|
|
Mvuvi
31 March, 2002
- Ndimi mvuvi halisi, kula vuvi nalijuwa
Nivuwaye mikambisi, na papa wenye khatuwa
Wala sivui vingisi, mishipi haisumbuwa
Nimekwambiya elewa
- Sivuwi bahari ndogo,hatia nanga fuoni
Havisimbika vigogo, vilivyozama majini
Na wala sivuwi ngogo, vidagaa na mbinini
Siwavui asilani
- Jabali hulijilisi, jishipi nikalitupa
Haotea mifulusi, na nguru na mijipapa
Si kasikazi si kusi, khabari yangu nakupa
Wala sivui kwa pupa
- Na nivuapo malema, huingia ndani ndani
Maji yangu ni ya pima, thalatha u thalathini
Na ndiyo ninayozama, lema halibwaga tini
Uliza mimi n'nani?
- Na nivuapo maziyo, mavuvi ya kizamani
Kwa hino hali niliyo, huvua kwa kutamani
Hatafuta kiteweyo, cha wali mwema kombeni
Haandaa siniani
- Ela uvuvi wa juya, kuvua siutamani
Sababuye takwambiya, ufahamiwe mwendani
Ni kwambakwe huingiya, samaki waso thamani
Kama wewe mwafulani
- Ni kuu yangu bahari, elewa sana elewa
Huko hakwendi Vihori, wala vyenu vimashuwa
Shoti nakhodha hodari, kisha ende kwa ngalawa
Na milango kuijuwa
Kutoka Malenga wa Mvita
Limeletwa na Maher Fundi
Mvuvi
03 April, 02
- Shairi limesukika, mjuzi hatosumbuka
Mvuvi wa kusifika, avua anapotaka
Havui vitakataka, samaki anayetaka.
- Kofia nakuvulia, na koja ninakuvika
Vibua waviachia, dagaa mwiko kushika
Simvuvi sinzia, ndio maana unawika.
- Beti tatu nachangia, kukupa heko sawia
Wengine wamo kulia, mbinu unazotumia
Waloweze kuwambia, nyayo zako kufatia.
wakatabahu
Hashil S. Hashil
Mvuvi
- Mvuvi na zako hila, kujisifu si wosia.
Mvuvi wacha papara, bahari si yako ndia.
Mvuvi unaokula, ni samaki wa bandia.
Nakwambia hujavua.
- Mvuvi huna haraka, kwa samaki walolala.
Mvuvi zamia sana, bahari za vina saba.
Mvuvi wavua koa, kwa huko hakuna kamba.
Hawana ladha wa huko.
- Mvuvi yako bahari, na milango kuijua.
Mvuvi yako nadhari, samaki kuwachagua.
Mvuvi huna habari, wengine si wakuliwa.
Wapevu wanuka vumba.
Walii Genderi.
Mvuvi
Date: 11 Apr 2002
- Mvuvi kutaharuki, Kwenye maji ufukweni
Mishipi haishikiki, Chambo hakionekani
Imekufika hilaki, Mvuvi wavua nini
-
Tambua hao samaki, Waishio baharini
Kuna dhofu walo dhiki, Wajao hata demani
Lakini kuna malaki, Kwao chambo si thamani
-
Mvuvi zako hamaki, Na maguvu muilini
Watwambia hawatoki, Watulia na yamini
Mbona kutahamaki, Wameshapenya nyavuni
-
Nakwambia usadiki, Uvuvi pia ni fani
Ujifunze umiliki, Maarifa kubaini
Kwanini huambiliki, Samaki hawi mwambani
-
Nisikize sidhihaki, Tutaonana mwakani
Papa chambo hakitaki, Aja mwenyewe chomboni
Kuvua kipande hiki, Wajisifu bandarini
A. Baja
Mvuvi
- Yarabi salama, leo ishapita.
Na jua lazama, tamaa nakata.
Mechoka tazama, macho yafukuta.
Mbona hajarudi,mvuvi matata.
- Sasa wiki moja, hajatuzukia.
Katoka kwa hoja, kwenda tuvulia.
Samaki wa haja, anaojilia.
Mbona hajarudi.
- Twemwambia zama, samaki si hao.
Watakuangama, vumba ndio lao.
Mbona hakuvuma, kwa kuwala hao.
Kenda vua wapi.
- Vihori havyendi, huko avuako
Nasi hatufiki, bahari za vumo.
Kina sikiwezi, nikaduru humo.
Mwenzetu kazama.
- Mpandao meli, tazameni huko.
Mvuvi habari, nyumbani hayupo.
Yu kwenye hatari, humo avuamo.
Bahari si lake shamba.
Walii Genderi.
N-GONGELE
Mvuvi
- Walii genderi, tua roho yako
Mvuvi mahiri, bado yungaliko
Ana yake siri, kwa huko aliko atarudi papo
- Ilikuwa kali, dharuba ya kusi
Ikangia vuli, hana wasiwasi
Alivua kweli, mapapa na ngisi
Poa roho basi
- Tarudi nyumbani, na mavuvi tele
Tena salimini, punguza kelele
Miye naamini, ana lake yule
Mso hili ana lile
- Siku ikifika, nitakukumbusha
Tena kwa hakika, nitakuamsha
Mvuvi kafika, tena kwa bashasha
Nyavu karejesha
Mbarouk
N.York
Mvuvi
28 April, 2002
Sie mvuvi wa pweza
- Mwenye kutaka kujuwa, huenda kwenye kiini
Ili apate elewa, kimekusudiwa nini
Haruki kwa kupotowa, bila kujuwa undani
Pandisha nguo tarowa, maji yapanda mwilini
Hayakupwi asilani
- Milango hujaijuwa, na dira za baharini
Nyota hukuzielewa, mekupoteza mwinani
Tafuta wanoelewa, wenye kuzama majini
Ndipo hapo utajuwa, siri ya uvuvi nini
Sirahisi asilani
- Uvuvi wako uzile, si samaki wa nyavuni
Hufiki maji kule, marefu si ya fuoni
Yakikupwa kachokole, chaza na pweza maweni
Si changu na kolekole, si samaki wa fukweni
Kiwataka baharini
Maher Fundi
Mvuvi kazama!!! (sikweli wajidanganya)
Date: 29 April, 2002
- Samaki uwavuao, wanishangaza mwenzangu
Samakio si mwambao, wala hungoji kiwingu
Kivulini ndio ngao, samaki wako wa changu
- Bahari uziendazo, ni za mbali kweli kweli
Moyoni unayo nguzo, samaki wako ni ghali
wewe huna matatizo, chumvi kwako si asali.
- Usemavyo ndio kweli, wendako huonekani
Waepuka na ajali, kwani wangia kizani
Ufanyayo ni halali, wabarizi barazani.
Hashil
|