|
|
Ya Rabbi Mola
Date: 16 June, 2001
- Ya Rabbi Mola Faridi, nakujia ni dhalili
Ya Rabbi Mola Wahidi, nimejaa ujahili
Ya Rabbi Mola Wadudi, wanitesa ubakhili
Kwa nini sikudhukuri, mimi ni mali ya nani?
- Ya Rabbi Mola Jalali, unitoe ujingani
Ya Rabbi Mola Kamali, nimeshindwa mtihani
Ya Rabbi Mola Zamili, nimepotea jangwani
Hutanitupa njiani, kwani mimi ni wa nani?
- Ya Rabbi Mola Karimu, sili sinywi cha haramu
Ya Rabbi Mola Rahimu , kamwe siishi dawamu
Ya Rabbi Mola Adhimu, sina kitu mahamumu
Nileje kitu si changu, nami ni mja wa Mungu?
Ahmed Rashid
Ya Rabbi Mola
Date: 16 June, 2001
Ya Rabbi ya Rahmani nirehemu mja wako
Ya Rabbi mola Manani ninaomba toba yako
Ya Rabbi mola Amini ghufrani sifa zako.
Kwa nini sikudhukuri ewe wangu Mwenye enzi.
Amour Nasser
Ya Rabbi Mola
Date: 16 June, 2001
- Ya Rabbi Mola Alimu, sitiri madhambi yangu
Ya Rabbi Mola Qayyumu, unilinde na machungu
Ya Rabbi Mola Hakimu, nayaogopa marungu
Nitatendaje ithimu, na siku kiko qiyamu?
- Ya Rabbi Mola Razzaki, nipe mja nitosheke
Ya Rabbi Mola Maliki, Kwako peke nijiweke
Ya Rabbi Mola Khaliki, shetani nipige teke
Nitakuwaje kiburi, sina lile sina hili?
- Ya Rabbi Mola Ghafuru, naasi wanisamehe
Ya Rabbi Mola Qadiru, nilinde nisiwe penhe
Ya Rabbi Mola Nadhiru, mja mimi hohe hahe
Yawaje sikudhukuri, Rabbana ya Rahmani?
- Ya Rabbi Mola Raufu, mja nimejaa hofu
Ya Rabbi Mola Latifu, ninashindwa na siafu
Ya Rabbi Mola Atifu, naja Kwako uniafu
Ni vipi sikudhukuri, Nawe u pamoja nami?
- Ya Rabbi Mola Majidu, ni Zako zote heshima
Ya Rabbi Mola Mujidu, nakuabudu kwa hima
Ya Rabbi Mola Muridu, kuwa nami kwa daima
Nitachezaje na zama, kumbe kesho ni qiyama?
Ahmed Rashid
|