.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Chombo Chaenda Mrama

 

 

 

 

 

 

Related links

Chombo Chaenda Mrama!

Date:  13 Feb 2003

  1. Naingia mitamboni, nazimwaga zangu beti
    Nitoe yangu maoni, juu ya Zanzineti
    Ya kuikaza demani, na kuziba kalafati
    Chombo kiende sawia.
  2. Miaka ya tisiini, watu wakajizatiti
    Kukitoa chelezoni, chombo hichi madhubuti
    Wakakitia majini, kwa faida ya umati
    Zanzibari wote pia.
  3. Azma yao makini, siyopitwa na wakati
    Kwamba na sisi jamani, inatupasa kuketi
    Kujadili kwa undani, ya Kojani na Kidoti
    Kwa faida ya jamia.
  4. Yatokeayo nchini, pakawekwa mkakati
    Kuyaleta ukumbini, ya ndani ya magazeti
    Na yale ya mitaani, pasipo na vizingiti
    Sote tupate sikia.
  5. Yakaletwa barazani, yakatipwa kitikiti
    Ya akina Salmini, na Baucha Marikiti
    Ya ndwele za matumboni, ya uhai na mauti
    Ya huzuni na ya kufurahia.
  6. Wazawa wa Visiwani, tukapaaza sauti
    Kuyasemeya kwa kani, tena bila ati ati
    Yaliyojiri nyumbani, tukayakazia nati
    Ya ratili na wakia.
  7. Tukifanya tathmini, kwenye yetu jamaati
    Wako wanaoamini, wima tunapiga buti
    Hatwendi tena usoni, twaliharibu busati
    Mchele mezidi chuwa.
  8. Sababu yao yakini, migogoro haisiti
    Habari za duniani, ndizo zilizo furuti
    Zile za kwetu Mwambani, sasa zimekuwa seti
    Malengo yanapotea.
  9. Wakikumbuka zamani, mwanzoni mwa hii neti
    Michango ya kila fani, wala sio tashtiti
    Ililetwa uwanjani, kwa mabunda na madoti
    Mengi tukizingatia.
  10. Makala za ugenini, zenye uzuri wa hati
    Mantiki hazilingani, macho yao hazivuti
    Wajumbe wanatamani, maneno kama boriti
    Mazima na yenye siha.
  11. Tulipo ndugu zanguni, yafaa kupiga goti
    Tutafakari kwa shani, magamba na mitikati
    Tusibakie kughani, yalaiti yalaiti
    Chombo chaende mrama.

 

Kassim O. Ali

 

Limetumwa tena ukumbini na Maher

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet