.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Chemsa Bongo

 

 

 

 

 

 

Related links

Chemsha Bongo!

Date:  12 August 2003

  1. Parakacha yuko chini, meno matatu yangoka
    Aaga enda kazini, akutwa kwenye kichaka
    Kakamatwa anazini, mke wa mwana Mashaka.
  2. Tabia yake uoza, ya wenziwe kuchunguza
    Yake yamcheza, amungunya na kumeza
    Mgonjwa kupeleleza, nyendo ni za pweza.
  3. Sefu amani amuri, mafya matatu kuweka
    Pembua mwenye kiburi, chagua asomashaka
    Tafuta pia ayari, alobaki kumuweka.
  4. Komamanga alipenda, shokishoki nazo pia
    Matunda mengi apanda , mengine aagizia
    Popote utaporanda, jina lake ni shezia.
  5. Mapenzi moto kifuu, yatia watu wazimu
    Yakufanya ule fuu, uwe wino wa kalamu
    Wengine kichefuchefuu, kulinda nyumba kwa zamu.

 

Hashil S. Hashil

Chemsha Bongo!

Date:  13 August 2003

  1. Mso hili ana lile, hakuna alotimia
    Hayo yake maumbile, sisi sote twayajua
    Usipige makelele, utaumiza kifua
    Chuwa mezidi mchele, Vipi utazidondoa?
  2. Kiumbe huyo mzito, kuishi nae udhia
    Huchemkwa na vukuto, ya watu kuyachungua
    Kakaa kama mtoto, ni bora kumwachia
    Atapewa mkong'oto, na mwalimu dunia
  3. Ngoma ikivuma sana, kupasuka ni dakika
    Wangapi tulowaona, Vyeo wakijipachika?
    Kijifanya maulana, na watu kiwatundika
    Leo wametoka maana, wapita wafedheheka

 

Said Paul

Chemsha Bongo!

Date:  13 August 2003

  1. Hakuna kilichozidi, chumvi waweka mwenyewe
    Wafanyao magaidi, mbinu zao ni za mwewe
    Hutoa wao miadi, chuwa wewe uzitowe
    Hayo kwao ni ya jadi, migombe isowenyewe.
  2. Kiumbe sio mzito, upekepeke mtamu
    Mwishowe huwa majuto, sukari geuka sumu
    Jiji huliwasha moto, wengine kuwapa pumu
    Watu wazima watoto, zote hizo ni awamu.
  3. Avumae baharini, twaambiwa papa
    Avumae majumbani, asomjua Mkapa
    Avumae majiani, umma anaye wachapa
    Avumae duniani, ni Bush kutapatapa.

 

Hashil S. Hashil

Chemsha Bongo!

Date:  13 August 2003

  1. Ya kweli uliyonena, na kasoro siioni
    umenena yalo mboni, ajuae ameona
    walikuwa juu sana, hawatuulizi sini
    Leo hii hawanani, wamebakia kulana.

 

John Smith

Chemsha Bongo!

Date:  14 August 2003

  1. Leo nitakupa kisa, uwaelewe viumbe
    Hii ni kweli kabisa, si uongo hata chembe
    Wawili katika tisa, Ni wanyama waso pembe
    Wamikia kutikisa, Niache leo niambe
  2. Nuhu Mtume wa Mungu, alikimbia gharika
    Akayafuata mawingu, akafika pakufika
    Akasema mlo wangu, njoo tuweni shirika
    Kwani wetu ulimwengu, leo utabadilika
  3. Nanga walipoituwa, maskani walitaka
    Kujisitiri mvuwa, Ikabidi kuezeka
    Yale asiyoyajuwa, maombi akapeleka
    Uwa aje kujengewa, Wapate kustirika
  4. Mafundi aliwapata, bila tabu na mashaka
    Kilichompa utata, pale walipotamka
    Binti yake kashata, mshahara walotaka
    Nae bila ya kusita, Naam akaitika
  5. Wake mmoja binti, wote amewaahidi
    Akayapiga magoti, kuongea na Wadudi
    Najua kwako sitoti, Nimeshaweka ahadi
    Kwangu wewe mlingoti, kurejea sina budi
  6. Mafundi walipongia, haki yao kuchukua
    Chui na pundamilia, Kwa uwezo wa Jalia
    Mabanati walikua, pasi kitu kupungua
    Naye Mtume Nabia, Ndoa akawasomea
  7. Elewa sasa kwanini, watu wote sio sawa
    Wengine ni hayawani, Chanzo chao kilikuwa
    Wawenda ndani kwa ndani, kama mwasho wa chawa
    Umshukuru Manani, kundi hilo kukutowa
  8. Taratibu ndio mwendo, mwenda pole hajikwai
    Mambo sio kwa vishindo, pupa nayo haifai
    Sharti uwe na miundo, Sio tu kujidai
    Muwa ukizidi fundo, Mlaji huukinai.

 

Said Paul

Chemsha Bongo!

Date:  14 August 2003

  1. Kuna kiumbe Kijiwe, jina lak Barzanji
    Kazi yake ni mayowe, kujifanya yeye jaji
    Akilala ni kiwewe, akumbuka mauwaji.
  2. Mwengine Ame wa Pandu, mwendo wake ni wa tandu
    Makali yake ya mndu, watu hawamuhusudu
    Shepu yake ni ya ladu, ..........................
  3. Mengi tunayoambiwa, Amani kafilisika
    Kaeni mukichunguwa, mtindi autandika
    Mtuno wa kitumbuwa, wamuona watapika.
  4. Mkapa aenda kapa, daraja jina kujipa
    Lipumba anamchapa, kukumbukwa kama papa
    Kabakia tapatapa, wapinzani wameapa.
  5. Mwendo wa kobe haraka, kinyonga asingiziwa
    Mke ataka talaka, ndowa asozitambuwa
    Kazi kutupa mashaka, jambo hili kulijuwa.

 

Hashil S. Hashil

Chemsha Bongo!

Date:  15 August 2003

  1. Mvuvi nyavu karusha, zikazama baharini
    Akangoja anakesha, mara aitwa majini
    Afuta kanasa kasha, kufunguwa yumo jini
    Kaanza kujichekesha, akamla kwa huzuni.
  2. Kisa cha pili porini, mnyama anaesema
    Paa kutwa analani, viumbe wasohuruma
    Mabunduki vichakani, nyuso zao kama chuma
    Kwetu sisi visirani, watusaka wale nyama.
  3. Mtoto amezaliwa, kila dakika akua
    Mdomo wake wa njiwa, wangara kuliko jua
    Wazazi wakauguwa, waganga wakatambua
    Muumba awazinduwa, kukumbuka wasojua.
  4. Kwenda mbio sikufika, kiumbe anza gutuka
    Uendako utafika, wasia huo futika
    Kinyonga anasifika, hakuna anomshika.
    Dunia yatikisika, wamfata watapika.
  5. Miujiza ufukweni, simba kichwa cha samaki
    Akapelekwa sokoni, kila mtu hamtaki
    Akachomoza chetani, bei akatoa laki
    Kamchukuwa mwituni, akageuka bunduki.
  6. Ladha haielezeki, kwa maneno kueleza
    Itakufika hilaki, hata wasema wacheza
    =20 Kitu hicho hukiweki, chabaki harufu chenza
    Ni mshindo wa fataki, wabaki kusikiliza.
  7. Vuta nkuvute, vyama viwili vikubwa
    CCM iwe pute, CUF izidi kukuwa
    Chakufanya tuwe sote, udhalimu kuungowa
    Kijiwe kiwe cha wote, Muungano kuutuwa.
  8. Hakuna shida milele, tukipania kikweli
    Tuyawache makelele, tupendane kweli kweli
    Debe shinda jaza tele, mwenzio mpe ukweli
    Tuyafukie ya kale, imani siyo ukali.

 

Hashil S. Hashil

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet