|
|
Machozi yalinitoka
Date: 15 Dec 2002
-
Safari ilinijia, sikupanga sikubuni
Rafiki yangu kangia, mchana niko kitini
Kaja kanizawadia, bahasha tiketi ndani
Kwa furaha kunambia, safiri nenda nyumbani
-
Mbio memkumbatia, nikamvuta pembeni
Asije mtu sikia, tunazungumza nini
Wakijuwa alojia, taingia mashakani
Yeye akaniridhia, akifahamu kwanini
-
Bila hata kuchelewa, haraka memuuliza
Kikubwa kilichokuwa, tiketi kujanitunza
Kanijibu nimepewa, na yule wako Aziza
Ufanye litalokuwa, wende ameniagiza
-
Begi nikalipachua, lilojuu kabatini
Nguo nikazitundua, zilizokuwa hengani
Baadhi nikachukua, zilizomo sandukuni
Nikapanga kipangua, zote ziingie ndani
-
Nikawaaga nyumbani, nakwenda zangu safari
Salaama usalimini, wakanambia kwaheri
Nikaenda uwanjani, ndege tayari tayari
Tukaruka tuhewani, hali ya hewa shuwari
-
Tukikaribu kutua, nje wingu limetanda
Kuteremka mvua, kushuka ikatushinda
Tukangoja kupungua, kwisha'jengoni tukenda
Muda haukuchukua, gari nikenda kupanda
-
Mvua bado kinyesha, nami nikiwa garini
Si yanguvu rasha rasha, miaka kiitamani
Mengi imenikumbusha, wakati wa utotoni
Njia nikainyoosha, moja kwa moja kwa eni
-
Pole pole meingia, akiwa usingizini
Wake meushikilia, mkono umkononi
Taratibu kimwambia, kinong'ona sikioni
Ewe mpenzi sikia, am'ka nakutamani
-
Sauti kuisikia, karuka hakuamini
Kuniona alilia, akanivaa mwilini
Neno alilonambia, ni wewe au ni nani
Huku kanishikilia, kama alivyo nguoni
-
Nami sikujizuia, yalinitoka machozi
Kwa kwikwi anavyolia, na kuzishusha pumzi
Ana mengi kunambia, kwa haliyake hawezi
Kila kimuangalia, yalinizidi majonzi
-
Nikamlaza shingoni, mkono kimpapasa
Mwengine uko begani, kiugonga kimuasa
Nikimpoza mwandani, ayasahau makosa
yakuishi ugenini, na mahaba kututesa
-
Tukazifanya dhihaka, kama watoto wawili
kwa furaha tukicheka, tukikumbuka awali
na nyoyo zikafunguka, mioyo ikakubali
nikawa nimeshafika, nikaapa sendi mbali
Maher Fundi.
|