.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

NIMLE VIPI SAMAKI

 

Related links

NIMLE VIPI SAMAKI

Date: 22 November, 2004

  1. Nawauliza malenga, ninyi mlio bobea,
    Magwiji kutoka Tanga, na hata wa kule Pemba,
    Unguja Mbeya Igunga, swali ninawatolea,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  2. Nimempata Mwaloni, ni pale Mwanza sokoni,
    Ninaye hapa jikoni, mwenzenu ninabaini,
    Ninayo njaa tumboni, samaki namtamani,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  3. Magamba nimeparua, namwandaa samaki,
    Na tumbo nikatumbua, nikapata taharuki,
    Hewa akaichafua, nikapigwa tahamaki,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  4. Njaa miya inauma, moyo konde nikapiga,
    Ndipo mimi nikasema, nitaandaa mafiga,
    Na nitampika vyema, nikaondoa uwoga,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  5. Limao nikanyunyiza, saumu na pilipili,
    Nikadhani nimeweza, samaki kumkabili,
    Nimewazoea pweza, hawahitaji shubili,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  6. Wala sikufua dafu, juhudi hazikufaa,
    Na ilizidi harufu, pote ilitapakaa,
    Imezidi maradufu, nimebaki kushangaa,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  7. Nimejipikia wali, na uko kwenye sinia,
    Naandaa maakuli, samaki namhofia,
    Dua zangu nikasali, na uma nitatumia,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  8. Nikamleta kinywani, harufu ikazidia,
    Amenishinda jamani, miye ninawakiria,
    Nifanye nini jamani, samaki nilopikia,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  9. Kijijini wanicheka, na wengine wamenuna,
    Na hamu imenitoka, njaa bado ninaona,
    Kipande kimedondoka, miye simtaki tena,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?
  10. Ninacho kichefuchefu, naweka mbali sahani,
    Imenishinda harufu, ya samaki wa Mwaloni,
    Sasa nimejawa hofu, samaki siwatamani,
    Nimle vipi samaki, samaki anayenuka?

Shairi la Mwanakijiji
Limeletwa na Walii Genderi.

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet