Waraka Kutoka Unguja

July 10, 2005

By

Jabir Idrissa



Wanaukumbi Aslaam Aleykum;

Nisameheni kwa kushindwa kuwatilia waraka wa wiki iliyopita. mahangaiko yalinitinga. kwa hisani zenu, naomba muupokee. hii ni faida kubwa kwa wale walio mbali na Tanzania linakofika gazeti la Rai zinamochapishwa makala za uchambuzi ikiwemo ya Waraka kutoka Unguja. bakhti mbaya Habari Corporation haijatia magazeti yake kwenye mtandao. Inshallah Jumamosi nitawatilia wa wiki hii.

Ahsanteni.

Jabir Idrissa+

Headline: Baraza la Wawakilishi ni Taasisi ya Umma (3)

 

Baraza la Wawakilishi linatumiwa vibaya, wakati linatarajiwa kuipeleka Zanzibar kwenye utandawazi ule wa kuchagua yanayotufaa na kuyatengeneza kwa mazingira yaliopo kwetu. Wapi?

 

Tulilonalo ni baraza la viongozi wenye uwajibikaji mdogo kwa umma. Wananchi wanaumia kwa ufukara mijini na vijijini, unaotokana na kipato kisichotosheleza mahitaji yao, wengi hawana maji ya uhakika, safi na salama na fedha za kununulia dawa nje ya Hospitali Kuu ya Mnazimmoja. Lakini wawakilishi wanapiga siasa barazani. Kila wapinzani wakiuliza inakuwa nongwa, majibu ni vijembe.

 

Maswali hayajibiwi ipasavyo na mawaziri. Hayajibiwi ipasavyo kwasababu utasemaje unaposikia waziri anajibu “nitamjibu kwa maandishi”, “nitampatia maelezo ya kutosha tukionana baada ya hapa”,  “namuomba mheshimiwa mwakilishi tushirikiane kutatua tatizo hili”, “namuomba anistahamilie kwa sababu takwimu sahihi sinazo hapa”.

 

Namkumbuka Waziri wa Ujenzi wa Dar es Salaam, John Magufuli. Namuita kamusi kwa sababu hana asichokijua katika eneo lake, na si kwa hisia, kwa uhakika hasa wa kilivyo. Anayajua madaraja makubwa na madogo yanayopita kwenye barabara kuu mijini na vijijini, anayajua si kwamba yapo tu, bali hata vipimo vyake vyote anavijua. Anajua habari ya nyumba za serikali, wapi zilipo, lini zilijengwa, marekebisho gani zinahitaji. Waziri Magufuli ni dictionaray bwana katika eneo lake. Sijamuona waziri namna hii barazani kwetu.

 

Uhodari wa waziri unahitaji mwenyewe kujishughulisha kwa mambo yanayohusu wizara anayoiongoza, lakini pia ana nafasi kubwa ya kujua mengi akitumia wasaidizi wake; wakurugenzi wa idara, makamishna wa kamisheni, wakuu wa taasisi na kadhalika. Akiwabana hawa, hakuna kitakachomshinda. Hawezi tena kusimama pale barazani akaueleza umma unaomsikiliza kwamba “sina takwimu hapa.” Wewe ni waziri unao wasaidizi wako, unao wataalamu wako lazima wajue kila kitu na wakujulishe wewe ili ujiweke makini ukiulizwa. Unajua katika orodha lipo swali kwanini usikusanye faili zima la eneo hilo ukaingia nalo barazani. Au unadhani wawakilishi wote ni kama wewe, hawafanyi kazi zao za nyumbani vizuri kabla ya kuja barazani. Wapo wenye uwezo mkubwa na ndio hao wakiuliza hawapati majibu ila kuonekana wambeya. Kwa hivyo mwakilishi bora aingie na kusinzia tu halafu asaini posho ya kutwa.

 

Yote haya yanatokea barazani ikionyesha kuna tatizo kubwa la uwezo wa baadhi ya mawaziri katika kufahamu shughuli za wizara zao. Kwa sababu hawajali majukumu yao, na makatibu wakuu wao, wakurugenzi na makamishna wao, wanawaacha vivyo wakome. Tatizo la uvivu wa kufikiri, na uwezo mdogo wa kutenda, kama asemavyo Rais Benjamin Mkapa. Wazungu wanasema true colour inajionyesha!

 

Hakuna kingine isipokuwa Zanzibar inahitaji mabadiliko ya kila namna na kila sekta ya maisha ndipo itajitoa katika umasikini wa kujitakia. Ilionao ni umasikini wa kujitakia kwa sababu inazo raslimali nyingi zilizosaidia nchi kama Mauritius kujikwamua hata leo kuwa ya mfano kwa Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara. Mauritius ina kipato cha dola 5,000 kwa mwaka kwa raia wake wakati sisi hatujafikia dola 300 kwa mtu.

 

Wao wana vifo 14 kwa watoto wachanga katika kila 1,000 dhidi ya 102 tulionao Zanzibar. Maana yake nini? Serikali ya Mauritius ina mtandao mzuri wa kujenga uchumi wake na matokeo yake matunda ya mafanikio yanarudi kwa raia zake. Wajawazito wanahudumiwa vizuri, wanalindwa dhidi ya magonjwa kama malaria yanayoua wajawazito na wazaliwa wengi Zanzibar.

 

Tofauti yetu nini na wao katika raslimali? Wanayo ardhi nasi tunayo, wanayo bahari inawazunguka, nasi tunayo ya kutosha, kwa hivyo wanategemea pia utalii, nasi tunayo hazina ya kustawisha utalii. Wanao wataalamu, nasi tunao. Nini sasa? Zile kelele zipigwazo na wahisani wakiwemo mataifa tajiri zaidi duniani yaitwayo G8: tunapalilia rushwa, tunaviza demokrasia, tunadharau utawala wa sheria, tunapuuza utawala bora na tunakiuka haki za binadamu.

 

Serikali na taasisi zake wanapodharau amri na maamuzi ya mahakama kama inavyofanyika kuhusu suala la Abdalla Shariff wa Shakani aliyehalalishiwa na Mahakama zote umiliki wa ardhi iliyovamiwa au suala la Nasser Rashid Nasser (Cholo) aliyetakiwa asiondoke nchini lakini ametoroshewa Dar es Salaam, maana yake nini? Wanajenga au wanabomoa? Mambo matatu yanapaliliwa hapa: dharau ya mahakama, uvunjaji haki za binadamu na ukosefu wa heshima kwa utawala bora.

 

Serikali inapompa mtu kazi bila ya kutangaza zabuni ilhali sheria ya zabuni ipo, inaporuhusu mtu kuiuzia tofali kwa sh 600 badala ya sh 250 mpaka 300, inapostawisha ukiritimba katika biashara ya mafuta huku ikidai imeacha biashara huria, inapojenga kituo cha afya msituni kama Founi Uwandani, na isipeleke daktari wala muuguzi, ni ukosefu wa heshima kwa watu wake, ni uvunjaji wa misingi ya utawala bora. Ni kuimarisha uozo na ndipo hapo wahisani wanapiga kelele.

 

Itatuchukua karne nzima kuifikia Mauritius kimaendeleo kwa mtindo huu. Wao wana uchumi mzuri kwa sababu wametumia vizuri raslimali na si kuzifuja. Wanaopewa kazi ya kuongoza wenzao hawatumii ubaguzi na uzandiki. Watapiga hatua nyingi mbele sisi kutambaa itaendelea kuwa ndoto. Ndipo tunaposema tunahitaji mabadiliko ili tujikwamue.

 

Awe mtu ana uwezo wa kazi ndio ateuliwe kuongoza tangu chini mpaka juu. Maendeleo yanaanzia kwenye nyumba. Tufike wakati mteuzi atafute mtu kwanza na kumteua Sheha, badala ya kumteua Sheha na kumpa kazi. Umetizama uwezo wake na uadilifu wake? Si kila mtu anafaa kuongoza jamani. Vigezo muhimu!

 

Niliahidi kuliendeleza suala la mwandishi wa habari wa gazeti la Nipashe, Mwinyi Sadallah aliyepo Zanzibar, kutakiwa aombe radhi serikali kwa kile alichokiripoti kutoka ndani ya Baraza la Wawakilishi akimnukuu mjumbe wa baraza hilo. Wakubwa wanasema kilichoripotiwa ni matokeo ya tafsiri potofu ya mwandishi wa habari. Eti alifanya tafsiri potofu tu, si kwamba alimkariri msemaji sivyo.

 

Kuna namna mbili katika maelezo yanayohusu suala hili yaliyotolewa na Ikulu ya Zanzibar: kwanza Serikali inajenga picha ikitaka watu waamini ya kuwa aliyenukuliwa na mwandishi hakutenda kosa. Pili ni ile kwamba kosa limetendeka kwa mwandishi kutokana na kufanya tafisiri ambayo kwao, Ofisi ya Rais, tafsiri inayodaiwa kufanywa haikuwa sahihi.

 

Kwanza suala limefikia hatua nyingine. Mwandishi anayejengewa hoja ya kufanya tafsiri potofu hana haja ya kuomba radhi bali ni wajibu wa Mhariri wake. Barua iliyotumwa kwa Mhariri ambayo imeambatanishwa na nakala ya kumbukumbu (kitaalamu inaitwa hansard) ya Baraza, inamtaka kufikia Julai 11 (Jumatatu) awe ameandika taarifa ya kuliomba radhi Baraza kwa “kulisingizia.” Afanye hivyo katika ukurasa wa mbele na kwa nafasi kama iliyotumika kutolea taarifa ya awali. Akishindwa kutekeleza hayo, “hatua za kisheria zitafuata mkondo.”

 

Duru za ufuatiliaji suala hilo zimesema kwa makusudi ‘ngoma’ imetupwa kwa Mhariri wa gazeti ingawa barua ya Katibu wa Baraza wa Wawakilishi ninayejua anafanya kazi asiyoipendelea kwa suala hili, inamsema hivi mwandishi: “juu ya tabia yake ya mara kwa mara ya kupotosha taarifa za vikao vya Baraza.” Hapa Zanzibar aachwe mwandishi anayependa kupotosha taarifa za Baraza, tangu lini? Mwandishi hajatenda kosa anaandamwa atende, tena mara kwa mara, aachiwe? Jaguju. Ukweli ni kwamba wakubwa wanajua fika mwandishi alifanya kazi yake vizuri lakini yaliyosemwa ni machungu kuyameza.

 

Waandishi wa habari Zanzibar tunajua mengi kuliko wakubwa wanavyofikiria. Kwani hatujui kwamba kuna mtu anaitwa Salum Abubakar alipewa kazi ya ujenzi sehemu, alilipwa na nani? Kuna mtu alitoa fedha mfukoni kumlipa basi hili lisemwe hadharani?

 

 

 

Naam, alikuwa mwakilishi Said Ali Mbarouk wa jimbo la Gando, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba aliyetoa malalamiko kuhusu kitendo cha Rais kukaa katika nyumba binafsi wakati Serikali inazo nyumba tatu mjini Zanzibar kwa ajili ya makazi yake. Akatoa mfano wa kwa hivyo rais akitoka Makunduchi serikali ijenge nyumba Makunduchi na akitoka Tumbatu ijengwe nyumba Tumbatu. Kwenye nakala ya hansard iliyoambatanishwa na barua aliyotumiwa Mhariri wa Nipashe, maneno hayo hayaonekani. Sasa yamekwenda wapi?

 

Isitoshe kwa kutaka aeleweke zaidi hoja yake, mwakilishi wa Gando alifanya kutoa mfano kwa kumtaja mwakilishi wa Rahaleo, Hafidh Ali Tahir, kuwa hivi naye akipata kuchaguliwa kuwa Rais basi naye aseme “nina nyumba yangu Maungani nakwenda kukaa kule, hili ni tatizo, utakuwa huu ni mchezo ambao hauwezekani, lazima tutamtaka tumuone hapa. Ile sehemu ya serikali tutamtengenezea hapa kama ni rangi, kama ni carpet, kama ni samani tutanunua kuhakikisha kwamba anakaa katika nyumba ambayo ni standard kwa wakati huo itakuwa lazima aishi. Hatutopenda kutoa pesa zetu kwenda kumtengenezea nyumba yake ile ya ghorofa pale Maungani. Mhe. Spika, hili nashauri kwa nia njema kwamba tulishughulikie.”

 

Inaeleweka wazi kwamba kulikuwa na jitihada nyingi za kutaka mwandishi abadilishe alichokiripoti lakini alisema wazi hana ila alichokiandika. Alitoa kauli hii mbele ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliyeita baadhi ya waandishi ofisini kwake kuzungumzia suala hilo. Kwa kuona mwandishi amesimama kidete na kwamba upo ushahidi wa alichokisema, amekwepwa na kutupiwa mzigo Mhariri wake.

 

Kitu kizuri katika suala hili ni kwamba wakati baadhi ya viongozi wa juu walipohusishwa, kama ni mbinu chafu ya kutaka kuwaingiza, walitoa indhari ya kuwa wanaweza kuja kukwama mbele kwa sababu kila kitu kinajulikana. Hapa ni Zanzibar, sema na wenzako wanne hata watano asubuhi, adhuhuri wanayajua wengine sokoni na magharibi yamefika majumbani. Sisi wamoja tu ziwepo jitihada nyingi vipi za kujaribu kututenganisha. Na hii itaendelea kadiri tusivyokuwa na utawala mzuri nchini. Kwa Mwinyi mimi nasema heko umeonyesha msimamo unaotakiwa na Mhariri hujaomba radhi nikiamini huombi. Acha suala hili lifike mahakamani ambako mwandishi na gazeti watapewa fursa ya kujieleza. Kitu kizuri na ukweli utajulikana.

 

Baraza litumiwe vizuri kwa maslahi ya umma badala ya kutafuta watu uchawi, kutungiana majungu. Hiki ni chombo adhimu na muhimu kwa maendeleo ya watu, kwa kubadilisha sura ya nchi. Nchi yenye chombo  cha kutunga sheria kilicho madhubuti, ina nafasi ya kupiga hatua ya kupata uchumi mzuri, utawala bora, utawala wa sheria na heshima kwa haki za binadamu, nyenzo muhimu za kubadilisha nchi kimaisha. Mabadiliko ya maana yatakayolinda misingi ya uhuru wa kila chombo kati ya vile vilivyo mihimili katika uendeshaji wa nchi, ndiyo yanayotakiwa na umma.

Ends.