|
|
IWEJE UWE WA TATU?
Date: 12 May, 2003
- YA RABBY YA RAHMANY,NAANZA KWAKO MWENYEZI
YA RABBY YA MUAWINY,KHERI ZAKO NIZIENZI
YA RABBY YA MUFARIJANY,MUYASOME KWA MAKINI.
- Wewe sie mpangaji, ya watu kuwapangia
Wewe sie mfunzaji, kidole kutunyoshea
Najua yako juhudi, kwanini ukaumia
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Pima ukizingatia, kweli yanaelekea?
Vibaya kumkalia, mwenzio mwana sikia
Wapita kila kijia, husuda kumtilia
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Mola Jalla wa Azza, akujazi ewe mja
baya kutufanyiza, kisimacho nawe chaja
Wataka kwako kujaza, kwa mwenzio kukufuja
Iweje uwe wa tatu,kutaka kutufitini?
- Ni bure unaumia, huna njema yako nia
Wallahi nakuapia, na sala nakusalia
Na mwenye kukusudia, baya kulisimamia
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Isilamu wajigamba, mbona baya hukatazi
Usimkae sambamba, mwenzio ana Mwenyezi
Alotukuka Muumba, kaniongoza kwa ngazi
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Tumeamua wenyetu, tena kwa hiari yetu
Yanopita kati yetu, ni siri baina yetu
Sijasikiapo katu, mke kuwa na watatu
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
-
Hebu soma historia, za waliotangulia
Zama za ujahilia, zilipowatawalia
Na ghafula kufikia, Amiri kutarajiwa
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Mimi nilivyofundishwa, chuoni na kwa malezi
Isilamu muepusha, baya lisimtelezi
Kheri zote kumvisha, kipata usimuudhi
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Lakuuma la jamali, alilopata mwenzio
Unatia na kejeli, ya nini dharau hio
Unajifanya mkweli, Kama baya kwako sio
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Unajifanya jabari, sio sifa yako hiyo
Lakini nakusaili, mimi si mke mwenzio
Nimefundishwa kauli, nzuri kuongea nao
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
- Sitobishana kwa hili, nakueleza yaliyo
Mikono hii miwili, uu kielekea kwayo
Namuomba ya KAHARI, akuondolee CHOYO
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini.
- Sisi tunaye MUUMBA, Inshaallah tatuongoza
Yako uliyoyakumba, gizani ulikofunzwa
Shuhuda wa hii nyumba, shahidi wataongoza
Iweje uwe wa tatu, kutaka kutufitini?
SALMA KHAMIS.
|