.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

NATAMANI

 

Related links

Date: 22 November, 2004

Nimelipenda sana shairi hili kwa kitu kimoja: beti ya mwisho imekusanya maudhui yote ya beti tatu za mwanzo kwa ustadi mkubwa sana! Hapa ndipo, chambilecho waingereza, wanapotafautishwa, "boys from men"!

Hili shairi ni zito kama nanga ya meli! Mtindo huu sijapata kuuona kwenye mashairi yote niliyowahi kuyasoma. Na ujue kuwa nimeshasoma mashairi mengi sana! Mtindo huu wa kuandikwa beti kama chane za ukili - ubeti mmoja mmoja, kwa maudhui yake - kisha zikapakaswa chane hizo zikaingia zote kwenye ubeti (ukili) mmoja wa mwisho, hakika umenifurahisha sana!

Hassan Omar Ali

Dallas.

NATAMANI

  1. Madamu maji mtoni , Daima yachuruzika
    Hata na ije tufani , Mwishowe huburudika
    Mto kwa kujiamini , Kwa pozi huteremka
    Na pendo langu jamani , Hasha halitanyambuka
    Mto kaukausheni , Ndiyo pendo takauka
  2. Madamu bustanini , Mauwa yanachanuka
    Jua na mvuwa si shani , Mauwa yatachipuka
    Vipepeo kitaluni , Haweshi kurukaruka
    Na pendo langu juweni , Muhali kupukutika
    Bustani zivunjeni , Ndiyo pendo tavunjika
  3. Madamu nyota angani , Kote zimechawanyika
    Hata lije wingu gani , Mwisho wingu huondoka
    Nyota hubaki makini , Huzidi kunawirika
    Na pendo langu yakini , Katu halitotoweka
    Nyota kaziangusheni , Ndiyo pendo taanguka
  4. Nikupendae moyoni , Powa usitie shaka
    Kwenye mto ukingoni , Nakusubiri kufika
    Twende kwenye bustani , Pendo lizidi pambika
    Na huku nyota mbinguni , Sisi zinatumurika
    Natamani natamani , Siku ifike haraka

KIITIKIO

Nikupendae moyoni , Powa usitie shaka
Natamani natamani , Siku ifike haraka

Shairi : Saleh M. Barkey

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet