|
Wanaukumbi Aslaam Aleykum;
Huu ni waraka mpya baada ya
kifungo cha siku 11. mtaona kama nimepunguza ukali wa
kalamu.
Faida kubwa sana kwa mlio mbali na Tanzania ambako
gazeti la Rai halijafika mkausoma.
Haya nufaikeni.
Jabir
Idrissa+
Heko ni huru! Muafaka CCM/CUF
ulishavunjwa tayari
Naam kifungo
kimeondolewa. Kile kifungo kilichokuwa kimewekwa shingoni kwangu
kimeondolewa. Ilikuwa kifungo kikali kile kwa sababu hakina muda
kitakaokuwa kimekwisha: inaitwa indefinite ban. Kwa bahati
mbaya inaonyesha kifungo chenyewe kilitokana na kazi ya watu
wachache ndani ya Serikali kwa hivyo wakubwa walipoulizwa na
wakubwa wenzao wakaishia kusema hawafahamu na wanahitaji
kufuatilia ili kuchukua hatua muafaka. Kama ni kweli
inashangaza.
Kifungo hakikuzingatia Sheria
namba 5 ya Magazeti na Machapisho ya mwaka 1988, ingawa ni kweli
ina vifungu vinavyotaka mwandishi wa habari apewe kibali na Idara
ya Habari Maelezo. Sheria inataka mwandishi ambaye atakuwa
hakusikia wito wa kuchukua kitambulisho, aitwe na kufahamishwa ya
kuwa anapaswa kuchukua kitambulisho. Sijapuuza wito wa kuchukua
kitambulisho hiki kiasi cha kutajwa mimi ni mhalifu wa sheria ya
magazeti.
Wala Idara hii haina uthibitisho
kuwa imewahi kuniita na kunieleza, kama alivyosikika mkuu wake
akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la
Uingereza (BBC). Yote ya muhimu kabla ya kuadhibiwa hayakufanyika
na ndiyo maana ninasisitiza kwamba kifungo kile hakikuwa na
uhalali wowote kisheria.
Nina thubutu ya
kusema haya kwa sababu ninaamini katika utawala bora. Utawala wa
sheria wa kwelikweli unaohimiza ufuataji Katiba, Sheria na
Taratibu zilizowekwa katika kuendesha mambo ya umma, la kama ni
kuonyeshana ubabe kwamba fulani ana mamlaka, ni sawa kusema kwamba
waliosuka mpango huu wamefanikiwa lakini bado njia ni
chafu.
Nimekuwa nikieleza katika safu hii
umuhimu wa kila mtu kuwajibika kuisaidia nchi kwenda mbele. Sote
tuwe na hima hiyo, isipokuwa tukubaliane katika njia za kufikia
huko. Tofauti ni chachu ya maendeleo popote pale. Lililo muhimu
zaidi katika kufanya kazi ya kuhudumia umma, ni kwa mtu, wakiwemo
maofisa wa serikali, kuhakikisha anachokifanya au anachokiamua
hakitaitia nchi aibu mbele za macho ya watu. Aliyekusudia
kunidhalilisha kwa kunitangaza mhalifu wa sheria, atambue
nimedhalilika kidogo kuliko ilivyodhalilishwa
serikali.
Zanzibar ni nchi ya watu na
serikali ni ya watu si ya mtu au kikundi cha watu. Ofisa wake
anapofanya uamuzi na ukahojiwa na umma pamoja na wawakilishi wa
kibalozi kwa kuona hauna mantiki ya kisheria au hata kwa
kuzingatia hali halisi ya wakati, inakuwa ni aibu. Aibu kama hii
haibaki tu kwa ofisa mhusika peke yake, inageuka aibu ya
nchi.
Nchi inaonekana ina watu wasioheshimu
mipaka ya kazi yao. Wazanzibari wangependa ofisi zao zipewe watu
wenye ujuzi na utulivu katika kutoa huduma. Watu wanaoangalia
athari za maamuzi yao kabla ya kuyatoa. Katika uanasheria, kuna
haja ya Hakimu anapotaka kutoa hukumu, kupaswa kujiuliza mara
kadhaa umma utaichukuliaje hukumu atakayoitoa? Basi kila ofisa wa
ofisi ya umma (ya serikali) naye anawajibika kufikiri kwanza kabla
ya kuamua. Ndio hapa tunasikia kuna mahitaji ya viongozi bora siyo
bora viongozi. Katika utendaji kazi, tusiwe kama pweza kuvutia
maslahi upande wetu. Tafakuri jambo jema.
Mkono
wangu uko huru kama zilivyo fikra zangu. Huru huru kabisa hakuna
kifungo tena. Lazima nisifu ujasiri uliotumika kwa Idara na
Serikali baada ya tukio lile. Kwa vile halikupendeza na kujenga
taswira nzuri kwa nchi, wamechukua uamuzi wa busara ule niliouomba
katika waraka uliopita na kukubali tu maombi yangu ya
kitambulisho. Nilitimiza wajibu wangu nimepata haki yangu. Sina
ubaya na Idara, Mkuu wake wala Serikali ila mambo kama haya
yanatupa mafunzo mengi na kila mtu ajifunze. Zanzibar haiwezi
kuishi peke ikajificha.
Kwa kuwa safu hii
haikupata kusimama kutokana na umuhimu wake kwenu wasomaji na kwa
umma kwa jumla, itazidi kuchanua kwa sababu yanayofaa kuandikiwa
waraka yangalipo. Tena mengine mapya ja shuka. Sifanyi utani
ninaposema kungekuwa hakuna madhambi katika jamii yetu
ningeshindwa kuijaza safu. Yapo madhambi kwa sababu haijaonekana
dhamira ya kuyazuia kutokea. Waraka utaendelea Mungu
akipenda.
Tunazidi kwenda katika tarehe za
uchaguzi. Nikasikia kumetokea vurugu Bagamoyo. Kabla ya wakuu wa
Polisi kutaja wahusika, nikasikia kauli za wanasiasa. Chama cha
Mapinduzi (CCM) kikalaumu Chama cha Wananchi (CUF), wapinzani wao
wakuu kwa namna inavyoonekana sasa hata Tanzania Bara. Mtangazaji
mkuu wa sera na maamuzi ya CCM akatoa sauti CUF ndio waliofanya
vurugu. Kauli ya mwisho ikawa lazima waombe radhi chama, wamuombe
radhi mgombea si hivyo Chama kitafikiria upya uhusiano wake na CUF
juu ya Muafaka.
CUF hawakuomba radhi na
viongozi wake wakasema wazi vurugu zilizochochewa na wafuasi wa
CCM waliokuwa na nia ya kusambaratisha mkutano wa CUF. Inaonyesha
Bagamoyo kungali na ushindani mzito wa udhibiti wa siasa katika
mji unaofanana kimazingira na Zanzibar. Mwenendo wa demokrasia
nchini petu, unaonyesha udhibiti wa siasa unaruhusika kwa CCM tu
si vyama vingine. Hiki ndio chama dola, kinacholea demokrasia
inayoendelea kuitwa changa haijapea. Basi kinavyotaka ndio
iwe.
Twaha amekuwa akionekana mwiba kwa siasa
za CCM Bagamoyo. Wapo wanauliza hivi Twaha kapata lini
uchechemeaji mguu. Eti wanasema zote ni siasa tu. Amekuwa
akichukuliwa kama ni kiongozi madhubuti wa chama cha upinzani kwa
hivyo dawa yake ni kumsukumiza. Na kweli wiki ya pili hii sasa
amekuwa ndani na yanaibuka maswali yuko katika gereza gani
Bagamoyo?
Ametiwa kitanzini baada ya
wanasiasa wa CCM kusema vurugu zimefanywa na CUF. Bagamoyo na
Zanzibar si mbali lakini tunapozungumzia Muafaka wa kisiasa
uliosainiwa na vyama vya CCM na CUF, kila mtu anajiuliza vurugu za
kihuni zilizoandaliwa Bagamoyo zitakuwa na uhusiano gani na
Muafaka uliohusu matatizo ya kisiasa yanayoihusu Zanzibar? Na
mpaka sasa wapo wanaojiuliza sababu ya Muafaka kuhusishwa na
vurugu za Bagamoyo. Lakini majibu yapo.
Wakati
CCM wanatishia kuuhalifu Muafaka waliousaini kwa mbwembwe na ahadi
nyingi mwaka 2001, CUF wamekuwa wakilalamika mara kwa mara kwamba
utekelezaji wa masuala muhimu yaliyobainishwa kwenye hati ya
Muafaka umepuuzwa na Serikali za CCM, hususan hii ya Mapinduzi
Daima (SMZ). Viongozi wa CUF wamekuwa wakilaumu ya kuwa mambo
yanayotokea Zanzibar yanatia hofu kwamba muafaka umewekwa kando na
CCM na kuamua kutumia mbinu za medani kuendesha
siasa.
Hapatafutwi mchawi lakini mshikwa na
ngozi ndiye mwizi wa ngombe. Tunapoambiwa gari za chama zinakutwa
kwenye matukio ya kihuni usiku na mchana huku yakiwa yamebeba
vijana wanaofanana na wale wa Sudan, tusemeje? Tatizo ni kwamba
hata machafu yaliyopangwa kufanyika yawe yamefanywa kwa ustadi
namna gani, dalili za uchaguzi hazitoki zote. Dalili za kuwepo
mkono wa chama tawala katika matukio mengi wakati wa uandikishaji
wapiga kura Zanzibar hazikufutika hadi leo.
Wafuasi
wa upinzani wakifanya uhuni haichukui siku kukamatwa na huchukua
zaidi ya saa 48 ndio hufikishwa mahakamani. Wengi wao huachiwa
vituoni mwa Polisi kwa hongo inayoshibishwa wakuu wa jeshi hili.
Wanaotiwa katika mitihani ya kushikwa kila wakati kunapotokea
uhuni uliopangwa ni watu tunaoishi nao mitaani kwa hivyo hawafichi
yanayowasibu wanapokuwa vituoni na njia wanayolazimishwa kuingia
ili kuachiwa.
Kama vikosi vya vijana
waliopangwa kando ya barabara wakati wa mapokezi ya wagombea wa
viti vya enzi katika uchaguzi ujao walikutwa na fulana nyekundu,
si rahisi kuwatenganisha na wale waliokutwa na fulana kama hizo
kwenye matawi ya chama na kukutwa na madumu na chupa za petroli
wakichoma viwanda vya mbao. Walinzi hawakuficha chochote
waliposhikwa Polisi lakini nani kafunguliwa mashitaka ya uharibifu
wa kiwanda cha Sana Express cha Kinazini (Saateni), nani kashikwa
kuhusu kiwanda cha Magogoni (Msumbiji) na nani kashikwa kuhusu
kiwanda cha Kidimni (Koani)?
Nani kashikwa
kuhusu uhalifu dhidi ya nyumbani kwa mwakilishi wa Chambani
uliosababisha madhara makubwa kwa Mzee Juma Muhunzi? Nani kashikwa
kuhusu ukatili na uharamia wa nguvu wa kuvamia raia wasio na hatia
katika foleni ya kusubiri kuandikishwa kuwa wapiga kura Kituo cha
Kinuni, Tumekuja, na uharamia mwingine wa kuteketeza kwa moto
nyumba za raia wa Kianga Kijijini? Eti usiku kucha doria ya Polisi
wakiondoka tu alfajiri, nyumba zinachomwa moto. Uhuni
mkubwa.
Sasa kama Muafaka wa CCM na CUF
unazungumzia kwamba daftari la kudumu la wapiga kura ni hatua
makini ya kuleta uchaguzi huru na wa haki na wa amani, halafu
tushuhudie uchafuzi wa daftari hili huku kukiwa hakuna hatua
madhubuti zilizochukuliwa dhidi ya wachafuzi, tuamini kwamba
watawala wangali na shida na Muafaka? Si kweli hata kidogo.
Muafaka ni kuleta uadilifu katika siasa.
Rais
Benjamin Mkapa anapomtaka Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula leo
aitishe haraka kikao cha Kamati ya Makatibu Wakuu wa vyama hivi
kuzungumzia Muafaka siku chache baada ya Rais Amani Abeid Karume
akikiri hadharani daftari kukumbwa na matatizo ya kiutawala, si
kitu cha bahati mbaya. Kuna matatizo ya kwelikweli yanayohitaji
kushughulikiwa sasa si halafu.
Lakini
matatizo haya yamekuwepo kwa muda mrefu na baadhi yake yamekuwa
yakipaliliwa kwa nguvu kupitia harakati za vyombo vya dola baada
ya viongozi wa dola wenyewe kutamka. Rais Mkapa mwenyewe
amekwishatamka ya kuwa atatumia hata ikibidi nguvu za dola
kukipatia chama chake ushindi, sasa nani anayeshangaa yanayotokea
kuhusu Muafaka? Si tunajua, Rais akisema tu jambo, wa chini yake
wanahangaika kuyatekeleza.
Katika rekodi,
tunaambiwa viongozi wa CUF wamemwandikia Rais Mkapa mara tano
kumtaka achukue hatua za kukwamua hali mbaya ya maendeleo ya
Muafaka lakini ametingwa na kazi za Ikulu. Huku Zanzibar, Rais
Karume hajakutana kwa miezi saba hivi na Tume ya Muafaka
aliyoiunda kuratibu utekelezaji wa Muafaka. Utaratibu unahitaji
kila mwezi angalau mara moja akutane na makamishna wa tume hii
lakini labda naye hana nafasi. Mwenyekiti Mwenza wa Tume hii,
Abubakar Khamis Bakary, amelalamika hivi karibuni kwamba mara
kadhaa vikao vya Tume vimeshindikana kwa sababu wajumbe wa CCM
hawafiki. Nini kimebaki kuamini CCM inaheshimu Muafaka?
Kwa
sababu ya yote hayo, hata wakati huu kwa mtazamo wangu wa mambo,
naona CCM ilishauvunja Muafaka na kinachofanyika ni jitihada tu za
kujaribu kuvutia wafadhili waendelee kukubali kwamba serikali
zimetimiza wajibu wake katika kuhakikisha unafanikiwa. Muafaka
ungetekelezwa kisawasawa, utandu ulioigubika hali ya mambo
Zanzibar usingekuwepo, wala wafadhili wasingeendelea kupata
wasiwasi juu ya hatima ya Zanzibar katika uchaguzi ulio mbele
yetu. Nawasihi wafadhili kwa kuwa wanatutakia mema, wasichoke
kutia shime uchaguzi ufanyike kwa uhuru, amani na kwa uwazi.
Tunasubiri kuona heshima ya Tanzania itakuwaje.
Ends.
|