.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Fitina

 

Related links

Fitina!

Date:  16 Oct 2003

  1. Fitina mtu khatari, siwezi kukhadithia
    Mzushi hana nadhari, mjasusi wa kuzua
    Anuka kama jodari, papa bovu la India
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  2. Fitina hana jeuri, usoni huchekelea
    Hudai hana kiburi, laghai kunyenyekea
    Hujifanya yu tayari, kitini kukwinukia
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  3. Fitina mtu ayari, heshi kukutembelea
    Si mwema na si mzuri, hakai akatulia
    Upole akuvinjari, apate kukuzulia
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  4. Fitina mfano ngiri, heshima hajatambua
    Domo halitaghairi, kutoa yasio njia
    Hata awe mshairi, fitina wote sawia
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  5. Fitina hana bahiri, maneno kupangilia
    Fitina hana dosari, zaidi ya laki mia
    Fitina katika pori, hukaa akangojea
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  6. Fitina si urafiki, ni utovu wa tabia
    Halimukhusu fikiri, kwa nini kushikilia
    Na kufanya dhamiri, kukaa kusimulia
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  7. Fitina khasa kafiri, karibu mwenye kuua
    Huzikusanya khabari, kila pembe ya dunia
    Uulizapo hakiri, adui wa watu pia
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  8. Fitina leo kariri, usome ukirudia
    Ndoa ikisha shamiri, huwezi kuitangua
    Ila atake Kahari, wakati ukiwadia
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

  9. Fitina hii nadhiri, siku moja tatimia
    kugundua ikijiri, kifungo nitachukua
    Fitina hata tajiri, ras yake taitoa
    Fitina mvunja mji, umwonapo tahadhari.

 

Eye Witness

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet