Kifo chake Zanzibari
23 may 1999
Nakualika hitima kifo chake zanzibari
Barua nayotuma ikufike jemadari
Ujule yanahima kufika uwe tayari
Tokea ulipo hama miaka ya dahari
Twalizidi kuzama maradhi makiriri
Daima kanaumwa kipenzi zanjewiri
Dawa zimekoma nyingi zenye kheri
Kensa imezama mauti yamejiri
Kaondoka daima mama zanzibari
Tulijaribu mapema kutibu kwa siri
Tukafanya hima labda tunusuri
Imetufika lawama kwanini tusisubiri
Mauti yake mama lilobaki nikaburi
Nalo walisakama wamo wamevinjari
Kulichimba hekima eti lina hatari
Upenuni wamezama wamo wanakariri
Mpango wametima tena upo tayari
Pengine utajinyima hitima wakihairi
Njoo tenda hima japo sema kwaheri
Usisahau ugema ndugu yangu jemadari
Kifo chake zenjibari kudumisha jamuhuri
Naomba kisha soma nijuze si tahayuri
Najuza kwa taaluma na wingi wako habari
Rais kuwa daima katiba twaisubiri
Namaliza nazizima nuru ya taa bahari
Kila nachosema ujue kiko tayari
Kaeni mkiyapima wazenji mtafakari
Mchache wa elimu
Baja
Kifo chake Zanzibari
24 may 1999
Wingu latanduka
Msiba huu na ule - zinjibari natamka
Mwanangu bado sifile - usinizike haraka
Jua lachomoza lile - wingu lile latanduka
Mwangaza ni ule pale - warudia kumurika
Kupatwa na masaibu - ni hikima za rabuka
Mitihani ya ajabu - wanangu kuweweseka
Hata mengine aibu - wanangu kubabaika
Ile mwanangu jawabu - ile pale ishafika
Subiri hebu ningoje - nitizame nainuka
Na hata nijikongoje - nipo kama mwanitaka
Wanangu nataka muje - moyo utafarajika
Ni machungu yalioje - wanangu kuatilika
Ni kama nyota angani - zinjibari namurika
Ninusuru ya manani - amina na muafaka
Saleh
Uhai wake Zanzibari
24 may 1999
Imenifika hilaki na mzigo wa lawama
Nje hakutokeki ndani kunanisakama
Jua sisameheki kwa maneno nilosema
Laiti ningehakiki katu singe nayasema
Kuona mahatuti ndipo pale katetema
Kadhani kuskuti nikutokwa na huruma
Mengi yamezatiti taabani wetu mama
Nikaona ya laiti tujiandae kwa hitima
Dawa iliyo smati mtini mlipo chuma
Nahizo zilonyeti zanafuu yake mama
Mnajuaje kizati afya yake ya daima
Kuwa hayamfiki mauti wetu mama
Muafaka sishariti wakulinda uzima
Wala simadhubuti kumponesha mama
Naona ndio tamati pemba weshasema
Marufuku kuketi wale walosimama
Ugonvi na tashtiti waendelea daima
Atasaini najati karandasi mlotuma
Lakini sikusaliti kasema mama salama
Nyumbani mikakati wapanga maziko mema
Katu sijamsaliti moyoni mapenzi ya mama
Nampenda marati mama awe mzima
Khofu imenizatiti akilini yanichoma
Naomba masahamati kama mama yumzima
Mchache wa elimu
Baja
Kifo chake Zanzibari
24 may 1999
Salaam
Nakushukuru mama kukiri kuwa uhai
Ya kuwa bado mzima ingawa ulizirai
Nzima yako kalima wanywa halua kwa chai
Na tena umesimama ya nyuma tena hujui
Kusema ku muangaza mwanao nimefurahi
Kusafika kwa giza kabla staftahi
Na vishindo kuchagiza jioni na asubuhi
Afyiayo kuchapuza mambo yetu kuyawahi
Uwambie ndugu zetu wasizue umekufa
Warudi nyumbani kwetu waje ziziba nyufa
Zinavuja nyoyo zetu kalafati kujazifa
Wasikimbie msitu zapungua zao sifa.
Mama useme sana kuwa dawa wahitaji
Wazilete kwa shehena waufanye ni mtaji
Waache mbuzi kuchuna unazama wetu mji
Yarabi ya subuhana tujazie mahitaji
Iwapo dawa tafika mama yetu hakikisha
Maishayo taokoka maradhiyo kusafisha
Donge nako tutafika hata kule kwetu wesha
Mama tamka hakika kwa kuwa muda waisha
Ally saleh
Barua ya muafaka
25 may 1999
Barua uloandika katika mwezi wapili
Umetuma menifika siku jumapili
Kukujibu ninataka kuanza kuinakili
Maneno mepangika mistari ya jamali
Nakshi zakushuka mezipanga kweli kweli
Lakini nina shaka mawazo kuyakubali
Umesifu muafaka eti njema dalili
Tena warukaruka wausifu kula hali
Wazipuuza shaka kwa pupa yakukubali
Maoni nakupa shika japo mimi nikombali
Daima kuaminika watu hao ni muhali
Chunga weka shaka muafaka mushkeli
Khofu moyo menifika madhubuti kwa dalili
Miaka iloyoondoka ulishinda kila hali
Kiti chako kakutoka kwa maguvu ukatili
Basi nakupa shika busara hii kalili
Muafaka tarajika uwe kitu cha halali
Lakini ukivunjika takulaumu dalali
Machozi tanimwaika nachelea udhalili
Kuchukua uloweka sikama kutupa mbali
Kama huo uhakika cheo chako ufahali
Kalamu yangu naweka kwa karatasi yapili
Majibu yako nataka japo maneno mawili
Uyatume kunifika yanitulize akili
Mchache wa elimu
Baja