|
|
Metanzwa na Kiswahili
Date: 02 June 2004
- Yanitatiza tatiza, lugha yetu Kiswahili
Maneno kukaza kaza, kurudia mara mbili
Silabi kujaza jaza, na kuonyesha kejeli
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Mifano ninayo mingi, ya maneno mara teni
Naanza na rangi rangi, neno hili sio geni
Angalia na shangingi, mnipe yenu maoni
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Nakupa na omba omba, uzidi kutafakari
Kuna kujikomba komba, si jambo la ufahari
Kwa nini zije sambamba, silabi zilovinjari
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Kuchochota si kuwasha, nakutaka ufahamu
Kuchachata na kuosha, vyalingana ki-isimu
Kukeketa, kutonesha, vyaweza kutoa damu
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Kupita pita kwa inda, vijumbani tachukiza
Kusita sita kutenda, ni ishara ya kuviza
Kukokota sio kwenda, ni sawa na kuburuza
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Mifano niliyoronga, itizame kwa mapana
Sio ninaunga unga, ithibiti yangu dhana
Lugha hii na kutunga, ni vitu vya kufanana
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Yako maneno asili, sauti zinalingana
Ni mengi sio kalili, hutumiwa kwa bayana
Ya awali na ya pili, silabi huongozana
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Gugusa ni moja wapo, linanipa wasiwasi
Dodosa nipe michapo, ukiipata nafasi
Papasa bado niwapo, nakusanya karatasi
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Naomba unidhukuru, msaada wa sarufi
Vipi neno msururu, lizirudie herufi
Na pia neno chururu, silabi zapiga kofi
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Usidhani nahariri, maneno ya maradufu
Ni mkubwa utiriri, orodha yangu ni ndefu
Si rahisi kukariri, bila kupata uchofu
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
- Ninaitua kalamu, nimefikia tamati
Lakini ninayo hamu, kuzipata zenu beti
Nipeni yenu matamu, msifanye ati ati
Metanzwa na Kiswahili, mwenzenu nisaidieni
Kassim O. Ali
|