|
|
Ndege wangu Kanitoka...
Date: 22 Jul 2002
- Namiminika machozi, ndege wangu kanitoka
Hadaa za mchuuzi, na posho za kila mwaka
Za mtama na mbaazi, na nyingi nyingi nafaka
Ndege wetu katutoka, hatunae mikononi.
- Toka kinda kamaizi, mithili panya na paka
Akinitega kwa uzi, mitego mpaka fyuka
Kila nilipobarizi, yeye alikwisha fika
Ndege wetu katutoka, hatunae asilani.
- Ninapata kisuunzi, ya kale nikikumbuka
Wakati tukila mbuzi, uhuru kushereheka
Akapanga mapinduzi, kwa mapanga na mashoka
Ndege wetu katutoka, hatunae abadani.
- Vidonda bado viwazi, ndipo alipotamka
Ndege nipe nimuenzi, wewe ndiye wangu kaka
Na ukifanya ajizi, tamuacha ataruka
Ndege wetu katutoka, hatunae amanani.
- Tawaondoa walinzi, wale wangu nilokupa
Niwaache majambazi, ulodhani wameng'oka
Wairudishe mizizi, ubaki kuhangaika
Ndege wetu katutoka, hatunae kataani.
- Kajifanya mfinyanzi, udongo akafundika
Akayafunga mapenzi, pingu zisizofunguka
Leo pataka hirizi, ndoa hii kudumuka
Ndege wetu katutoka, hatunae tunduni.
- Akavinjari komanzi, ndege wangu kumnyaka
Kawatia jinamizi, watetezi wa kichaka
Akaukata mzizi, vyama vikaunganika
Ndege wetu katutoka, hatunae milikini.
- Utamu wa maandazi, na makuku ya kupaka
Karubuni walowezi, upofu kuwagubika
Wasifanye yao kazi, ya ndege kumfunika
Ndege wetu katutoka, hatunae hatunani
- Sasa hatuna pumzi, ndege wetu kasharuka
Kufukuza hatuwezi, bahari kashavuuka
Hata tukipiga kwenzi, harudi kashatoroka
Ndege wetu katutoka, hatunae sikiani.
Maa salaam.
Kassim
Ndege wetu Katutoka...
Date: 22 Jul 2002
- Nimesikia yalokusibu, Hayajafika ya firauni
Unyago isiwe sababu, Kuubeza utamaduni
Kidegecho Kitaratibu, Kimeingia mwituni
Kimezipata zabibu, harudi tena tunduni
- Ulijilabu kwa mikogo, Yuwako uhmo ndani
Hilaki isio ndogo, Kumfungia bandani
Kidegecho sio mfugo, Chataka ruka angani
Kimezipata Zabaibu, Harudi n'go tunduni
- Japo kuwa ulikienzi, na kukipa kila raha
Kilikosa usingizi, tunduni chaona karaha
Kilijawa na simanzi, moyo ulijawa jaraha
Kimepata zabibu, hakirudi tena tunduni
- Takupa langu jawabu, Ndege kiumbe adhimu
hakitaki masharubu, Na ukali kama ndimu
Hukawii kuharibu, Sifa na zake isimu
Kimezipata zabibu, Harudi tena tunduni
- Ndege kazowea kuimba, Asubuhi na jioni
Wewe umekifunga kamba, Kihoi tunduni
Kakiokoa muumba, Na taabu za bandani
Ndege sasa chajingamba, Harudi tena tunduni.
Nduguyo
Eddie Masoud.
|