|
|
Kibati!
Date: 27 Jul 2002
- Kibati ngoma ya inda, sijaona mfanowe
Ina vijana makinda, wanaopiga mayowe
Na malenga anadunda, kwa kuchokoza wenziwe
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
- Wababe kimewashinda, walipotaka wajuwe
Malenga aliwaponda, ikabadi wazomewe
Wakafungua mikanda, wapate yatupa mawe
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
- Warembo wanaodanda, wajionavyo wenyewe
Sauti kama kinanda, watafuta mfanowe
Ziligeuzwa magunda, mithili yake nguruwe
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
- Wee mpiga kayanda, nina maneno na wewe
Usijifanye kamanda, ujuwe yana mwishowe
Ngazi hiyo ulopanda, haikugeuzi mwewe
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
- Mwisho wa kuranda randa, nguvu Mola azitowe
Takupachuwa kwa panda, tukukeshee msewe
Tukutie kwenye sanda, uwe chakula cha chowe
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
- Haneni mtakaunda, kibati na malengawe
Wakifunguwa mafunda, Muhidini na Jumbewe
Mapengo kama mabanda, meno hana mdomowe
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
- Ingawa ninakipenda, ngoja wasia nitowe
Chataka kisu cha landa, kufuata mdundowe
Hashili usijekwenda, kheri wewe upumuwe.
Avumilia wee, kumbe chamtafuna kidonda.
Maa salaam.
Kassim
Kibati!
27 Jul 2002
- Kumbe mwenzetu mkali, wajificha vichakani
Ushairi wako ghali, wenye macho hawaoni
Na pia waona mbali, mbizi zako ni za shani.
Nduguyo
Hashil
Kibati!
Date: 27 Jul 2002
- Ama nionavyo kweli, bado sijawa wa sifa
Nikitunga tungo mbili, ya tatu sina umafa
Hivi huitwi mkali, bali mtunzi kifafa
Nawaomba maarifa, malenga wa kiswahili.
- Nawaita madalali, mlo juu ya ghorofa
Tokeni niwasaili, msinigeuze lofa
Mbaruku na Hashili, Salehe wacha dafafa
Nawaomba maarifa, malenga wa kiswahili.
- Nawe Mahiri humbali, zilete zako sahifa
Mwite na Hassani Ali, tuzizibe hizi nyufa
Ngongele wa manazili, singoje hadi arafa
Nawaomba maarifa, malenga wa kiswahili.
- Njooni nisijefeli, nikapatwa na maafa
Tatengeza maakuli, niwaandalie dhifa
Kwa mkeka wa ukili, sio juu ya masofa
Nawaomba maarifa, malenga wa kiswahili.
- Nimeishiwa kauli, na nina njaa ya kufa
Ngoja nitafute buli, nina mkate wa mofa
Nigange yangu akili, nangoja zenu taarifa
Nawaomba maarifa, malenga wa kiswahili.
Maa salaam.
Kassim
Kibati!
Date: 28 Jul 2002
- Salamu zimenifika, ndu'yangu Kassim Ali
Nimeitika labeika, wito mikono miwili
Tajitahidi kwandika, lau sahafia mbili
Kila zinapo punguka, kazi zangu na shughuli
- Natamani nikufate, lakini uliko mbali
Hukaribu nikupate, uliyo bahari kali
Tajaribu kwenda tete, kwa hatua mbili mbili
Kusudi nisikuwate, nikiwa ntahimili
- Mungu kakupa kipaji, pasi mwenyewe kujuwa
Khibra kakufariji, ukawa mwingi kwelewa
Huna unachohitaji, maarifa ushapewa
Huhitaji mkongoji, unakwenda sawa sawa
Maher
|