.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Nakutamani Mwandani

 

Related links

NAKUTAMANI MWANDANI

Date: 18 March, 2003

  1. Hadhira ninaijuza, kwa yote niliyofunzwa.
    Mapenzi niloyakuza, mwandani kumliwaza.
    Ni pekee nayatunza, yako nimeyatukuza.


  2. Yangu ya ndani fuadi, naahidi takuenzi.
    Mapenzi yaloshtadi, si kwa sababu simanzi.
    Lisanio meshadidi, nyamae nzuri azizi.


  3. Mwandani ulo wa ndani, wangu ninakutamani.
    Baidi yako hanini, nakupenda niamini.
    si yeyote insani, aliyekuzidi mwandani.


  4. Mapenzi yako mwandani, yanaishinda asali.
    Mapenzi yenye imani, thabit tena ya kweli.
    Mpenzi nakutamani, kwa yeyote ile hali.


  5. Nashindwa kujitambua, Nashindwa kuvumilia.
    Natafuta kila njia, Ridhaa kuifikia.
    Tafrani nimekuwa*azizi nakuhitajia.


  6. Natamani ya mwandani, Naumia kwa mwandani.
    Ungefungua moyoni, ukaona tathmini.
    Kwa ninavyokuthamini, Nakutamani mwandani.


  7. Mwandani usinikhini, nakuomba niamini.
    Umuamini Manani, Nakulia na yamini.
    Ni kubwa yako thamani, hakika nakuthamini.


  8.          Pokea hii zawadi.
             Wengi hawaifaidi.
             Nyoyo zao hufisidi.
             Na chuki zao huzidi.

    Waitafuta kwa dhati, Na kwa miguu ya futi.
             lakini hawaipati.

SALMA.


NAKUTAMANI MWANDANI(JIBU)

Date: 18 March, 2003

  1. Mwenzetu ulivyorowa, chapachapa hujiwezi
    Mapenzi yakukongowa, umekonda kama uzi
    Dawa yakukuokowa, kumsahau mpenzi.


  2. Mapenzi yakitoweka, kuyarejesha udhia
    Hugeuki malaika, kazi kiguu na njia
    Pakucheka watapika, ndani kwa ndani walia.


  3. Huwi wewe ni wa kwanza, wengi wameangamia
    Gonjwa mapenzi lameza, lakuchoma kishazia
    Lilobaki kujikaza, mwishowe lakuwachia.

Hashil

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet