Waraka Kutoka Unguja

July 3, 2005

By

Jabir Idrissa





Wanaukumbi wenzangu;

Ufuatao ni waraka uliochapishwa na Rai toleo la Juni 30. Wale walio mbali na Tanzania na hasa wasiobahatika kuyaona magazeti ya Tanzania na kwa kuwa yale ya Habari Corporation hayajatiwa kwenye mtandao, basi kwa faida yenu nawatilia netini humu.

Ahsateni.

 

Headline: Baraza la Wawakilishi nalo ni Taasisi ya Umma

na jabir idrissa

Nilisema hivi wiki iliyopita: Wazanzibari wangependa ofisi zao zipewe watu wenye ujuzi na utulivu katika kutoa huduma. Watu wanaoangalia athari za maamuzi yao kabla ya kuyatoa. Katika uanasheria, kuna haja ya Hakimu anapotaka kutoa hukumu, kupaswa kujiuliza mara kadhaa umma utaichukuliaje hukumu atakayoitoa? Basi kila ofisa wa ofisi ya umma (ya serikali) naye anawajibika kufikiri kwanza kabla ya kuamua. Ndio hapa tunasikia kuna mahitaji ya viongozi bora siyo bora viongozi. Katika utendaji kazi, tusiwe kama pweza kuvutia maslahi upande wetu. Tafakuri jambo jema.

 

Maneno haya nimeona ni vizuri kuyarudia leo hapa. Yana umuhimu mkubwa kurudiwa kwa sababu mada yangu safari hii inajikita ndani kabisa ya Baraza la Wawakilishi, chombo adhimu cha kuwasilisha masuala ya maslahi na wananchi. Katika chombo hiki hakutakiwi ubinafsi wa kiasi chochote kile. Kumbe wapo viongozi wanajisahau wamepelekwa mle ndani kwa sababu zipi.

 

Wapo viongozi katika chombo hiki hawatambui wajibu wao wakiwa katika chombo hiki na kwa sababu hiyo, kwao, kupiga vijembe wenzao ndio mchango mkubwa na wa pekee kila wakiruhusiwa kusema. Na hali hii iliyokuwepo hata baada ya kuanza kwa baraza la kwanza lenye wawakilishi mchanganyiko mara baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 1995, imenikumbusha nyuma kidogo.

 

Wapiga kura wa jimbo la Mkunazini (wakati ule) walipiga kura ya kutokuwa na imani na mbunge wao baada ya kuona hawakilishi mawazo yao ndani ya Bunge bali akitumia muda mwingi kueleza yasiyosaidia maendeleo na maslahi ya jimbo lake. Watu wanaweza kusema hatua ya wapiga kura wale haikuwa na nguvu yoyote kwa sababu haikufanikisha mbunge yule kuachia kiti, lakini kidemokrasia, wapiga kura walionyesha kutoridhika kwao na utendaji wa mbunge wao. Sema tu hatujawa katika jamii iliyoshiba utamaduni wa mtu kuachia nafasi akiona amekanwa na watu wake.

 

Na ndipo yalipokuja mawazo ya kutaka iwepo sheria inayoruhusu wapiga kura kuweza kumkataa mwakilishi wao katika vyombo hivi wakitosheka kuwa hafai tena kuwakilisha mawazo yao kwa mujibu wa yalivyo maslahi yao. Tatizo kubwa hapa ni kutokuwepo misingi madhubuti ya kuendeshwa nchi kidemokrasia. Tuliingia kwanza katika mfumo ndipo tutafute misingi ya kufanya shughuli zetu kwa kuzingatia misingi.

 

Tumetafuta soji kabla ya farasi. Matokeo yake soji limekuwa haliendani na farasi tuliyempata na ni vigumu kutafuta farasi mpya anayelingana na soji tuliyokwishagharimika kuinunua. Balaa tupu na tupo kwenye kona tunahitaji msaada mkubwa na muafaka madhubuti. Kwa hakika, njia bado ndefu na ina miiba. Labda hatimaye tutavuka mkondo na kufika salama safari yetu ya kupata kuishi kwenye nchi ya maziwa na mito iliyonona na ikiwa haijachafuliwa mazingira yake. Amin.

 

Pengine tungali na watu wasiofahamu maana hasa ya chombo cha kutunga sheria: Baraza la Wawakilishi hapa kwetu. Jamani hiki ni chombo adhimu. Chombo kinachotarajiwa kunufaisha wananchi bila ya kuwabagua kwa aina yoyote ile ya ubaguzi. Chombo adhimu kinachostahiki kila sifa ya kuwa ni chachu ya kuendeleza watu wa nchi yetu Zanzibar. Chombo adhimu chenye jukumu zito la kuendeleza uhusiano wa Zanzibar na Tanzania, Zanzibar na nchi jirani, Zanzibar na Afrika, Zanzibar na Asia, Zanzibar na Australia, Zanzibar na Uropa, Zanzibar na Marekani. Uhusiano mzuri wa Zanzibar na dunia bwana.

 

Hiki si chombo cha mzaha hata kidogo. Ndani ya ukumbi pale, si mahali pa mtu, mwakilishi mtu mzima, kujinasibu eti kafanya hivi na vile jimboni kwake, eti chama chake kimefanya hivi na vile, eti mapinduzi daima, eti kupinga kila kitu kwa kuwa tu kimesemwa na mpinzani wako. Sivyo na haitakiwi kuwa hivyo hata kidogo. Baraza la Wawakilishi ni chombo kinachotakiwa kuwa njia ya kutatulia matatizo ya umasikini mkali unaowakumba wana wa Unguja na Pemba. Si chombo cha kutolea moshi wa chama fulani cha siasa.

 

Kila mtu aliye ndani ya chombo hiki anapaswa kutambua kwamba akipewa nafasi ya kuzungumza basi anatakiwa achunge atakayo kuyasema. Afikiri mara mbili kabla ya kuomba nafasi ya kuzungumza. Afikiri anayotaka kuyasema yatasaidia nini azma ya kuondoa (siyo kupunguza) umasikini unaozidi kuwatambalia wananchi akianzia na wapiga kura wa jimbo atokalo.

 

Mazungumzo ya ndani ya chombo hiki yasiwe ya kuonyesha ubabe wa chama kwa sababu kama chama kila mtu ana chake, na kwa kweli wapo wasiokuwa na vyama na wanataraji wasemewe kwa yale yenye maslahi nao. Wa kuyasema haya ni yule aliye ndani, mwakilishi aliyeingia kupitia tiketi ya chama. Ndivyo itakavyo sheria uingie kupitia chama, lakini tambua ya kuwa ukishaingia unawakilisha kila mtu wa jimboni kwako siyo tu wa chama chako.

 

Kwanza hufahamu kwa uhakika kama wote wa chama chako walikupigia au wote wasiokuwa na vyama hawakukutilia voti. Ni uhuni tu unaofanyika petu lakini haitakiwi kuwepo namna ya mpiga kura kutambulika amempigia mgombea gani. Niisemayo ndiyo demokrasia iliyopea ambayo mizengwe na takrima si njia ya kuingilia kwenye chombo hiki.

 

Hiyo ni kwa waliopigiwa kura kuwakilisha wananchi ndani ya Baraza la Wawakilishi. Wajibu wao hauna tofauti na wajibu wa kiongozi wa Baraza, Spika anayeongoza vikao. Naye ana wajibu wa kuongoza chombo hiki kwa uadilifu wa kuonekana hasa si wa kuhisiwa. Spika anapokuwa muadilifu, atachunga heshima ya Baraza na asipokuwa atavunja heshima ya Baraza hili. Uadilifu unatakiwa kwa kutoruhusu wawakilishi kukashifiana kwa namna yoyote ile.

 

Uadilifu unatakiwa udhihirike kwa kutoruhusu mwakilishi kusema asiyoyafahamu au kusema ya kubuni kama zisemavyo kanuni. Lakini ni namna nyingine ya kuchunga uadilifu pale Spika anapotenda haki kwa wawakilishi wote bila ya kuzingatia fulani ni wa chama gani. Kwa sababu Spika anatokana na chama cha siasa, haitarajiwi kwa namna yoyote adhihirishe ukereketwa wa chama chake akiwa kwenye kiti kile cha enzi. Kutenda kwa usawa na haki ndio iwe msingi mkuu.

 

Baraza la Wawakilishi liongozwe kwa kanuni na sheria si utashi wa Spika. Inakirihisha kuona kiongozi wa chombo hiki anapalilia ukereketwa ndani ya Baraza hata kwa kuzitenga kanuni. Ikitokea mwakilishi anatoa maelezo yaliyo kinyume na kanuni za Baraza, ni kumsimamisha haraka. Mkiukaji kanuni hapaswi kuonewa huruma. Kuna kitu kimenishangaza kukishuhudia. Mwakilishi anahoji uthabiti wa maelezo ya mwenzake lakini ikabainika ni kinyume na kanuni. Ni uadilifu kuchunga ile kanuni kuliko kuachia ile hoja iendelee.

 

Tumeshuhudia mara nyingi majaji wanapozikataa rufaa kwa sababu katika kuwasilishwa kwake, utaratibu wa kisheria haukufuatwa. Jaji hapaswi na kwa kweli wengi walio waadilifu wanakwepa kujiingiza katika mtego wa kulazimisha rufaa hiyo isikilizwe eti kwa sababu ni nzuri na ina umuhimu. Kufuata utaratibu wa kuiwasilisha hiyo rufaa ni moja ya msingi mkuu wa utendaji haki katika mahakama, na kwa hivyo katika chombo chochote kinachotakiwa kutenda kwa haki.

 

Kiongozi wa Baraza anaporuhusu mwakilishi aliyekiuka utaratibu katika kuwasilisha hoja barazani, anapalilia kiburi kwa huyo mwakilishi aliyeruhusiwa na papo hapo anamtia katika unyonge yule anayekusudiwa kuathirika na hoja hiyo ikitolewa. Hapa inaonyesha wazi haki haikuzingatiwa badala yake utashi wa mtu. Hii ni hatari kwa vyombo vyenye majukumu mazito kinchi kama Baraza la Wawakilishi.

 

Lazima iingie katika akili ya kila mmoja wetu imani kwamba Baraza la Wawakilishi ni moja ya mihimili mikuu mitatu ya uongozi wa nchi, ikijumuishwa na Utawala (Serikali) na Mahakama. Kama mhimili huu utakuwa unayumba katika utendaji wake itakuwa si vingine bali kuashiria kwamba bado tuna safari ndefu ya kuondoa umasikini. Umasikini wa kwanza tulionao wengi wetu ni wa kifikra, nao wapasa kuondoshwa mawazoni mwetu.

 

Hata katika dini tunaambiwa mtendee mwenzio unayopenda kutendewa wewe. Maana yake mtendee mazuri kwa sababu nawe unapenda mazuri. Kauli hii imekusudiwa kujenga uadilifu si kitu kingine. Uadilifu unatakiwa katika kukaribisha mijadala inayojenga jamii siyo inayochochea uhasama. Kwa kuwa Baraza la Wawakilishi nalo ni taasisi ya umma kwa maslahi ya umma, basi ingekuwa jambo jema, uendeshaji wake ukawa unaozingatia tu kanuni si jambo jingine.

 

Mada hii nitaiendeleza wiki ijayo kwa kubainisha mifano inayoonyesha udhaifu na umakini katika mijadala barazani.

Ends.