.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Laiti Siwele Nyuni

 

 

 

 

 

 

Related links

 

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  12 March 2004

  1. Laiti ! siwele nyuni, haruka haja uliko
    Tukangia faraghani, hapungua sikitiko
    Hakupa yangu lisani, nawe ukanipa yako
    Natamani kuya kwako, lakini sina idhini
  2. Dalili ya kutamani, nawe waifahamia
    Uningizile moyoni, siwezi kuvumilia
    Ndipo hafanya huzuni, shughuli ikaningia
    Kwako natamani kuya, lakini sina idhini

 

Muyaka Bin Haji Al Ghassany

Limeletwa Zanzinet na Maher Fundi

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  13 March 2004

  1. Ulitakalo wafanya, halihitaji idhini
    Fanya kama panya, kutafuna kwa imani
    Wala usione haya, mapenzi yatakulani
    Mahaba yanahikaya, hukufanya hamkani.
  2. Mapenzi sumu ya nyoka, yakikupamba hutoki
    Mndu utaita choka, furusadi shokishoki
    Akiitaka talaka, machozi tabu kutoka
    Lakufanya kwenda Makka, huenda ukaokoka.
  3. Mengi tunayatamani, kuyapata si rahisi
    Leo wawa nyani, kesho wageuka ngisi
    Ulimwengu mtihani, si wengi wanaopasi
    Walobaki ni kulani, nakutwangana risasi.

 

Hashil S. Hashil

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  13 March 2004

  1. Idhini simali kitu, mapenzi sumu katili
    Haraka njoo kwetu, kwa nini wakaa mbali?
    Hapa kwetu ni kwetu tu, ni lazima ukujali
    Njoo nakwita njoo, Njoo nakutamani.
  2. Idhini uisemayo, sidhani kama dharura
    Idhini uitakayo, ni nani aloipora?
    Idhini niijuayo, unayo tena ni bora
    Njoo nakwita njoo, Njoo nakutamani.
  3. Laiti utaamua, kuja kwetu japo mara
    Moyoni nitapungua, majonzi yanonikera
    Kusita kwako tambua, moyoni waniparura
    Njoo nakwita njoo, njoo nakutamani
  4. Njoo nakwita njoo, mwenzako nnaumia
    Usinitenge, njoo, wabaya wanirandia
    Unaibiwa, njoo, kwa haraka kimbilia
    Idhini wacha, njoo, njoo nakutamani

 

Mohammed Omar

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  14 March 2004

  1. Siko mbali ni njiani, ni njiani nnakuja
    Nakuja bila idhini, nione ulo yataja
    Ulotaja hadharani, ndio kubwa yangu haja
    Ingawaje siamini, lakini kwako nakuja
  2. Umenijaza tamaa, na hamu ya kukuona
    Shauku imenivaa, siwezi kungoja sana
    Kwangu ishatimu saa, subira sinayo tena
    Nnatamani kupaa, niruke tuje kutana

 

Maher

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  16 March 2004

  1. Lau kama huamini, kwanini ukathubutu
    Unatarajia nini, kama hujajidhubutu
    Hujalazimishwa sini, uje unifuate kwetu
    Ndoo wangu mwandani, moyo umeota kutu
  2. Ndoo kwa kuridhia, ndipo nitafurahika
    Sio kunisumbulia, kwa vile uliniweka
    Sasa hebu angalia, waja wasije kucheka
    Ndoo japo chungulia, moyo upate pozeka
  3. Idhini nani atowe, wakati tulishabana
    Nilikuwa mimi nawe, ahadi tulopeana
    Tukakamatana ndewe, muhali kupoteana
    Ndoo usichelewe, utimize uungwana

Said Paul

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  16 March 2004

  1. Kujaribu si makosa, kosa pale kirudia
    Nami siviwezi visa, sifanyi kukusudia
    Lakini unanitesa, hujuwi, nnakwambia
    Ndipo haomba ruhusa, na hali kukulilia
  2. Mara ngapi mekuomba, na miguu kukushika
    Ukaniona naimba, kila nnalo tamka
    Ukawa unanitimba, wanifanyia dhihaka
    Ulivyo kinitirimba, si sahau nakumbuka
  3. Moyo hauna pengine, uko kwako umependa
    Hauja ona mwengine, ambaye amekushinda
    Kwa uzuri si jengine, wanimaliza nakonda
    Nnakuja nikuone, na woga sije nitenda

Maher

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  16 March 2004

  1. Ukweli umeusema, kosa kurudia kosa
    Sitayarudia tena, makosa na kukutesa
    Shahidi wangu Rabana, nimebadilika sasa
    Njoo sifanye visa, yaliyopita si ndwele
  2. Ni dhahiri nilonena, utani meweka kando
    Nawe utakujaona, nadharia na vitendo
    Mapenzi yalo mwanana, si yale yenye vishindo
    Njoo ewe kijana, njoo ujionee
  3. Mapenzi ni pande mbili, ikiwa munapendana
    Mapenzi si ukatili, wala si kukomowana
    Mapenzi ni kukukubali, mazuri kutendeana
    Njoo sifanye khiana, njoo sikae mbali
  4. Na mimi ni kama wewe, jinsi nnavyokupenda
    Wala sina mwenginewe, awezae kukushinda
    Njoo sinisumbuwe, silali, sili, nakonda
    Njoo sifanye inda, njoo usichelewe.

Mohammed Omar

Laiti Siwele Nyuni!

Date:  17 March 2004

  1. Hukuondoshwa na miye, hapo ulipoondoka
    Wemfuata apitaye, mimi ukanitoroka
    Yanini nikuzuiye, na hali ushanichoka
    Haona nivumiliye, wema utaukumbuka
  2. Madhila yanifika, nikalitafuta tanga
    Waja wenisusuika, nikakihama kiunga
    Kila pembe neisaka, nayatafuta maganga
    Kidogo ningelifika, kuwatukana wakunga
  3. Wako moyo niuenzi, tusahau yalopita
    Uje niujaze penzi, la utamu wa kashata
    Ila usifunge tanzi, ni rahisi kulivuta
    Funga fundo la hirizi, liwe gumu kukeketa
  4. Njoo kifua mbele, bado nakuhitajiya
    Uchome kama mshale, ardhini ulongiya
    Yaliyopita si ndwele, muhimu yalobakiya
    Tupendane kwa milele, na tusafiane niya

Said Paul

Kutoka kwa Muyaka bin Hajia: Ushukuru!

Date:  28 March 2004

  1. Namshukuru Karima, ndiyo hali ya duniya
    Kiumbe hupata mema, mawi yakamwondokeya
    Kaongezewa rehema, milele kumshukiya
    Nami yamenifikiya, kupata hivi si haba
  2. Nami yamenifikiya, sina nisilofahamu
    Mashaka yalonijiya, yali mazito magumu
    M'ngu kaniondoleya, mwishowe hatabasamu
    Namshukuru Karima, kupata hivi si haba
Tafsiri yake: SHUKURANI
  1. Namshukuru Sattari, Mola asiye shirika
    Mtu hupata mazuri, maovu yakamwepuka
    Akaongezewa kheri, kwa miyaka na mikaka
    Na mimi yamenifika, nilichopata si tembe
  2. Na mimi yamenifika, sina nisiloelewa
    Mashaka yalonitweka, si mapesi kutukuwa
    Mwisho nilifurahika, kwa M'ngu kuyaondowa
    Namshukuru Moliwa, nilichopata si tembe

Maher

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet