|
|
Kisa kilichonifika (shairi)
Date: 10 Aug 2002
- Ilikuwa saa nane, nimetoroka kazini
Siku ya jumaa nne, mchana jua kichwani
Sina hata pesa nane, kapanda gari njiani
Mbio nenda nimuone, mpenzi alo nyumbani
Nahamu naye ayuni
-
Nkawasili nyumbani, wambele wangu muango
Mekuta kitasa ndani, kimefungiwa na gongo
Nikenda wa ubavuni, meshindikwa kimipango
Meusukuma kwa chini, mgumu kama mpingo
Lipo jambo si uongo
-
Nikabaki mlangoni, nusu bega ukutani
Sijui nifanye nini, huyu bibi simuoni
Silewi kenda kwa nani, hayangii akilini
Hajibwaga zangu chini, moyo wanipiga ndani
Kwa uchungu siutani
-
Nikarukia ukuta, nikachupa hadi ndani
Mambo niliyoyakuta, chungu chapwaga jikoni
Mchuzi unatokota, unakauka chunguni
Na moto unafukuta, unazimaliza kuni
Meuepuwa motoni
-
Kubwa lilonishangaza, njia aliyotokea
Milango ameiweza, yote ameikomea
Hakuna alobakiza, hata tundu kupenyea
Chanipasuka kuwaza, kichwa nikifikiria
Khabithi amekimbia
-
Masaa kwenda pitani, dalili kuja sioni
Sasa niende kwa nani, najiuliza moyoni
Nianze kwa majirani, au ni kwao nyumbani
Ikanijia kichwani, bora nibaki makani
Mepiga konde moyoni
-
Ilipongia jioni, nusu jua limajini
Bibie yuko njiani, arudi miguu chini
Yeye hajanibaini, kuwa niko dirishani
Kakazana macho chini, kama mtu hayawani
Kajuwa yu mashakani
-
Sikumgoja kufika, nikatoka kwa haraka
Ghadhabu zimenishika, moyo ukiungulika
Nani sikushughulika, kujuwa anakotoka
Mempa yake talaka, aende anakotaka
Yaniepuke mashaka
Maher
Date: 10 Aug 2002
Umeifanya haraka, Kake Mahiri sikia
Kwa kuitoa talaka, Sisubiri kusikia
Kile kilichomfika, Bibie akakwambia
Ngesubiri kwanza kaka, Mwenzio kaelezea
Hujui kilomfika, Huko alikotokea
Hweupata uhakika, Haraka mmevamia
Alikutwa na mashaka, Sababu angekwambia
Ukaitoa talaka, Siweze kujitetea
Hata kama sehusika, Naona memuonea
Na awe mbaya fika, Hakiye kujitetea
Hapo ingefahamika, Mbichi na mbivuye pia
Lakini membandika, Talaka bila kujua
Kwa hapa nilipofika, Leo sitaendelea
Nakuomba wangu kaka, Jambo hili fikiria
Kwa kuitoa talaka, Bila nafasi kutoa
Bora ngepata hakika, Hatua ukachukua
Myonge wa Nyali
Mbarouk
N.York
Date: 11 Aug 2002
Hatua ulochukua, japokua si murua
Haki kwako kuchukua, kwa aliyokufanyia
Kutoka bila kujijua, kukuacha hofuu pia
Haya mambo wayatambua, hongera nakupa pia.
Salim.
Date: 11 Aug 2002
Kwa ndugu na majirani, tungo zenu kisikiya
Huburudika moyoni, sikio kafurahiya
Mwanikumbusha zamani, lugha wakiichezeya
Malenga wa kusifiya, adimu hatuwaoni
Chunga vina na mizani, ukitaka wafikiya
Mfano havilingani, vina vya owa na iya
Kitahadhari mwendani, haya ninayokwambiya
Mashaha tawafikiya, bila tatizo yakini
Ibrahim
Date: 12 Aug 2002
Ulilofanya si kosa, bali hukutumia hekima.
Hamaki zako hasa, sheitani amesimama.
Hujajua yalosaza, jahazi walizamisha?
Chama.
Date: 12 Aug 2002
Hatua uliyochukua, japo hukufikiria
Haki kwako kuchukua, kwa aliyokufanyia
Hutoka bila kujijua, kukuacha hofu pia
Haya mambo wayatambua, hongera nakupa pia.
Salim.
|