.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Naitamani Sauti

 

 

 

 

 

 

Related links

Naitamani Sauti!

Date:  09 Feb 2003

  1. Ndege uliye angani, Kiringia hewani
    Sauti yenye kughani, inaponitoa ndani
    Nikaapo dirishani, Isishe nnatamani.
  2. Urukapo kwa madaha, asubuhi na jioni
    Sauti yenye furaha, hupita masikioni
    Nami huona raha, isimalize natamani.
  3. Napenda yako sauti, aliyokupa Manani
    Nami nikaja kititi, kubaini yako shani
    Mola kakupa sauti, nzuri naitamani.
  4. Ndege wanibembeleza, asubuhi na jioni
    Nami sina cha kuwaza, Nikuonapo waghani
    Sauti huniliwaza, Kunitoa majonzini.
  5. Ndege nakuomba pita, jioni imewasili
    Mazuri yakufuata, Sauti meisabili
    Mikono imefungata, mtama wakusubiri.
  6. Moyo meingiwa wahka, njoo mbawa zako mbili
    Hakuna ataekupa, Mazuri nakusaili
    Kubwa ndani kukufunga, nje uione mbali
    Usiwe na mhimili.
  7. Ushindwe pa kupapasa, mti uuone mbali
    Urudi ninakuasa, Tizama yaliyo mbali
    M-baya akikunasa, atakukata kilimi
    Usiweze na kughani.
  8. Ndege meumbiwa anga, Utandie na ughani
    Usiwe ndege kubanga, alojitoa thamani
    Akashindwa ya kupanga, akaleta tafrani.
  9. Ndege uliye adhimu, Sauti yako ni tamu
    Asubuhi wasalimu, Jioni nayo timamu
    Umeumbwa na KARIMU, Sifa usiituhumu
    Sauti yako ni tamu, Njoo unikirimu.
  10. Imba unipe raha, na uruke kwa furaha
    Macho yenye madaha, yakuangaze kwa raha
    Moyo mejawa furaha, Natamani zako raha.
  11. Njoo unipe furaha, Kwa sauti ya madaha
    niokoe na fadhaa, Dirisha nilipokaa
    Kimya chako si ridhaa, Na si yako khulka.
  12. Au kama mekosea, Sina budi kukwambia
    Samahani ipokea, Moyo wako ufumbua
    Ndege unayeenziwa, Au Hajj umekuwa?
    Umenipa mazowea, Nashindwa kujitambua.
  13. Sauti yako ni neema, ni dua kwa masikini
    Asubuhi ukinena, Mchana nauthamini
    Jioni ukiitema, Kwa nyimbo zenye thamani.
  14. Sili nisipokuona, Ukirukia angani
    Moyo unasonona, Sauti naitamani
    Ndege ninakutamani, Sinitie hamkani
    Nipo hapa dirishani, macho kiangaza hewani.

 

Chama

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet