Mwaka 2005 uwe wa kuijengea Z'bar hatima
Waraka kutoka Unguja
Na jabir idrissa
Mwaka
2005 umeingia na umetuingilia huku tukikumbuka maafa ya kijinga
yaliyotokea wakati wa uandikishaji wa watu katika Daftari la Kudumu la
Wapiga Kura. Yale yalikuwa maafa ya kijinga kwa sababu kulikuwa na
sababu nyingi za kuyaepuka.
Kama hujafahamu nini
tunazungumzia kuhusu suala hili, hebu jiulize ni kwanini kuna utulivu
mkubwa wakati huu uandikishaji unapoendelea katika Mkoa wa Kaskazini
Pemba. Ukiwa ulisoma waraka uliopita umepata jibu. Nimeondoka Pemba
lakini ripoti mbalimbali zinazonijia zinathibitisha kuna utulivu wa
hali ya juu vituoni.
Kwa sababu hiyo basi,
nachukua fursa hii kuwaunga mkono wote, iwe kwa makundi ya kibinafsi,
mtu binafsi yake au makundi ya kitaasisi, waliochangia kustawi kwa
utulivu kwenye vituo vya uandikishaji. Kutoka ndani ya moyo wangu,
nawajuvya kuwa wanayotenda hata kuchangia utulivu huu, ndio uzalendo wa
kweli.
"Uzalendo wa kweli" itakuwa ndio mkazo
wangu mkubwa katika mwaka huu muhimu mno kwa Zanzibar kwa kuwa inaingia
katika mtihani mwingine utakaoijengea hatima. Itakuwa ni hatma mbaya au
nzuri. Kwanini?
Mara mbili, tangu kuingia tena kwa
mfumo wa vyama vingi (Zanzibar ilikuwa na vyama vingi kabla ya
Januari 12, 1964), wenye siasa za ushindani, Zanzibar imeshindwa
kujenga jamii ya kistaarabu inayong'arisha demokrasia ya kweli, siasa
za utengamano na mustakbali mzuri wa nchi. Hatujafanya uchaguzi mzuri
hata mara moja, ingawa huwa tunaanza vizuri lakini tamati inakuwa ya
mashaka matupu. Mashaka haya ndiyo yanakuwa chanzo kikuu cha matatizo
yanayofuatia uchaguzi huo.
Hatukuwa na muafaka
tulipoingia uchaguzini 1995 lakini baada ya matokeo kuwa ya mashaka
matupu, na kwa kuwa mashaka hayo yalisababisha nchi kukwama
kimaendeleo, na kwa kuwa watawala hawakuwa tayari kutumia nguvu ya
utawala kutandika mazingira mazuri kwa ajili ya uchaguzi wa 2000,
tuliingia tu huku mashaka yakiendelea.
Muafaka wa
1999 uliosimamiwa na Jumuiya ya Madola, ukaonekana upuuzi mtupu. Hakuna
wa kulaumiwa bali CCM ambao viongozi wao walisema mapema kuwa muafaka
huo hauna mashiko. Kauli za kukebehi muafaka huu zilikuwa dhahir shahir
upande huu. Kuteuliwa mjumbe wa kawaida wa Baraza la Wawakilishi
kuusaini kwa niaba yao, waliona haitoshi kuonyesha dharau juu ya
wananchi, wakazidisha kebehi kwa kauli nzitonzito ikiwemo ndani ya
Baraza tukufu. Ikathibitika utayari kwa chama hiki ulivyokuwa bado.
Wa
chama tawala wanaweza kuguna hapa, lakini ndiyo ukweli kwamba
mapendekezo yaliyokuwa katika muswada wa sheria wa Mabadiliko ya Katiba
ulioandaliwa (ilitakiwa uzingatie yaliyoafikiwa ndani ya Muafaka)
na Serikali iliyotokana na Mapinduzi matukufu, ili upitishwe kabla ya
uchaguzi ule wa pili, hayakuwa ya maslahi ya kweli ya wananchi wa
Zanzibar, zaidi ya kuwa ya watawala. Huu ndio ukweli.
Muswada
ungekuwa umetoa mapendekezo ya kuwezesha kuwepo mazingira mazuri ya
kufanyika uchaguzi ulio huru hasa, wa haki kabisa, na ulio wazi
kikwelikweli, mambo yangekuwa mengine. Na hili ndio tatizo letu la
msingi; kutengeneza kitu kwa ajili ya maslahi ya Zanzibar.
Mara
zote hapa kwetu, kwa kuwa kuna viongozi wanaendekeza uhafidhina wa
kutupwa, kinatengenezwa kitu kwa ajili ya kulinda maslahi ya wachache
wenye nacho dhidi ya wengi wasio nacho. Hawa wasio nacho, kwa kuwa ni
wengi kwa kila namna, wakionyesha kukataa kutumiliwa, ndipo mashaka
yanapokuja.
Na inafaa tukubaliane ya kuwa kupinga
kutumiliwa ni jambo la ukombozi wa nafsi na kwa maana tunayokusudia,
kwa nchi kwa ujumla wake. Hivyo lazma watu wapinge kutumiwa kwa sababu
wasipopinga wataingia katika dhima ya kuwa njia ya wengine kupanda
ngazi. Ni hapa hapa hupenda nisisitize kuwa Zanzibar, kama keki, ni
yetu sote na tuile kwa ushirika.
Hivyo kwa kuwa
mashaka yaliendelea baada ya uchaguzi wa 2000, na kwa kuwa wasio nacho
wengi walipinga kutumiwa kupandisha wachache ngazi ya kufaidi peke yao
keki tulohulukiwa sote na muumba, vyama vikuu vinavyotugawa Unguja na
Pemba, CCM na CUF, viliamua na viliketi.
Masikini!
Vyama vyenye watu wa kufaa kuheshimiwa vilivutwa mpaka kwenye kona,
vikawa havina pa kushika, isipokuwa kukaa pamoja, huku kila kimoja
kikijua fika kwamba ni kazi ngumu kukutana meza moja. Lakini angalau wa
CCM waliona wana dhamana ya ulinzi wa wananchi, lazma wakubali kukaa na
watu ambao kwa bahati mbaya, wanaowaona si lolote si chochote.
Wakubwa
hawa walipomaliza kutafakari makosa yaliyotendeka walitoa tamko mapema
la haja ya kuendeshwa siasa madhubuti zinazozingatia maslahi ya nchi na
watu wake. Tamko hili la Machi, lilihitimisha na Muafaka II uliosainiwa
Oktoba 9, 2001 viwanja vya Ikulu. Laiti kama si dharau ya muafaka wa
1999, kusingekuwa na Muafaka II asilan abadan.
Upinzani
unaposema hakutakuwa na Muafaka III si kwamba unatishia watawala, bali
unawatanabahisha kutekeleza wajibu wao kwa nchi na watu wake kuweka
mambo sawa ili uwanja wa ushindani uwe mwanana usiochoma. Kila chama
kinapotia mguu kiwanjani, kusiwe tena na kupigana madaluga. Si tunajua
kupigana madaluga ni dhambi mpirani!
Yaliyotokea
Mkoa wa Kusini Pemba katika uandikishaji wapiga kura ni ishara kuwa
bado tuna tatizo kubwa la wakubwa kutotaka mabadiliko. Huwa wanaamini
kuwa wanachokisema wao kupitia vyombo vya habari vinavyowatumikia
badala ya kutumikia umma, kitaungwa mkono na kila mtu tena kwa wakati
wote, maana wao ndio walioshika hatamu za uongozi wa nchi. Ni wao peke
yao hakuna wengine. Hatuna kingine ila kupata kiwanja mwanana cha
kupambana kisiasa.
Wengi tunaamini mchawi wa
Zanzibar angalipo. Naona hasa tungali naye karibu na anatafuta tu cha
kufanya ili azidi kudhihirisha ubaya wake kwa nchi yetu. Huyu ni mchawi
asiyetaka watu wa visiwa hivi watembee kifua wazi wakitamba kwa
maendeleo ya kweli si ya hadithi. Kwao, wacha, waione Zanzibar inapiga
hatua mwiko!
Wajua ikipiga hatua, nakusudia tukiwa
na utawala mzuri, sheria zikisimamiwa kwa haki si kwa kelele za
majukwaani huku watawala wakizipuuza amri za mahakama, huduma za jamii
zikiwa imara kikwelikweli, njia zikiwa zinawaka lami kisawasawa si kwa
kuhabatisha, na bandari ya Malindi ikiwa inasheheni meli kubwa na ndogo
za bidhaa za kuingia na kutoka, hakutakuwa na mivutano ya kijinga, na
isipokuwepo, wengi wa watu wanaoamini keki ni yao peke yao, watakuwa
wameanguka puu ja ndege aliyehujumiwa.
Ndio unajua
kwao siasa ni ajira, wasipokamata madaraka wameadhirika njiani. Si
tumekuwa tukiwaona baadhi yao wanavyokufa haraka mara wanapotoka.
Tunawaona hawa leo wanakodi milango ya maduka sawa na walalahoi,
wanapanda gari za umma nasi, wanaomba nafuu ya bei ya vitu
marikiti (sokoni), wanarudi kwenye baraza zetu walizokuwa
wameziasi kwa sababu ya ukubwa. Wafanyeje? Ni kwa sababu walichokipata
kimekwisha haraka wasivyotarajia kwa sababu kimetokana na dhulma tupu.
Kutetea
mauaji ni aina ya dhulma na kwa sababu muumba aliapa anayeitoa roho ya
kiumbe wake pasina kusimamia sheria aliyoiweka atamuadhibu naye, ndio
tunaona wanaadhirika mitaani wakitoka ukubwani. Mauaji ya kijinga
yanayotokea kutokana na mazingira ya ovyo yanayojengwa na watawala,
hayakubaliki. Damu ya mwananchi wa Shumba mjini mwaka 1992, ya wenzetu
wengine wa 2001, na hii ya Juma Omar Juma na Meja Ayoub Mohamed
Suleiman itarudishwa.
Ukisema hivi watawala
wanakasirika na kuishia kuandaa kesi. Wanaogopa kwamba watu wangali
wanakumbuka maovu yaliyotendwa nao. Na woga zaidi ni kwamba wanajua
kelele hizi zikiendelea, itatokea siku kweli itadhihiri. Na si uongo,
ukweli utadhihiri siku moja kama tunavyoshuhudia kwa Mzee Pinochet. Yu
kikongwe, lakini wapi Mahakama imempa nafasi ya haki yake ya kuhilikika
kwa maovu aliyoyafanya, hata kama si kwa mkono wake lakini alikuwa
kiongozi yakitendeka. Itakuwa hivyo hivyo.
Kwa
hivyo mwaka 2005 ni wa uchaguzi. Kila chama kinatengeneza karata zake
ili wakati utakapofika wazitupe kwa makini na kutegemea matunda makini.
CCM na CUF tunavitarajia ndivyo vitakavyoendelea kushikana koo hapa
kwetu Zanzibar. Vitaendelea kugombania kura labda 400,000 na kidogo za
Wazanzibari. Wanatafuta nini vyama hivi kutoka kwa umma? Ulwa tukiamini
ni kwa ajili ya kutumikia watu ambao takwimu zinaonyesha zaidi ya nusu
yao wanaishi chini ya kiwango cha umaskini kinachotakiwa na mataifa.
Wengi
wetu tunaishi bila ya kula milo mitatu kwa siku. Maana yake hatuna siha
ya kupambana na raia wa mataifa mengine katika ulimwengu uliojaa ustadi
katika kila nyanja, hata ya ujambazi, kwa sababu ya maendeleo makubwa
ya sayansi na teknolojia. Hakuna biashara, hakuna soko, hivyo hakuna
uchumi unaoweza kutuhudumia hivi tukiendelea kuzaliana kwa sababu
kwingi hakuna umeme watu ikiingia magharibi wafanyeje kama si kulala.
Tunajigamba
mijini tu huku wenzetu kule Kiuyu Mbuyuni, Maziwang'ombe, Shumba
Viamboni, Makangale, Msuka (Wilaya ya Micheweni), Gando, Mgogoni,
Kinyasini, Fundo Kisiwani, Ole dodo (Wete) wanalala gizani kila
siku. Tuko katika mpumbao mkubwa mijini kwa sababu wenye hatamu
hawawajibiki kuhudumia walio masikini vijijini. Akinamama wanatembea
masafa wakitafuta maji, vinginevyo waendelee kutegemea maji ya kisima.
Mkulima
wa Micheweni lazma aende mjini Wete kuuza viazi na ndizi zake kidogo
maana hakuna soko karibu naye. Mvuvi alazimike kusafiri kwa miezi
mitatu nje ya anapoishi akihangaika kutafuta soko nchini Kenya. Kipindi
hicho mama na watoto wake sita saba anamtegemea nani? Dunia
ilivyoharibika jamaa mara anaoa kule hata bila ya kupima virusi,
analeta nini nyumbani? Ukimwi.
Ndivyo anavyoteseka
mwanamke wa Kizanzibari wa kijijini. Anaachiwa familia kubwa huku waume
wametoka kwenda kuchuma mbali kwa sababu karibu nao mazingira ya
biashara, ya kilimo, ya uvuvi, ya viwanda, yamevurugwa kwa sababu ya
utawala mbovu.
Lahaula, hali ya Micheweni
imenisitikisha na wenzangu tukiwa katika semina ya kutathmini vipi sisi
waandishi wa habari tunaweza kufanya kusaidia kuondolewa umasikini.
Unakuta mtoto wa miaka kumi hana shule, eti katumwa mjini kuja kununua
vidonge vya Panadol lakini amepewa sh 20. Ataipata wapi? Unamuuliza
umetumwa kweli dawa, anakujibu "ni kweli amenituma mama maana
ndugu yangu anaumwa homa." Umepata kusikia kinachoitwa malaria kupona
kwa kidonge hiki? Hiki si ni kidonge cha kupozea tu nguvu za
malariaquine au zile zinazoitwa za kisasa zinazosumbua waumwaji kwa
kuwamaliza nguvu? Ndio lakini afanyeje mtoto huyu na ametumwa?
Unamuona
alivyo mchafu si wa nguo tu bali yaonyesha hajakoga kwa siku mbili
tatu, lakini usiulize kama amekula asubuhi. "Sijala kaka." Ikiwa
ni wewe utafanyaje? Unazo za kumpa kutosha kupata vidonge? Unafikiria
vidonge vitamezeka kwa mtoto ambaye hajala kitu na maziwa kufuani kwa
mama yanatoka kwa shida kwa sababu ya njaa pia. Utoe tu japo kidogo
kumsaidia. Huyo unampa angalau sh mia tatu. "Unasikia hii mia
kanunue dawa lakini hizi nunua unga pale ukampe mama mwambie hii zawadi
kutoka mjini tupike uji tunywe." Eti ndio tunaondoa umasikini hivi. Na
siku inayofuata?
Basi haya ndiyo maisha ya watu
wengi wa vijijini Unguja na Pemba. Hawawezi kupata milo mitatu, hawana
umeme, hawana maji safi na salama, wakiumwa hawana dawa maana hawana
uchumi nyumbani, ingawa wamezungukwa na mikarafuu, bahari kubwa
inayotambaa kwa masafa na fukwe murua za kuchochea watalii kutesa kabla
ya tsunami kuhamia. Pembeni mwao kuna ardhi ya rutba kwa kilimo, kuna
ardhi haina rutba lakini ikitengenezwa itazalisha kama si mazao ya
kilimo, basi viwanda vidogo vya usindikaji samaki, mbogamboga na
matunda mtawalia tuliyonayo.
Leo Pemba inafikia
wiki haina umeme kwa sababu hakuna mafuta ya kuendeshea vinu vya umeme
vya Wesha. Na hapa inasingiziwa tsunami imeleta fadhaa baharini kwa
hivyo eti meli haijafika kutoka Mombasa? Meli ya mafuta ilitumwa lini
wakati gharika ikija tayari inajulikana mafuta ya IDO yatakwisha? Mambo
ya wakubwa wakipata zulia wanaficha uzembe wao. Ndivyo tunavyokwenda
karne ya 21. Tubadilikeni maana inawezekana. Au kwanini haiwi?
Ni
kwa sababu hatuna wataalamu wazalendo, hatuna nyenzo kweli kama
tunavyoendelea kuambiwa tungali katika nchi changa na demokrasia
haiwezekani kwa sababu tungali na njaa matumboni? Si kweli. Vyote
tunavyo, tunao wataalamu maana wapo Wazanzibari kwa mamia nje ni
wataalamu walisomeshwa na serikali yetu lakini walibezwa wakatimkia
huko. Wana hamu ya kurudi lakini waje kufanya kazi na nani?
Tukubali
hatuna ukweli, hatu wazalendo wa nafsi zetu wala nchi. Tunajidai tu
kuipenda huku moyoni tunajipenda wenyewe tu. Ofisa wa serikali anajua
kumhamisha mtumishi atapaswa apatiwe mafao kwanza, analazimishwa ahame
kwanza, asipohama anafukuzwa. Walifukuzwa kwa mamia baada ya uchaguzi
1995, leo wanarudishwa kwa shingo upande. Barua zao hazijawafikia kwa
miezi miwili eti hawajulikani walipo? Walifukuziwa wapi mwituni?
Kinachotafutwa washindwe kuripoti mapema wafukuzwe tena.
Basi
ni kufukuzana tu kazini, na ukiwa si CCM ndio utajuta kuzaliwa au
kuhamia Zanzibar. Siku hizi hakuna kazi, nafasi ya kusoma nje, wala
nini kama hakuna uhakika u mwana CCM kidhati. Wakubwa wameweka mtandao
wa kutafuta mizizi ya muombaji kazi, baba yake, babu yake, na
waliowatangulia. Kisa? Unatafuta kazi. Usiondoke ukaenda nje
unakotakiwa. Mamia wako nje kwa namna hii.
Tunataka
uongozi utakaowaona hawa ni hazina, warudi hata kwa ahadi ndogondogo za
kuwapatia nyumba hizi mpya zinazosubiri huruma kugaiwa. Wawekwe pale,
wapatiwe gari mpya mpya zinazoshindana kwa honi mpaka vichochoroni
nyakati za usiku. Wapatiwe wafanye kazi ya umma badala ya kuziachia
zikipakia vimada na watoto wa kimayai. Nyingine (hasa za wazi)
hupakiwa miche ya migomba, makaa na vifaa vya ujenzi siku za Jumamosi
na Jumapili, safari za wapi? Sehemu ambako wakubwa wanajenga mahekalu.
Tuwe
wakweli tukitambua kuwa kuna kundi la wenzetu hawana chakula cha siku
na hawana pa kutegemea ila hapa nchini kwao. Tuonyeshe utu kwa
kuwasaidia kwa kila mtumishi na alipo. Nafasi aliyonayo ajue yaweza
kushikwa na mtu kama yeye hivyo asiwe mungu mtu; atumikie watu.
Tuondokane na ubwana na utwana ambao kwa bahati mbaya umerudi maofisini
kwa sura mpya baada ya kusokomezwa kupitia mapinduzi. Mapinduzi yenyewe
ni ya miaka 40 lakini nchi inarudishwa nyuma kwa zaidi ya miaka 100.
Ajabu na kweli. Itaendelea kwa hapa "Heri ya mwaka mpya 2005."
Ends.
_______________________________________________
Zanzinet mailing list
Zanzinet@zanzinet.org
http://www.zanzinet.org/mailman/listinfo.cgi/zanzinet