|
|
Kuandika
Date: 27 April 2004
-
Uandishi una meno, wataka nyingi hikima
Usanifu wa mikono, umahiri uso kima
Ustadi wa maneno, na msamiati mwema
Uandishi ni sanaa!
- Uandishi ni hazina, haipatikani bure
Hii ni bahari pana, si bakuli la kaure
Wavuao wakavuna, sio wavuvi uchwere
Ni wajuzi wa sifa!
- Kuandika ukasibu, uliyonayo moyoni
Wakakiri masahibu, na vijana viamboni
Ni kama vile zabibu, zilizoiva mtini
Zimetunzwa zikapea!
- Andikeni kwa muala, vifungu hadi vituo
Yapangeni masuala, kwa makara na mapeo
Sio kama majalala, yakaja kwa mkupuo
Bila ya kuongozana!
- Hata hivyo nawaasa, uandishi una hulka
Kitokea kudodosa, kalamu ikakutoka
Vyema kukiri makosa, kuliko kuaibika
Kwa kutaka kubishana!
- Muandishi muungwana, hafanikiwi kwa ngumi
Huandika yenye maana, pasi nyanyua ulimi
Sadifu kuwa mwanana, mahakimu ni wasomi
Wasomi na jamii pia!
- Siwachoshe bobo yangu, vidole ninavitua
Namuomba mola wangu, anipe kubwa hatua
Nijue ya Ulimwengu, na mbinu za kutongoa
Mbinu na kauli thabit!
- Rabi nijaalie mimi, na kila mwenye kusoma
Tuondolee vichomi, tuandike yalo mema
Rabi zidni ilmi, warzukna fahama
Aaamin!
Kassim O. Ali
|