|
|
Mwana Msambe Dhihaka
Date: 25 October, 2001
- Mwana msambe dhihaka, ni majani ya ukoka, tuyatunzeni.
Mwana kito kitukuka, ugomvi tumeshachoka, tuuateni.
Mwana msambe karaha, tumtunzeni.
- Mwana mwokovu fahali, tumtunze mwanamwali, zingatieni.
Mwana habibu kauli, tusikubali kitali, tahadharini.
Mwana msambe karaha, tumtunzeni.
- Paka shume lavinjari, letoroka guniani, tukumbukeni.
Hasidi wa mwanamwari, hamtaki muhisani, mfukuzeni.
Mwana msambe karaha, tumtunzeni.
- Kelele za mlangoni, mwenye nyumba burahani, tutambueni
Halahala na matoni, hoho imo ujitini, ikimbieni.
Mwana msambe karaha, tumtunzeni.
- Si usiku si mtana, kula kunywa usimama, wa hamkani.
Mwari sasa si usena, kuchoma kutafunana, tukuateni.
Mwana msambe karaha, tumtunzeni.
- Muungwana ni vitendo, fadhila tukitendewa, tushukuruni.
Hongera kwa huu mwendo, mwari akishaolewa, tufurahini.
Mwana msambe karaha, tumtunzeni.
Ahmed Rashid
|