|
|
UJANA
Date: 06 May, 2003
- Ujana kitu kitamu, tena ni azizi sana
Maungoni mwangu humu, nilikuwa nao jana
Kwa wingi katika damu, tahamaki leo sina!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Kichwa kimejaa mvi, kinywani meno hamna
Nikenda kama mlevi, miguu nguvu haina
Kumbe ujana ni hivi, ukenda hauji tena!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Jua langu limekuchwa, na nyota nilizoona
Ukinitizama kichwa, nywele nyeusi hakina
Kama zilizofikichwa,zikang'olewa mashina
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Natatizika kauli, midomo najitafuna
Nimekusanya adili, walakini hali sina
Dunia kitu bahili, hiki una kile huna!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Nilikuwa ni waridi, furaha ya wasichana
Neno hawakunirudi, wakati wa kukutana
Sasa nanuka baridi, wanionapo waguna
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Walio wakinibusu, walikuwa wengi sana
Wanawake wenye busu, uzuri na usichana
Sasa sina hata nusu, ya wanitajao jina
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Wazuri wenye uturi, na mikono yenye hina
Kila mtu mashuhuri, alipenda kuniona
Nilifaa kwa shauri, na sasa sauti sina
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Dunia bibi arusi, kwa watu kila namna
Inapendeza nafsi, wakati wa kuiona
Na leo sina nafasi, kwa uzee kunibana
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Kilichokuwa gizani, niliweza kukionap
Nikakijua thamani, sura yake hata jina
Sasa sijui ni nini, hata ikiwa mchana
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Kilichotaka fikira, niliweza kukinena
Kwa mfano na kwa sura, mpaka kikafanana
Leo tazama hasara, nguvu hiyo sina tena
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Kilichotaka mapimo, sikifahamu mapana
Marefu yake na kimo, siifahamu bayana
Nusu nimo nusu simo, duniani najionap
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Hadumu nasikitika, rafiki yangu ujana
Machozi yamiminika, na la kutenda hapana
Ni wakati umefika, uzee dawa hauna
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Hauna dawa uzee, mabega yamepetana
Anionaye ni"wee!, ondoka hapa laana"
Wanaposema na miye, niliyekuwa na jina!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
- Wakatabahu shairi, uchungu wanitafuna
Walakini nafikiri, twafuata Subuhana
Katika ile amri, ya"kuwa"na "kutengana"
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana
Shairi la Shaaban Robert
Limeletwa na Maher
|