Waraka Kutoka Unguja
May 5, 2005
By
Jabir Idrissa
Kwa wale walio mbali na magazeti ya
Tanzania, pateni uhondo wa waraka uliochapishwa katika gazeti la Rai
la Mei 5.
Headline: Yakhe Zanzibar hatuachi mazonge
siye?
Wengi wetu binadamu tumejengwa katika kuamini ya kuwa
mmoja wetu anapoanzisha jitihada za kuelekeza njia sahihi kwa kukosoa
juu ya maovu yanayotendwa, anatumaini wale wanaokosea wamsikie na
waache maovu hayo. Tunaamini hivyo kwa kuwa tunaamini pia kuwa siku
zote mwisho wa maovu ni chuki na kulipizana visasi.
Pale
inapotokea wanaotenda au kuchochea maovu wakawa hawasikii na ikawa
hawasikii kwa makusudi tu siyo kwa sababu hawasikii kilio cha hayo
maovu wanayoyasaidia, basi mkosoaji anavunjika moyo. Anaacha kukosoa.
Kwa hivyo kama ni muandishi wa habari kama mimi niache kalamu;
ninyamaze kimya. Inakuwa nifunge mdomo wangu.
Kwa karne ya
leo, kama ilivyokuwa za huko nyuma walipoishi waliotutangulia, hili
haliwezekani. "Mhh hiyo ni ngumu," wanasema wenyewe. Na
kweli, kwangu ni ngumu kufunga mdomo kwa sababu kufanya hivyo si
ishara ya kukomaa kiakili bali kudidimia. Jamii inafikia enzi, lazima
kujitolea kwa sababu hata nasi tungependa kuishi bila ya kuhofia
maisha yetu. Ikiwa hali inaonyesha ni ya kutiwa hofu kila siku, ni
vigumu kusalimu amri. Basi waraka mtaendelea nao mpaka pale
aliyetuumba, Allah (SW) atakaposema basi!
Kwanini
tuendelee? Jibu ni rahisi: bado tunaowaelekeza njia hawajaamua
kutulia, wangali wakiamini ni wao tu na si wengine. Wanaamini bado
zama hii ni yao tu ya kutesa, na wala haitakuja ya wao kuwa nje ya
utawala. Wao hawafanani asilani na akina Adolph Hitler, Haile
Sellasie, Shah na Mboutu Sese Seko. Wao ni wao tu hawana mfano. Basi
wataendelea kutesa tu na wala Mwenyezi Mungu hawapitii wao.
Wamejiumba hawa si waumbwa. Tunaomuamini na kupata ushahidi kuwa yupo
karibu nasi kwa kila tutendalo, tuseme tu ukweli utadhihiri wakati
ukifika.
Ni kwa sababu tu maovu yanaendelea kusawiri katika
Zanzibar yetu tuipendayo, na kwa vile walio madarakani hawajaamua
kutia akili kubadilika wakayasimamisha, ndio inabidi tuendelee
kueleza haya. Si mmeona nilitumia nafasi kubwa wiki iliyopita
kuelezea suala hili lakini wakati mkiendelea kusoma, ndo kwanza
yakaibuka mengine, si mapya. Tukisema zamani "chungu ndo kwanza
kiko jikoni."
Kupita kwenye baraza za watu walio katika
utekelezaji wa uhuru wao, wa haki zao, wa utamaduni wao, na kupigwa
bila ya kuchagua. Rungu, tako la bunduki, waya, teke na matusi ya
nguoni pamoja na kauli za kashfa za kisiasa bado inaonekana ndio
silaha ya kukifanya Chama Dola kiungwe mkono uchaguzi ujao. Ni kweli
naamini sasa binadamu anapoporomoka kiakili hajifichi; hufanya mambo
hadharani maana hana soni tena. Hana wa kumuogopa angeogopa.
Kwa
hivyo wanaamini lazima watumie Polisi. Wapite mitaani na kwenye
baraza za watu waendeshe vipigo na vitisho halafu si watatengeneza tu
taarifa za kuzitoa kwenye vyombo vya habari wanavyovimiliki? Ni kitu
kidogo tu kupiga na kudhalilisha raia kwa sababu haiwi chochote maana
hakuna wa kuogopwa. Mambo safi na amani na utulivu vinaendelea
kawaida. Hivi ndivyo inavyotakiwa maana tupo katika nchi ya
kusadikika; Zanzibar, panapotokea yasivyoweza kutokea kwingineko
duniani. Hapa si ndio kwenye jumba la ajabu; Beit el Ajaib? Basi na
mambo yake yawe ya ajabu ajabu. Haya.
Taasisi hii kwa hapa
kwetu muflis. Imekwisha kwa vigezo vyote. Dondola imejihidhirisha si
ya kulinda raia bali Dola chini ya CCM, yalopangwa kutokea wakati wa
uandikishaji yametimia, nini kimebaki? Hakuna lakini bado, malengo
hayajafikiwa kwa sababu bado uchaguzi, tulipo ni kwenye maandalizi
tu. Hizi ni rasharasha bwana, mvua bado. Raia wema inabidi tuendelee
kustahmili maana safari ni ndefu mpaka siku ya kusema na kisanduku.
Lakini kwa sababu sisi hatukujiumba tumeumbwa, tutavuka salama
usalimini ili tuje tuseme. Amin.
Hapo kati nimesema
yaliyopangwa wakati wa uandikishaji yametimia. Ni kweli, si Wapemba,
CUF na wa vyama vingine hawakuandikishwa. Basi ni kweli yale walo
wakiyasema akina Borafia Mtumwa Silima, na yale aloyasema Katibu wa
Idara ya Itikadi na Uenezi ya CCM, Vuai Ali Vuai alipokuwa Pemba
baada tu ya kuanza uandikishaji Mkoa wa Kusini na mambo kuanza kuwa
magumu (kumbukeni MNM). Alilalamikia alodai yanayofanywa na Tume
ikishirikiana na CUF mpaka akasema: "uandikishaji ndo tumeanza
tu wajue watakuja Unguja." Tumeona wala si uongo. Mamia kwa
mamia wamerudi wao tu kutoka vituoni, hawana shahada wala fomu za 2D,
wao peke yao; wavyokwenda ndo wavyorudi. Patupu.
Haya kama ndo
hivyo nini sasa? Ndo Chama dume kimeshinda? Kama kimeshinda uchaguzi
wa nini tena? Si kitangaziwe tu kimeshinda uchaguzi wa 2005, na
wagombea wake wote wa kiti cha Ikulu na majimbo 50 ya Unguja na
Pemba. Kumbe? Ikiwa chama kimoja tu katika uendeshaji Serikali si
basi, ndo kukosa kula? Si tutakuwa tumerudi kwenye mfumo wa chama
kimoja kwa mlango wa nyuma. Bado ipo kazi kubwa ya kutendwa hata CCM
itangazwe bingwa. Mechi imeanza tu magoli bado na hakujawa cha
kutambia.
Angalau tulipo Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC)
imekiri vituo vya uandikishaji vilitekwa na masheha. Lakini
hawajamaliza kusema ukweli, vilitekwa hata na makarani wake wa
uandikishaji; walikubali kunyongwa shingo namna ile kwa sababu
hawakuwa makarani kweli, walikuwa mawakala wengine wa CCM. Wangapi
mliwaondoa vituoni kwa kutotimiza uadilifu mloutaka iwe ndio ngao ya
utendaji wao? Nilipata kusema "semeni mkiwatoa" hamkusema
tukiamini hakuna muandikishaji aliyeondolewa zaidi ya yule mmoja
kituo cha Kwamtipura ambako hata Sheha mlimuondoa lakini akarudishwa
na Mkuu wa Mkoa kwa jeuri ya nguvu. "Atokee atakayekuambia
uondoke niletee jina." Afanyeje na kituo kile ni chini yake
mwakilishi wa rais si Tume?
Haya na yule ofisa wa jimbo la
Mikunguni aliyekamatwa na nailoni za kubandikia vitambulisho
mlitutangazia kuwa ameshikwa? Hamkufanya hivyo wakati mna watu wawili
wa idara ya uhusiano. Ninawafahamu walivyo wachapa kazi hodari hawa
lakini naweza kuamini hawakupewa mamlaka ya kutangaza hata tukio hili
ambalo limepelekwa mahakamani tayari. Ndo nini. Ndio utendaji gani
kuajiri maofisa wa habari halafu habari hazitoki. Ni aibu kuwafanya
hawa wapeleka makabrasha tu kwenye vikao vya wakubwa. Acheni kugeuza
waandishi wazuri ni matarishi, wapeni nguvu na uhuru wafanye
kilichowaingiza kazini ZEC. Nanyi waandishi tumikieni fani yenu si
utarishi, mtajaulizwa.
Zile siku 21 zimekwisha na masheha
mmerudi mitaani. Mzungumze na nani wakati wakaazi wenu mkiwaambia
vituoni hamuwatambui? Je bado mnalindwa na kuchukuliwa na kurudishwa
kwa gari majumbani? Tuliwaeleza mkadhani tunawafitinisha na wakubwa
zenu. Sivyo, tulikuwa tukiwaaidhi mtambue mamlaka yenu na mipaka
yenu. Mchunge uadilifu dhidi ya kutumikia watawala, au hamkujua
uadilifu ni jambo la kheri. Mkaacha kukubalia mnaowajua mkaingiza
msiowajua wakaandikishwa kiulaini.
Mtu mmoja aliniambia
alipokwenda kituoni Jang'ombe akapingwa asiandikishwe kwa sababu eti
alitukana Sheha mtaani. "Niliumia kuona naondoshwa kwa mtutu
huku akipitishwa mtu aliyetoka Mtima hata hajui alikuwa jimbo gani?"
alijisemea. Hadithi kama hizi ni nyingi mno. Wapi umesikia mtu
anamkataa mtu aliyemfia baba yake mzazi mapajani kwake? Ulisikia wapi
itafika siku baba anamkatalia mwanawe, mkewe, mkwewe na jirani yake
kwa sababu tu anaona si mwenzetu katika CCM? Na ikathibitika kuwa
masheha wote ni CCM. Ndio ukweli, Masheha mliukwepa uadilifu kwa
sababu ya mshahara kiduchu na zile elfu arubaini mlizolia kiapo
mtatekeleza matakwa ya Serikali hata kama kufanya hivyo ni uhuni.
Nawaachia wenyewe. Wanasema mtajiju, maana kusudi haiambiwi
pole.
Uhuni wa masheha na undembendembe wa Tume kwa hakika
umesababisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK) la Zanzibar
liingie waliomo na wasiokuwemo. Nilipata kusema uchaguzi huru na wa
haki utapatikanaje kwa daftari la waliomo na wasiokuwemo. Bado
nauliza itakuaje, tutafanyaje katika hali kama hii. Sawa Tume mkisema
mtachunguza madai ya watu kutoandikwa na kutopewa fomu za kulalamika,
lakini matokeo ya uchunguzi yatatolewa hadharani au ndo yamekwisha?
Na kuwa yamekwisha haiwezekani kwa sababu mmeapa uadilifu mbele na
mtafanya kazi kwa mujibu wa Katiba na Sheria ya Uchaguzi. Tunataka
Tume mjirudi mtimize matumaini ya umma si hivyo mkubali kubeba
lawama.
Ni vitendo vinavyomjenga au kumbomoa mtu au taasisi,
si maneno matamu kwenye majibu ya barua. Hapana, hakukuwa na maneno
matamu katika barua zilizotumwa vyama vya upinzani. Nyingi
nilizoziona kutokana na kazi yangu, zilikuwa na lugha ya kukirihisha;
mbaya ajabu kama vile kila mtu katika Tume aliamua kuacha ustaarabu
wa uungwana tuliouzoea. Lugha chafu tupu isiyoleta matumaini kwamba
tumekusudia kweli kujenga jamii yetu.
Matokeo yake watu kwa
maelfu wameingia kwa hila ndani ya daftari. Sasa ndo daftari gani
hili mlotakiwa kulisimamia huku wenyewe mkikiri mamilioni ya fedha
zikiwemo za wahisani yametumika kuligharimia? Siamini kama Wahisani
walitoa fedha zao ili kutuletea daftari bomu Zanzibar na wabaki radhi
kwa yaliyolisibu. Siamini na yahitaji mtafakari kwa makini na kuondoa
uozo huo ili walio wa kweli wabaki na wasio watoke.
Leo
vituoni mwa uandikishaji Daftari la Muungano ni aibu tupu. Kutwa
nzima makarani wanasinzia ovyo maana hawana kazi ya kufanya.
Wamuandike nani? Hawapo eti maana watu waliopaswa kuingia humo
wameingizwa kwa hila za Dola katika Daftari la Zanzibar. kilichobaki
ni kupoteza muda wa watu na fedha za umma. Na hayo ndiyo matokeo ya
mipango mibovu ya waliopewa mamlaka. Ni matokeo ya uvimbishaji vichwa
wakubwa usio na kifani. Ni aibu jamani aibu. Hatuachi yakhe Zanzibar
mazonge?
Ends.