.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

KIMEPOTEA MACHONI

 

Related links

KIMEPOTEA MACHONI

Date: 26 September, 2004

  1. Lau kuwa ni adimu, kitu nikakitafuta
    Mapema nikafahamu, kilipo nikakifata
    Ikatoka yangu hamu, nnachotaka kupata
    Au nikangoja zamu, ikafika sijajuta

  2. Kimenitoka machoni, mbali na upeo wangu
    Naangaza sikioni, hakipo,simbele yangu
    Kimenifunga moyoni, kwa dhana ati ni changu
    Sinacho nifanye nini, nawauliza wenzangu

  3. Kimeibiwa mchana, kweupe nje pepepe
    Hakuna kino fanana, mfano wake niwape
    Naogopa raha sina, alo kiba asitupe
    Kikaokotwa na wana, nikabakia mweupe

Maher Fundi(Unique)

KIMEPOTEA MACHONI

Date: 27 September, 2004

  1. Utulize moyo wako, kilicho chako ni chako
    Sijitie sumbuiko, kuutesa moyo wako
    Madhali ni haki yako, kilipo tarudi kwako
    Halijawa sokomoko, lihifadhi chozi lako.

  2. Konde upige mtima, kisicho chake si chake
    Ngangari wima simama, sijali papara zake
    Haki hutwawa nzima, simwombe haki si yake
    Halijawa sokomoko, lihifadhi chozi lako.

  3. Kingakutoka mbonini, visivyo ndivyo vilivyo
    Ni shari ungaidhani, sivyo ni kheri ilivyo
    Asau ya Rahmani, subiri itakiwavyo
    Halijawa sokomoko, lihifadhi chozi lako.

Ahmed Rashid

KIMEPOTEA MACHONI

Date: 28 September, 2004

  1. Unakitafuta nini, na kitu kimikononi
    Humuhitaji jirani, unacho na kimo ndani
    Kishafahamu yakini, siingiwe na huzuni
    Si wawakili baini, ni mapenzi ya moyoni

  2. Jitokeze uwanjani, kikuone hadharani
    Karata zimchezoni, kwako huna mshindani
    Turufu ividoleni, kubwa khofu yako nini?
    Itupe ujiamini, ushashinda si utani

Sayed Al Mugheiry

KIMEPOTEA MACHONI

Date: 28 September, 2004

  1. Kitandawili kipevu, kukitanzuwa vigumu
    Usiwe huo ni wivu, matunda yake ni pummu
    Jaribu kuwa mwerevu, penye raha pana sumu
    Kuwa wewe mtulivu, subira kweli ni ngumu.

  2. Utafutacho hakipo, usiku kwako mchana
    Uvumao ni upepo, wafananisha wa jana
    Hebu mchunguze popo, nyendo zake zina maana
    Chunguza kwanza ulipo, huku wakusanya zana.

  3. Aloiba msichana, wala hatowapa wana
    Kama kwake kina mana, atakienzi mnana
    Usikae unadhana, mtafute kwa adhana
    Tulia huku wabana, huo ndio uugwana.

Hashil S. Hashil

KIMEPOTEA MACHONI

Date: 28 September, 2004

  1. Changamoto umepewa, ipokee tafadhali
    Turufu yako kutowa, afadhaike afeli
    Uweze kumkongowa, abwetuke kidhalili
    Halijawa sokomoko, lihifadhi chozi lako.

  2. Ngoma yataka matao, werevu si ujahili
    Sawa patasi na mbao, kung'arishana wawili
    Mbona ekushinda bao, akakutoka wa pili?
    Halijawa sokomoko, lihifadhi chozi lako.

  3. Maheri Bwana pulika, jina lako litasibu
    Dagaa hapewi paka, kulinda ni masaibu
    Mwenyewe hukuyataka? kukusaliti muhibu?
    Halijawa sokomoko, lihifadhi chozi lako.

Ahmed Rashid.

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet