.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

KINU KIMEVUNJIKA

 

Related links

 

KINU KIMEVUNJIKA

Date: 13 November, 2004

  1. Ndugu zangu sikieni, ninatafuta shauri,
    Wataalamu changieni, mniepushie shari,
    Wenye Elimu ya dini, na hata madakitari,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

  2. Nina nafaka ghalani, za mahindi na mpunga,
    Na nyingi ziko shambani, katika vyangu viunga,
    Ninahitaji maoni, mnaojua kutunga,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

  3. Ni mgumu si laini, hivi leo umepinda,
    Sijui nifanye nini, mchi wangu naupenda,
    Nitumie mbinu gani, kwa upya nikauunda,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

  4. Tatizo hili ni geni, halikuanza zamani,
    Na kinu hiki si duni, ni changu hapa nyumbani,
    Natwangia kwa makini, asubuhi na jioni,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

  5. Kinu hiki kina nini, au tatizo ni mchi,
    Ni njama yake jirani, nikamkatie pochi,
    Kutwanga ninatamani, hilo mimi siwafichi,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

  6. Maji kidogo kinuni, kutwanga kuwe rahisi,
    Tatizo lake ni nini, nimepatwa wasiwasi,
    Au hili jini gani, au ni yule chunusi,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

  7. Shime shime wa jamani, mnijibu kwa makini,
    Mazao yalo ghalani, kutwanga ninatamani,
    Mniondolee soni, nirudishie imani,
    Kinu kimevunja mchi, kutwanga hakutwangiki!!

Shairi la Mwanakijiji
Limeletwa na Walii Genderi.

 

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet