.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Ninani Dhaifu Miye

 

 

 

 

 

 

Related links

Ninani Dhaifu Miye!

Date:  26 Feb 2003

  1. Bismillahi Wadudi, Allahu Rabbi Khaliki
    Kwa haki nakuhimidi, Allahu hugawanyiki
    Umpweke u Wahidi, huna haja huna dhiki
    Ewe Mola Mutaali, pokea ungamo hili.
  2. Ninani dhaifu miye, sijiwezi sijishiki
    Ninani hakiri miye, sitoi na similiki
    Ninani fakiri miye, sina kile sina hiki
    Ewe Mola Mutaali, sikiza ungamo hili.
  3. Sikiza ungamo hili, kama ni yangu laiki
    Hizingatia mawili, ya mimi nawe Khaliki
    Nakiri huna wa pili, U Pweke Mola Maliki
    Ewe Mola wa Ukwasi, pokea ungamo hili.
  4. Naungama takiraba, haja kwangu imesaki
    Rabbi Bwana wa Qaaba, mja nimejaa dhiki
    Bila Wewe sina heba, maadumu makhuluki
    Ewe Jallahu Jalali, sikiza ungamo hili.
  5. Nimedhoofu nafusi, inanichoma mikuki
    Vipi mja nakuasi, kwendekeza uzandiki
    Kama si Kwako Quddusi, kwa nani kuso mfaki?
    Ewe Rabbana Rahimu, pokea ungamo hili.
  6. Najidhalilisha Kwako, Ya Rabbi Mstahiki
    Ninanyenyekea Kwako, Ya Rabbi Dhati ya Haki
    Kila kiumbe ni Chako, Ya rabbi unomiliki
    Ewe Qadiru Qahari, sikiza ungamo hili.
  7. Mja kamwe hafanani, hata hafananishiki
    Na dhati yako Manani, hata halinganishiki
    Hutaniacha njiani, si kufu yako Razzaki
    Ewe Mola wa Ukwasi, pokea ungamo hili.

 

Ahmed Rashid

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet