Vikuba Vilonukia!
Date: 20 Sep 2002
Viwapi vile vikuba, vilokuwa kinukia
Vilokitungwa kiriba, shingoni kining'inia
Kila kimwana kibeba, jioni ikiingia
Kikivaliwa kwa hubba, mume akafurahia
Usiku ukatimia
Vitalu vimeondoka, hakuna kilobakia
Wenyewe wametoroka, kwengine wamehamia
Waliko wajialika, kwa uturi kujitia
Moto nao waukoka, udi kujifukizia
Ndipo wanaponukia
Wamewaachia pumba, makapi ya vumbi lao
Wakifukiza ni vumba, harufu wanukiao
Wamo nao wajiwamba, wajihisi ndio wao
Kumbe mafusho wakomba, na udi hauko nao
Masikini roho zao
Maher
Vikuba vilonukia
Date: 23 Sep 2002
Sheikh Maher & wanaukumbi,
Vikuba uviulizavyo, viko kama kawaida
Haviuzwi ovyoovyo, wavipata kwenye shida
Ufahamu hivyo hivyo, wala sitaki ziada
Wamegubikwa na choyo, akili zao ni rada.
Vitalu bado tunavyo, majina yabadilika
Jela zaitwa mafunzo, ukingia waokoka
Wenyewe yao mawazo, wamebaki kumenyeka
Uturi kwao uwezo, paka mekoni acheka.
Waloacha hizo nyumba, ndani wakuta mitumba
Harufu kweli ya vumba, kama udongo wa shamba
Lilobaki ni kupamba, mapakacha na marimba
Wengine ngozi ya mamba, ukipita wakuimba.
Wakatabahu
Hashil