watu wa mrengo wa kushoto, halafu unakuta ndugu zao
wahangaike kuwatoa na hawatoki ila kwa Kitu Kidogo (KK). Ni mpango
maalum wa kuwatumia raia kushibisha matumbo yao: ni dhulma ya nguvu
hiyo. Malipo ya dhulma mnayajua au mwayasikia tu kwa sababu mko mbali
na aliyewaumba? Tabaan muache dhulma wakubwa ili hata hija zenu
ziingizwe kwenye amali zenu.
Hivi wakubwa
hawaoni kwamba mafuriko yalokumba ndugu zetu ni mtihani kwao
wajifungue waone wapo walipo na wapi wanatakiwa kwenda. Si huambiwa
tuna watabiri wa Hali ya Hewa, walikuwa wapi wasitupe indhari ya kuwa
kuna mvua nyingi zitanyesha na kusababisha gharika? Haiwezekani kujua
kila kitu, mengi yanahitaji kubakishiwa mwenyewe muumba. Mvua imekuja
ya kutosha na imeleta madhara hatujaona tu nguvu zake Allah?
Tufumbuke macho kwa kutangulia kuacha maovu.
Mafuriko
yanapita hata mule mulimotengenezwa kwa mamilioni ya fedha. Mitaro
mikubwa mikubwa imepitisha maji yasiyo kiasi chake na makalavati
kuvunjwavunjwa. Uko wapi mtaro wa Kwahani Uwanja wa Farasi ulojengwa
kwa fedha nyingi? Uko wapi na ule wa Jangombe uliojengwa kwa
mbwembwe? Uko wapi mtaro wa Kariakoo wa kupeleka maji kwao yasidhuru
jamii? Hakuna kishindacho muumba. Mafunzo haya tupate.
Nifunge
basi kwa kutanabahisha ya kuwa umma na jamii ya Unguja na Pemba iko
katika hatari ya kudidimia zaidi na zaidi kwa mtindo unaoendelea.
Vitendo vya kuangamizana kwa sababu ya siasa lazima vipigwe kumbo.
Tungependa kuona watu wanasabihiana kikawaida badala ya ile staili ya
kumjibu mtu kwa mgongoni. Serikali ina wajibu wa kutandika misingi ya
maelewano ya kweli si ya juujuu.
Utawala
unapaswa kuheshimu haki za watu. Kwa hakika haupaswi kuingilia
walioteuliwa kutenda haki ili wasiitende. Yaliyotendwa na masheha ni
aibu katika nchi kama Zanzibar inayojulikana kwingi kwa huruma,
ukarimu na ustaarabu miongoni mwa watu wake. Haya kama viongozi hawa
walikuwa nusu mitume katika siku 21 si zimekwisha. Watabaki kwenye
vituo vya kuandikisha wampinge nani? Warudi basi kwa jamii waliyoitia
katika misukosuko isiyo lazima. Kila anayeingia kituoni Sheha
hamfahamu au anasema sikutambui utatambua wangapi ngurumbili
wewe?
Masikini nao kutokana na kutotambua kwao
haki, wakakubali kutumiwa kama ngazi ya wakubwa kupandia kwenda
watakako; nchi ya kusadikika Zanzibar. Walisema mapema nchi haitolewi
kwa karatasi, itolewe kwanini basi na malendo ya mapinduzi yametupwa?
Tulio nao ndio Muungano aliouasisi Mzee Abeid Amani Karume? Si kweli.
Mzee mwenziwe, Ali Sultan bin Issa alitukumbusha juzi pale Bwawani ya
kuwa mzee akiipenda Zanzibar, akivutana chini kwa chini na Mwalimu
Julius Nyerere ili kuijengea hatima. Tuliyonayo ndio hatima
aliyoikusudia hii ya kuhujumiana sisi kwa sisi? Heko miaka 41 ya
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na udumu!!!
Ends.