|
|
Ndege Unayetafutwa
Date: 28 Jan, 2003
- Ewe ulobahatika, ndege uliye hewani
Unopita ukiruka, na kuranda mitaani
Mwenzio ahangaika, aparamia mitini
Fanya urudi haraka, zikuone zake mboni
- Fani yako memponza, memuathiri moyoni
Dunia kaimaliza, kwa wengine hulingani
Na sasa wamuumiza,'akutaka,hakuoni
Jaribu utavyoweza, ungie mwake tunduni
- Fuadi kitanda chako, yeye kakutandikiya
Kifua ndicho tandiko, chake kakuzawadiya
Mwengine kwake hayuko, wewe mekusabiliya
Wafanya nini uliko?, hwendi ukamridhiya
- Lau moja mevunjika, ya pili mbawa rukiya
Ano'itwa huitika, labeka huitikiya
Huwa hafanyi dhihaka, huenenda kisikiya
Nawe jihimu shituka, ushike wangu wasiya
- Bahati mekugongeya, iko pako mlangoni
Sioni cha kungojeya, na kuchelewa njiani
Naona waichezeya, shilingi yako chooni
Ikangia mepoteya, ndio basi huioni
Maher Fundi
|