.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Mapenzi

 

 

 

 

 

 

Related links

 

Mapenzi!

Date:  12 November 1999

  1. Mapenzi kitu ajabu, ni shani yake Manani
    Hayahitaji sababu, sababu ilo makini
    Hujimwaga bubububu, bububu maji ya pwani
    Watu wakataajabu, kilichokupata nini!
  2. Hayahitaji dhahabu, mapambo mingi mwilini
    Au wingi wa adabu, adabu za kizamani
    Jamani mapenzi tabu, tabu yake huioni!
    Mpaka uwe karibu, karibu yake mwendani!
  3. Mapenzi yakikusibu, yakasibu mtimani
    Wageuka kuwa zubu, kwa wingi wa hamkani!
    Wataraba kama dubu, dubu lisilo makani
    Bila wako mahabubu, hakika umashakani.
  4. Mapenzi kama zabibu, zabibu mbivu mtini
    Hata yawe ughaibu, utayafata kwa kani
    Humsemesha na bubu, mapenzi akibaini
    Wala hayana ubabu, ujana wa kizamani!
  5. Mapenzi si madhehebu, ya fikira au dini
    Mapenzi si ustarabu, si haiba wala fani
    Mapenzi si ukatibu, cheo hakina thamani
    Mapenzi yanaghilibu, ajabu hii jamani!
  6. Hayana utaratibu, mapenzi ni maluuni!
    Mapenzi kisebusebu, na kiroho mkononi!
    Mapenzi ni merikebu, isiyo nahodha ndani!
    Au punda mwenye nabu, hatari iso kifani.
  7. Mapenzi hayana jibu, mapenzi si mtihani!
    Mapenzi sio kitabu, cha kusoma darasani
    Mapenzi si aghalabu, kuwa sawa duniani
    Imechoka yangu nibu, kalamu naweka chini.

Hassan Ali,
Ottawa.

 

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet