.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Muamu

 

Related links

 

Muamu ...

Date: 27 Jul 2002

  1. Havisemeki, vituko vya muamu
    Sasa halitaki, langu la muhimu
    Anitia dhiki, na yangu kaumu
  2. Nilipowafiki, tuchanganye damu
    Na yangu batiki, nikaikesemu
    Nikampa rafiki, wangu muadhamu
  3. Pesa kwa lukuki, katoa sehemu
    Idhibiti benki, hilo sio gumu
    Nitunzie hati, zenye tarakimu
  4. Wamimine nyuki, washike hatamu
    Uwape bunduki, wachunge binamu
    Walinde kasiki, na vilivyo humu
  5. Wavalishe kaki, walinzi wa zamu
    Wapitishe reki, penye ndumu ndumu
    Wasostahiki, wasilete sumu
  6. Siwezi mikiki, we wangu mramu
    Ya nje ya miliki, chukua jukumu
    Na yaliyobaki, hayo tarasimu
  7. Akawa hachoki, mapenzi matamu
    Yakaniashiki, kapata wazimu
    Kujatahamaki, kashanihujumu
  8. Huwezi sadiki, orodha timamu
    Kuhusu itifaki, tuliyoazimu
    Sitaki dhihaki, kumi hayetimu
  9. Ametarazaki, akanidhulumu
    Madini samaki, elimu na simu
    Mgao hautoki, kwa kimaalumu
  10. Kachochea chuki, nikawahasimu
    Wangu marafiki, na yangu isimu
    Nikawataliki, wote kwa awamu
  11. Sasa sidiriki, hata skirimu
    Wanangu wa Piki, hawana kalamu
    Na walio wengi, wakosa stimu
  12. Nikidai haki, ananishutumu
    Papatu sitaki, lakini fahamu
    Talenga mikuki, ikinilazimu
  13. Zile shoki shoki,zanitia hamu
    Ewe mzanaki, siwe chakaramu
    Nipe yangu keki, nami binadamu

Maa salaam.

Kassim

Muamu!


Date: 28 Jul 2002

  1. Hayo siyashiki, Aah Ya Kasimu
    Wala siyataki, Ulonena humu
    Usinidhihaki, Amu nkutamu
  2. Ulomuashiki, Akakudhulumu
    Si kindakindaki, Mwenyewe wa Amu
    Hakustahiki, Usijilaumu
  3. Kuipiga ndiki, Kwataka nidhamu
    Panapo kisiki, Uwe ni timamu
    Ndipo humchoki, Na hakwishi hamu
  4. Yanini malaki, Hayo si muhimu
    Bora jimiliki, Na miko idumu
    Hukuvuwa dhiki, Ukatabasamu
  5. Hutaki fataki, Na washika zamu
    Wala mahandaki, Na wala mizimu
    Ilindayo haki, Ni yako maqamu
  6. Hebu nisadiki, Nnayafahamu
    Mie sishikiki, Na wangu Muamu
    Ni wangu rafiki, Rihi ya nasimu

Ahsanteni

Saleh

 

 

  About Us | Poems | Privacy Policy | Contact Us | ©2004 Zanzinet