.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

MTUKUFU RAMADHANI

 

Related links

 

MTUKUFU RAMADHANI

Date: 14 October, 2004

  1. Bismillahi naanza, kwa jina lake muweza,
    Nilo nayo kueleza, mupate kuyasikia,
    Ya muhimu kuwajuza, na ya kheri kuyajua,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  2. Mtukufu Ramadhani, sasa kishatufikia,
    Tumjue kwa makini, kuwa ni kujizuia,
    Kutia kitu kinywani, na maasi yote pia,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  3. Tufunge kwa lengo lake, ucha Mungu kufikia,
    Pia umuhimu wake, tupate kuutambua,
    Tuzipate radhi zake, kwa kutekeleza Twaa,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  4. Mwezi huu Qur'an, ndio imetushukia,
    Kafaradhisha Manani, kwa watu kujifungia,
    Nguzo zake kwa yakini, nia na kujizuia,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  5. Nia kila Isilamu, moyoni kukusudia,
    Kujizuia muhimu, alfajiri sawia,
    Hadi jioni kutimu, bila ya kuingilia,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  6. Katika yaliyo Sunna, ni kufuturu mapema,
    Na daku usiku sana, na Qur'an kusoma,
    Na kuwa karibu sana, na kwa swala kusimama,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  7. Kufanya mema muhimu, na miezi ilosalia,
    Kwa kutafuta elimu, na swala kujiswalia,
    Zaka na hija kutimu, kila ovu kuondoa,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.
  8. Kama unalazimika, mwezi ukiusikia,
    Ufunge bila mashaka, hadi siku kutimia,
    Viwanjani kufurika, Iddi kwenda jiswalia,
    Karibu mgeni wetu, mtukufu Ramadhani.

EYE WITNESS

 

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet