.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Linanukiya Miyaka

 

Related links

Linanukiya Miyaka

Date: 18 March, 2003

  1. Najuwa unaniona, ni mbele machoni mwako
    Si mbali,karibu sana,ni kope na mboni zako
    Nami sina la kunena, nakusikiya uliko
    Ukitaja langu jina, naitika huko huko


  2. Kikohowa nashituka, haraka hukuitika
    Roho ikashugulika, kujuwa nini wataka
    Wasi wasi hunishika, moyo hunipaparika
    Mbio nikakurupuka, vyumbani ingiya toka


  3. Fahamu zangu huruka, zikirudi nikacheka
    Kuwa nnahangaika, nawe hupo kwa hakika
    Chako kimenifunika, kivuli menitandika
    Sina nnachokumbuka, ila wewe sina shaka


  4. Huwa nawe kisinziya, ubavuni chini yako
    Mikono hukuwekeya, kipakata kichwa chako
    Ukawa wanilekeya, nami haeleka kwako
    Huku nikikubembeya, ulale kwa raha zako


  5. Ni ndoto iliyo refu, iso mwisho na mpaka
    Yenye masafa marefu, tusoweza kuyafika
    Si jambo kuwa halafu, litaweza kamilika
    Ni huba lenye harufu, linonukiya miyaka


  6. Usikae ukaliya, wala ukasikitika
    Nafahamu waumiya, roho yako inalika
    Ilo bora Vumiliya, yetu siku itafika
    Wakati ukiwadiya, kwa shangwe tafurahika


  7. Yako yananiunguza, machozi yakikutoka
    Huyahisi kichuruza, tone tone kidondoka
    Ya moto nikiyapoza, kifuani kibabuka
    Usione menyamaza, nakwisha namalizika

Maher

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet