|
|
Yamenishinda Wenzangu!
Date: 12 Aug 2002
- Haya yaliyonikuta, sihadithi ni ya kweli
Nimarefu kuyaleta, kikubwa kitendawili
Siyakuomba kumkuta, kwa yeyote ile hali
Nauchungu nnajuta, kusema yote muhali
- Nilimgeuza ndege, tundu nikamjegeya
Hati ya mambo msige, jina memuandikiya
Kama yai kimuenge, kiogopa kuteleya
Singoji nyayo ikanyage, kimuekea zuliya
- Yamenishinda wenzangu, mazito kifikiriya
Hamupo pahala pangu, kwa dhati kuyahisiya
Ukweli ajua Mungu, alivyo kinitendeya
Kiniwacha peke yangu, nyumba kinielemeya
Maher
Yamenishinda Wenzangu!
Date: 13 Aug 2002
- Maher pole sana, kwa maafa yalokupata.
Tena nasikitika sana, kwa hayo yalokukuta.
Uchungu wake kifana, muasi huyo matata.
Vizuri ulivyofanya, kumpatia talaka.
- Mwanamke memuenzi, kwa kila analotaka.
Imanie jinamizi, moyo wake unawaka.
Hana hata simanzi, hisia kuzikokota.
Hurumae ibaidi, angalau kukupoza.
- Mke mwenye balaa, tamjua akipaa.
Maneno yake alaa?, uso umekurupaa.
Kumbe anaye balaa, mwenziwe wanayekaa.
Maher sitaharuk haya, kula na unywe murua.
- Sali kiomba na dua, Mola atakushushia.
Mabaya atakuvua, kheri atakuletea.
Inshaalla utatulia, kwa rehma za Jalia.
Ndoa utaifikia, na husda kukuondoshea.
CHAMA.
Zimenifika salaam
Date: 13 Aug 2002
- Salaam zimenifika, na wasia mepokeya
Bi Chama,tawajibika, kwa kila ulonambiya
Na yale memalizika, hakuna lilosaliya
Tatu zote memtweka, talaka haikubakiya
Kwaheri nimemwambiya
- Mfano wangu kizuka, nimo ndani nnatawa
Mwenzangu mie mkeka, sala ikiadhiniwa
Nafusi yafurahika, moyo wangu unapowa
Maudhi huniondoka, kila niombapo duwa
Namshukuru Moliwa
- Wakati utapofika, tatafuta ntaoa
Sasa sinayo haraka, nadondoa kama chua
Pupa,ntaghilibika, nisijuwe kuchaguwa
Nami muhimu silika, natabiyae kujuwa
Ndipo ntakapo powa
Maher
Yamenishinda Wenzangu!
Date: 14 Aug 2002
- Ni ajabu ilioje, vitimbi vya huyo mwana.
Vyote apewa vereje, ikawa hatulizana.
Auonapo uwembe, hujichinja kwa kuona.
Yuradhi apawe pombe, sumuye asoiona.
- Mke uliyemtunza, vizuri ukamuweka.
Leo aja kukutimba, kayda yake kidhaba.
Hii yaonesha kwamba, imani yake ni haba.
Na ukija kumkumba, pabaya atakuweka.
***************************
- Sura iliyo njema, husni tabia zake.
Dini imemsimama, twayib ahli zake.
Huyo ndie wa kusema, na kuarifiwa walid wake.
Starehe yenye neema, mke na uzuri wake.
- Mtume hakukosea, aliyoyasema kuwa.
Starehe ya dunia, mwema mwanamke oa.
Mwenye dini na hisia, huruma kukuonea.
Maher vumilia, huku ukizingatia.
CHAMA.
Yamenishinda Wenzangu!
Date: 15 Aug 2002
- Lau kama yu mkosa, asingeingia mtandaoni.
Akaelezea visa, vya aliyekuwa shetani.
Ambavyo vimemnasa, na kumkhasi moyoni.
Ingekuwa hivi sasa, atanua viwanjani.
- Kutunga kwake shairi, si kuonesha fahari.
Hadithi yake ya kweli, dukuduku lilo dhihiri.
Ataraji zenu kauli, kujipoza muhadhiri.
Siku zote neno zuri, huishinda sadaka yenye kiburi.
***************************
- Mwanamke huweza kuwa chanzo, cha mabaya na mazuri.
Na kwake yeye ni chambo, kwa yule mwenye uzuri.
endapo akenda kombo, mazuri hayatojiri.
Labda afate mkondo, wa dini ulo mzuri.
- Mwanamke ana vituko, vikubwa anavyofiili.
Na haya sio mashiko, bali ukweli kamili.
Vya sheitani ni vituko, ni dhaifu na dhalili.
Twayajua tokea huko, thibitisho la JALILI.
Chama.
|