|
|
Binaadamu Bora Mimi
Date: 16 May 2004
Wana-Zanzinet na Wapenzi wa Mashairi,
Assalaam alaykum.
- Boramimi bin'adamu, napenda jiweka kati
Na kutukuza isimu, yangu bila ati ati Na kujiona muhimu, wengine wote makuti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Na ile yangu kaumu, taisomea kunuti
Ibariki na kudumu, kuishinda Imarati Ndiyo jamii adhimu, taibeba kitikiti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Kila ninapostakimu, ninachunguza kwa chati
Ni nani mwenye kukimu, wa mali na nyingi noti Nani mwingi wa elimu, nani mbovu wa goti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Nitatafuta kwa hamu, wasifu na zao nyeti
Mali mwenye kuhizimu, tamheshimu kwa dhati Ama akinidhulumu, tamchomea baruti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Mwenye nguvu taheshimu, lakini tajizatiti
Na hata kama sitimu, urefu wa tatu futi Hilo halijawa gumu, taongezea majiti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Kijaaliwa fahamu, nikasoma darasati
Ninajiona mwalimu, mjuzi wa kila hati Wengine wote mabomu, tawakanyaga kwa buti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Na yule alonisumu, katu sitomsaliti
Tamuenzi mahmumu, yeye wangu mwanasiti Yeye ndie muadhamu, sitofanya tashtiti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Tamuenzi nimchumu, hata kama simpati
Sifaze tatarakimu, pasi kukosa wakati Tamwandalia karamu, nimpe na yangu voti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Hata wengi kilaumu, swahibuyo afiriti
Ndipo nitapoazimu, kumjaza kalafati Katu hamnikhasimu, na huyu wangu banati Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Lakini nisomhamu, katika huu umati
Hata akijaza fomu, awe wangu hazarati Tatamani mpa sumu, yamfikie mauti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Wewe mwana wa Adamu, wabweka wala hujuti
Waabudu ya nujumu, na ubinafsi huwati Humchi Mola Karimu, hadi uwe makhtuti Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Mezoea kuhukumu, na kuzigawa jamati
Uyaonayo matamu, yatafikia tamati Ndipo itapolazimu, safari bila tiketi Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
- Niliyotongoa humu, si sera si mikakati
Si hoja wangu wa damu, kuafiki zangu beti Ninaibwaga kalamu, sasa nakwenda kuketi Udhaifu mtikati, boramimi bin'adamu
Maa salaam. Kassim
|